Na. Paschal Dotto-MAELEZO
Waziri wa Habari, Mwasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Ashatu Kijaji amesema kuwa
Serikali itaendelea kushirikiana na kufanya kazi na vyombo vya habari katika
kutangaza mambo mbalimbali yanayofanywa
na Serikali kwa watanzania.
Akizungumza katika Mkutano wake na Wahariri wa Vyombo vya
Habari nchini, Waziri Dkt. Kijaji
amesema lengo la Serikali ni kujenga uimara wa vyombo hivyo ili viweze
kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi katika kuwaelimisha, kuburudisha na
kutangaza mandeleo ya nchi kwa wananchi.
“Ndugu Wahariri lengo la Mkutano huu ni kujitambulisha kwenu kwani tangu
niteuliwe, Jambo hili ni muhimu hususan baada ya Mhe. Rais kuamua kwamba tasnia
ya Habari sasa isimamiwe na Wizara yangu na kuunda Wizara Mpya yaani Wizara ya
Habari, Mawasiliano, na Teknolojia ya Habari, kwa hiyo ndugu wahariri ninaomba
ushirikiano katika kukuza hii tasnia”, Alisema Dkt. Kijaji.
Dkt Kijaji alisema
kuwa ushirikiano wa Vyombo vya Habari na Wizara ya Habari, Mawasiliano na
Teknolojia ya Habari ni tunatimiza takwa
la kisheria Ibara ya 18 ya Katiba ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambayo inatamka kuwa kila mtu yuko huru
kutoa maoni na kutoa mawazo yake, kutafuta, kupokea na kutoa habari kupitia
chombo chochote bila ya kujali mipaka ya nchi.
Aidha Dkt. Kijaji alivishukuru Vyombo vya Habari nchini kwa
kuendelea kuelimisha na kutoa
ushirikiano katika changamoto kubwa ya UVIKO 19, ambapo aliwataka
waendelee kufanya kazi kwa weledi ili wananchi wapate elimu na kuchukua maamuzi
sahihi ya kuchanja na kujikinga na madhara ya janga hilo.
Katika hatua nyingine Dkt. Kijaji alisema kuwa ushirikiano
wa Vyombo vya habari na Serikali kupitia Wizara yake ni moja na nguzo muhimu
katika kuendeleza sekta hiyo kwani ni sekta ambayo kwa kiasi kikubwa ndiyo
inafanya wananchi kupata taarifa ya utekelezaji wa miradi na mambo mbalimbali
ya Serikali, lakini pia inaonyesha wadau wa maendeleo nini Serikali inafanya.
“Pamoja na juhudi
kubwa mnayoifanya, naendelea kuwaomba ushirikiano mkubwa kutoka kwenu ili
tuweze kuindeleza sekta ya habari hapa nchini na kutangaza masuala muhimu na
mazuri yanayofanywa na Nchi yetu ikiwa ni pamoja na miradi mbalimbali
inayotekelezwa na Serikali, Wadau wa Maendelo na Wananchi wetu kwa ujumla
wao”Alisema Dkt Kijaji.
Kuelekea Maadhimisho ya Miaka 60 ya Uhuru, Dkt. Kijaji alieleza
umuhimu wa vyombo vya Habari katika kuelezea nchi ilikotoka, ilipo na
inapokwenda, ambapo kuelekea siku hiyo ya
tarehe 9 Disemba 2021, vyombo vya habari vinatakiwa kueleza maendeleo na
mambo mbalimbali yaliyofanyika tangu uhuru
Aliongeza kuwa kutokana na umuhimu wa sherehe hizo,
Watanzania wote hawana budi kujivunia
miaka 60 ya Uhuru wakiwa na amani na
maendeleo katika sekta mbalimbali
ikiwepo tasnia ya habari.
“Naomba nitumie fursa hii kuwaomba wanatasnia ya habari
kushiriki kikamilifu katika kutangaza shughuli zote zinazohusu Uhuru wa nchi
yetu kama sehemu muhimu ya kutoa elimu kwa Watanzania na dunia kwa ujumla.
Umoja wetu katika jambo hili utasaidia sana kuelimisha wananchi”, Alisema Dkt.
Kijaji.
Akijibu Swali lililoibuliwa na Wahariri, kuhusu Maagizo ya
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, Dkt. Kijaji
alisema kuwa maagizo yote yaliyotolewa na Rais Samia Suluhu Hassan kuhusu
kufunguliwa kwa media mbalimbali zikiwemo zile za magazeti na online za Wizara
inalifanyia kazi agizo hilo na atahakikisha anapata ufumbuzi hivi punde.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Zainabu
Chaula amevitaka vyombo vya Habari kufanya kazi kwa weledi na kwa kufuata
sheria kwani kwa kufanya hivyo tasnia itakua na kuwa na watalaam zaidi.
“ Waandishi wa Habari, tukifanya kazi kwa weledi hakuna kuvutana na fujo haziwezi kutokea, tukifanya kazi zinazotuhusu hakuna vurugu yeyote kwa hiyo tufanye kazi kwa kufuata sheria na kutumia taarifa vizuri ili kutoa taarifa za kuaminika”,
Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Dkt. Ashatu Kijaji akieleza jambo kwa wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari hapa nchini umuhimu wa vyombo vya habari katika kujenga taifa na kuketa ustawi wakati wa kikao chake na wahariri hao kilichofanyika leo Oktoba 25, 2021 Jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu Wizara ya
Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Dkt. Zainab Chaula akizungumza na
wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari leo Oktoba 25, 2021 Jijini Dar es
Salaam kuhusu mikakati ya wizara hiyo katika kuimarisha ushirikiano na vyombo
vya habari hapa nchini.
Naibu Katibu Mkuu
Wizara ya Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Dkt. Jimmy Yonazi akieleza
jambo wakati wa kikao cha pamoja kati ya Waziri wa Habari Mawasiliano na
Teknolojia ya Habari Dkt. Ashatu Kijaji leo leo Oktoba 25, 2021 Jijini Dar es
Salaam.
Mkurugenzi wa Idara
ya Habari MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali Bw. Gerson Msigwa akieleza kwa
wahariri kuhusu utayari wa Idara ya Habari kuendeleza ushirikiano uliopo na
vyombo vya habari hapa nchini kwa maslahi ya Taifa.
Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Dkt. Ashatu Kijaji akiwa kwenye picha ya pamoja na wahariri wa vyombo vya habari hapa nchini mara baada ya kikao chake na wahariri ha oleo Jijini Dar es Salaam
Wahariri wa vyombo
mbalimbali vya habari wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
Dkt. Ashatu Kijaji wakati wa kikoa chake na wahariri hao leo Oktoba 25, 2021
Jijini Dar es Salaam.
(Picha
zote na Idara ya Habari MAELEZO)
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...