Na John Walter-Babati

Mwenyekiti wa mtaa wa Komoto Paskali Petro amesema atajiuzulu endapo mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Babati hatozipeleka fedha za fidia shilingi milioni 132 zilizolipwa na TANESCO kupisha Mradi wa gesi uliopita katika eneo la shule ya Msingi na Sekondari Komoto zilizopo katika mtaa huo.

Mwenyekiti huyo ameeleza hayo mbele ya mkuu wa mkoa wa Manyara Makongoro Nyerere aliyeambatana na mkuu wa wilaya ya Babati Lazaro Twange kusikiliza malalamiko ya viongozi na wananchi wa Mtaa wa Komoto kuhusu fedha hizo.

Amehoji kwanini mkurugenzi akae na madiwani kugawa fedha za mtaa wa Komoto, kwamba jambo hilo halikubaliki kwani shule ni mali ya Umma ambao ni wananchi wa mtaa huo?

“Kama kuna vinginevyo basi leo niambiwe kwa maandishi ili niwaambie wananchi wa Mtaa wa Komoto kuwa shule ni mali za Mkurugenzi, na kauli hii mkurugenzi aliwahi kunitamkia kwamba shule ni mali yangu na ninaweza kupeleka pesa popote ninapotaka”alisisitiza Mwenyekiti huyo

Ameongeza kuwa shule hiyo ya Msingi Zaidi ya miaka kumi haijawahi kupatiwa ruzuku aidha kutoka kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri au serikali kuu. ”Iweje leo mkurugenzi atumie fedha ambazo zimepita kwenye eneo la shule,imeathiri eneo la shule,hiki kitu hakiwezekani”

Amesema kama atapatiwa taarifa kwa maandishi yupo radhi na hatosumbuka na kwamba atawaambia wananchi kuanzia leo naomba nijiuzulu niachane na hizi shughuli ili serikali ifanye inayoyajua kwa kuwa wamefanyiwa uonevu.

“Haiwezekani watoto wetu wanakaa kwenye vumbi,mbao zinawaangukia hata hela ya ukarabati tusipate, naomba kupewa kwa maandishi na nilishwahi kumwambia DAS anipe maandishi kwamba shule kwamba shule ni mali ya mkurugenzi,ameshindwa kunipa” alimwambia Mkuu wa mkoa

Akitoa taarifa kwa mkuu wa mkoa na wajumbe wa Mtaa wa Komoto kwa niaba ya Mkurugenzi wa Mji wa Babati Faustine Masunga amesema fedha hizo ziliingia kwenye akaunti ya Halmashauri ya Mji wa Babati na zimeshatumika katika miradi mbalimbali ya maendeleo.

Masunga amesema mkurugenzi aliziwasilisha taarifa ya fedha hizo kwenye vikao vya Halmashauri na baadae baraza la Madiwani kuamua ambapo fedha hizo za fidia ziligawanywa kwenye kata mbalimbali ambapo kata ya Babati ilipewa Milioni 30,Bagara Milioni 30,Bagara Milioni 30,Maisaka Milioni 50,Mutuka Milioni 30, Sigino Milioni 30,Bonga Milioni 30,Singe Milioni 30 na Nangara Milioni 50.

Baadhi ya wajumbe katika serikali ya mtaa huo wamesema fedha za fidia zimepelekwa sehemu ambazo sio sahihi na kwamba zingepaswa zielekezwe moja kwa moja katika mtaa huo ili zisaidie kukarabati shule hizo mbili zenye upungufu wa madarasa na miundombinu mingine.

Mkuu wa mkoa wa Manyara Makongoro Nyerere amewataka Viongozi wa mitaa na vijiji katika mkoa huo ambao wamepitiwa na miradi kwenye maeneo yao yenye taasisi, wafuatilie fidia zao wanazostahili kulipwa kwa kufika katika ofisi za mkuu wa wilaya husika ili kufanyiwa kazi.

“Msiache kuja kufuatilia fedha za fidia,wito wangu ni kwamba viongozi wa mitaa,vijiji mkoa wote wa Manyara kama kuna fidia inatakiwa kutolewa na hamjapewa, msikate tamaa,fikeni toeni taarifa ofisi ya DC wa wilaya husika,matumaini yangu litafanyiwa kazi na endapo itachukua muda mrefu njooni kwangu” alisema Nyerere

Makongoro Nyerere akizungumzia mzozo uliopo Komoto baada ya fedha za fidia walizopaswa kupatiwa kugawanywa katika maeneo mengine,amesema taarifa alizipata kupitia viongozi wa mtaa huo na anaendelea kuzifanyia kazi

Licha ya fedha hizo kutolewa kwa ajili ya shule mbili za Komoto Sekondari na Komoto Msingi wajumbe hao wameshangazwa na kitendo cha kugawanywa na kupewa shilingi milioni 30 kinyume na matarajio yao.

Fidia iliyolipwa na TANESCO ni milioni 132 ambapo Shule ya Sekondari Komoto ilipaswa kulipwa shilingi Milioni 103 huku ya msingi ikitakiwa kupewa Milioni 29.

Mkuu wa mkoa wa Manyara Makongoro Nyerere 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...