KATIKA Kuelekea maadhimisho ya Miaka 60 ya Uhuru Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC,) kwa kushirikiana na na vyombo vya habari vya Mwananchi Communications, Clouds Media Group (CMG,) na Wasafi Media wamesaini mkataba wa makubaliano katika kuadhimisha miaka 60 ya Uhuru na kuzindua nembo itakayotumika muda wote wakati wa utekelezaji wa maadhimisho hayo kwa kauli mbiu ya '60- Pamoja Tanzania Tena na Tena.'

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa TBC, Mratibu wa Masoko na Vipindi wa shirika hilo Gabriel Nderumaki amesema, vyombo hivyo vinne kwa pamoja wameanzishaa ushirikiano wa kuandaa maudhui na matamasha mbalimbali katika kuadhimisha miaka 60 ya uhuru inayoadhimishwa Desemba 9, kila mwaka.

Amesema, lengo la ushirikiano huo ni kuunganisha Watanzania na dunia nzima katika kusherehekea miaka 60 ya uhuru, kuhamasisha uzalendo pamoja na kutumia changamoto na fursa zilizopita kwa ajili ya kutengeneza mustakabali utakaoleta tija kwa jamii.

'' Maadhimisho haya pia yamelenga kukuza tamaduni na mila zetu ndani ya miaka 60, pamoja na kuwakumbusha watanzania juu ya maadui watatu walioainishwa na Baba wa Taifa na changamoto zinazilikabili Taifa kwa sasa.''

Aidha amesema kuwa, ushirikiano huo umelenga kuwakumbusha watanzana juu ya mchango wa Tanzania katika Ukombozi wa bara la Afrika na kuendelea kulinda amani ya mataifa mengi duniani.

Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa Clouds Media Joseph Kusaga amesema, katika ushirikiano huo watakusanya taarifa za uhuru wa nchi katika kipindi cha miaka 60 kutoka kwa watu mbalimbali kwa kutumia teknolojia ya kisasa ili kuwafikia watu wengi zaidi hususani vijana.

Kusaga amesema TBC imetengeneza njia kwa vyombo vingi vya habari kwa muda mrefu na ushirikiano huo pia umelenga kuunga juhudi za Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassani katika kujenga Taifa imara na muunganiko wa vyombo hivyo vinne ni sherehe ya kihistoria ya kulipeleka mbele zaidi.

''Tunatarajia mengi kupitia ushirikiano huu hasa kujenga uelewa wa watanzania juu ya uhuru wa nchi yetu na mambo mbalimbali ikiwemo magonjwa, afya, umuhimu wa kuenzi uhuru wa Taifa pamoja na tamaduni.'' Amesema Kusaga.

Vilevile Mkurugenzi Mtendaji wa Mwananchi Communications Limited Bakari Machumu amesema, kampuni hiyo ilianza kuchapisha Makala kuelekea siku ya uhuru na wamekuwa wakifikia watu milioni 20 kwa mwezi na kupitia ushirikiano huo ni matarajio yao watu zaidi ya milioni 100 watafikiwa na kupata elimu ya siku ya uhuru wa Desemba 9.

Mkurugenzi wa vipindi kutoka WASAFI FM, Nelson Kisanga amesema kupitia ushirikiano huo na kuelekea katika maadhimisho hayo shughuli mbalimbali zitafanyika ikiwemo mashindano ya mpira wa miguu kwa timu za Taifa Stars na Twiga Stars utakaochezwa Desemba 4 katika uwanja wa Uhuru jijini Da es Salaam, matamasha ya Muziki wa wasanii kuanzia uhuru hadi sasa, mbio za Marathon zitakazofanyika Desemba 5, midahalo na kuhitimisha maadhimisho hayo kwa kupanda mlima Kilimanjaro kuanzia Desemba 5 hadi 9.

Kisanga ameomba watanzania na wadau wengine vikiwemo vyombo vya habari kushiriki katika mchakato huo wa kuelekea maadhimisho ya miaka 60 ya uhuru.




Wakurugenzi wa vyombo vinne vya habari vya TBC, Clouds Media, Mwananchi Communications na WASAFI Media wakikata utepe kuashiria makubaliano ya ushirikiano wa kuadhimisha miaka 60 ya uhuru na kuzindua nembo maalumu itakayotumika kwa muda wote wa utekelezaji wa maadhimisho hayo, leo jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mtendaji wa Clouds Media Group (CMG,) Joseph Kusaga akizungumza wakati wa hafla hiyo ya makubaliano baina ya vyombo vinne vya habari kuelekea maadhimisho ya miaka 60 ya uhuru, Kusaga amesema ushirikiano huo ni muhimu katika kuleta hamasa ya jamii hasa vijana ambao wanahitaji kujua Taifa lilipotoka lilipo na linakoelekea kiuchumi, jamii, mila na tamaduni. Leo jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mtendaji wa Mwananchi Communicaations Limited Bakari Machumu akizungumzaa wakati wa hafla hiyo ya makubaliano na kueleza kuwa gazeti la Mwananchi Septemba 9 lilianza rasmi kuchapisha makala na kuandaa makongamano Septembea Mosi mwaka huu, leo jijini Dar es Salaam.




Matukio mbalimbali wakati wa hafla hiyo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...