Jaji Athumani Matuma Kirati akizungumzia hali ya utoaji  haki Katika Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, kwa Makatibu Wakuu, ( Sifuni Mchome, John Jingu na Christopher Kadio )  hawapo pichani. Pamoja na  mambo mengine,  Jaji Kirati alielezea uhaba wa mawakili wa serikali na waendesha mashtaka unavyowakwamisha  katika utekelezaji wa  majukumu yao  ya utoaji wa haki kwa wakati. Makatibu  Wakuu hao walikuwa katika ziara ya kikazi  katika mikoa ya  Tabora,  Kigoma na Kagera,



Na Mwandishi Maalum, Kagera

IDADI ndogo ya Mawakili wa Serikali, wakiwamo Waendesha Mashtaka katika baadhi ya Mahakama Kuu za Kanda, kumeelezwa kuwa moja ya changamoto zinazokwamisha utekelezaji wa utoaji hakijinai.

 Hali hiyo imebainika wakati wa ziara ya kikazi ya Makatibu Wakuu watatu wakiongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Profesa Sifuni Mchome katika Mikoa ya Tabora, Kigoma na Kagera.

Jaji Athumani Matuma Kirati wa Mahakama Kuu Kigoma, aliwaeleza Makatibu Wakuu hao kwamba, ukamilishaji wa idadi ya kesi ambazo wamejipangia unaathiriwa sana na uchache wa Waendesha Mashtaka na Mawakili wa Serikali.

“Sisi katika Mahakama Kuu Kigoma, tumejipangia utararibu wetu wa ndani wa kumalisha kesi tulizo nazo kwa muda, na tunakwenda vizuri sana kuanzia hapa Mahakama Kuu mpaka mahakama za chini. Lakini tunashikwa mashati na wadau wetu wakiwamo waendesha mashtaka ambao ni wachache, tunaomba msitushike mashati ili tufikie malengo yetu tuliyojiwekea” akasema Jaji Athumani Kirati.

Jaji Kirati anakwenda mbali kwa kueleza kwamba, katika Jengo lao jipya wametenga Ofisi kwaajili ya Mawakili hao wa Serikali, lakini Ofisi zimekuwa tupu kwa kuwa hakuna mawakili wa serikali na kama wapo basi ni moja, jambo analosema linakwamisha si tu katika uendeshaji wa mashataka bali hata pale unapotakiwa ushauri wa kisheria. Uchache wa Waendesha Mashtaka katika Mkoa wa Kigoma, pia ulichagiwa na Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Kanali Isack Mwakisu ambaye alisema Mahakama ya Hakimu Mfawidhi Kasulu ina mahakimu watatu lakini waendesha mashtaka wawili na hivyo Hakimu mmoja anashindwa kufanya kazi ipasavyo.

“ Tutafurahi sana kupata mawakili wa serikali wa kutosha , na wilaya yangu ipo tayari kuaanda mazingira mazuri ya ufanyaji kazi” akabainisha Kanali Mwakisu, Naye Dkt Ntemi Kilekamajenga, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Bukoba, amesema.

Kanda hiyo ina waendesha mashataka na mawakili wa serikali wachache hali inayokwamisha utekelezi wa majukumu yao.

Amesema kwa mfano kitakapo anza kikao maalumu ya kusikiliza kesi mapema mwezi ujao, baadhi ya Mahakama zitashindwa kuendesha kesi kwa kukosa mawakili wa serikali kwani wachache waliopo watakuwa katika vikao hivyo maalum.

“ Tunaiomba serikali iajiri mawakili wa seriali wa kutosha ili tusikwame, hawa ni watu muhimu hatuwezi kuendesha kesi bila wao, na tutakapoanza vikao maalum hapana shana mahakimu wengine hawataweza kuendelea na kesi zao, tunaomba tusaidiwe katika hili.

Kwa upande wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, kuna waendesha mashtaka wanane (8) ikilinganishwa na idadi ya mahakimu na mwanasheria mmoja wa Serikali, hali ambayo nayo imetajwa kuchelesha utoaji wa haki.

Mikoa ya Tabora, Kigoma na Kagera ni mikoa ambayo inamuingiliano mkubwa wa watu kutoka nchi za jirani, lakini pia ina idadi kubwa ya kesi za jinai zikiwamo za mauaji, migogoro ya ardhi, ubakaji, na wahamiaji haramu kutoka nchi jirani.

Akijibu hoja hiyo ya uhaba wa mawakili wa serikali, Katibu Mkuu Sifuni Mchome, amesema Wizara imeomba kibali cha kuajiri mawakili wa serikali na wanasubiri jibu.

Aidha pamoja na changamoto mbalimbali zikiwamo za uendeshaji wa mashauri kwa kupitia mfumo wa TEHAMA, mfumo ambao ulielezwa na Majaji hao kwamba bado unachangamoto kadhaa zikiwamo za magereza kukosa vifaa vya TEHAMA na uhafifu wa mtandao, Katibu Mkuu amezipongeza Mahakama katika mikoa hiyo kwa utekelezaji mzuri wa umalizaji wa kesi.

Vile vile amesifu ushirikiano baina ya Taasisi ambazo zinahusika na mnyororo wa utoaji haki,huku akisisitiza kwamba, ushirikiano uendelezwe pasipo kuingiliana katika utekelezaji kazi wa kila Taasisi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...