Jeshi
la Polisi Mkoa wa Mbeya linawashikilia watuhumiwa wawili 1. LIPANDE
SAID @ SIMWICHE [62] na 2. JUMA PIUS [32] wote wakazi wa Kapyo wilayani
Mbarali mkoani Mbeya kwa tuhuma za kupatikana na nyara za serikali
vipande saba [07] vya Meno ya Tembo.
Watuhumiwa
walikamatwa tarehe Oktoba 20, 2021 majira ya saa 10:00 asubuhi huko
Kijiji cha Kapyo kilichopo Kata ya Igurusi, Tarafa ya Ilongo, Wilaya ya
Mbarali baada ya Jeshi la Polisi mkoani hapa kupata taarifa za siri na
kisha kufanya msako na upekuzi nyumbani kwa mtuhumiwa LIPANDE SAID @
SIMWICHE na kufanikiwa kukuta nyara hizo zikiwa zimefichwa kwenye mfuko
wa sandarusi.
Aidha
katika upekuzi huo, watuhumiwa walikutwa wakiwa na nyara nyingine za
serikali ambazo ni kipande cha Ngozi ya Fisi Maji nacho kikiwa
kimefichwa kwenye mfuko wa sandarusi.
Vipande
hivyo saba vya Meno ya Tembo vina uzito wa kilogramu 33 na thamani ya
Tshs. Milioni Sitini na tisa laki mbili kumi na nne elfu mia nne na kumi
[Tshs.69,214,410/=] huku ikikadiriwa kuwa Tembo waliouawa ni wawili.
Upelelezi
wa shauri hili unaendelea na mara baada ya kukamilika watuhumiwa
watafikishwa mahakamani kwa kosa la kupatikana na nyara za serikali
kinyume cha sheria ya Wanyamapori ya mwaka 2009 kifungu namba 86 na kosa
la uhujumu uchumi kinyume cha sheria ya uhujumu uchumi ya mwaka 2019
kifungu namba 57 (First Schedule).
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...