KAMPUNI inayongoza ulimwenguni kwa usambazaji wa mbolea na utengenezaji wa virutubisho vya mazao, YARA, leo imezindua programu ya kidijitali kwa ajili ya wakulima ijulikanayo kama Yara FarmCare, ambayo inatoa taarifa sahihi za kilimo zinazostahili kutumiwa na mkulima, ikiwa na lengo la kuinua ufanisi katika kilimo, na kuchangia katika kujenga sekta ya kilimo inayojitegemea na wakati huohuo kuhakikisha kuwa wakulima wananufaika na uwekezaji wao.
Programu hii, ambayo inaweza
kupakuliwa kwenye Google Playstore, imetengenezwa mahsusi kwa ajili ya
kutatua changamoto zinazojitokeza kila mara katika shughuli za kilimo
kama ufanisi, upatikanaji wa faida,mabadiliko ya hali ya hewa,
ikizingatiwa kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa Tanzania,
kikichangia asilimia 25 ya Pato la Taifa (GDP), kikiajiri zaidi ya
asilimia 40 ya nguvukazi na asilimia 70 ya wakazi wa maeneo ya vijijini.
Akiongea katika hafla ya uzinduzi wa programu hiyo jijini Dar
es Salaam leo, Mkurugenzi Mtendaji wa YARA, Winstone Odhiambo,alisema
kampuni ya Yara inatambua kuwa mabadiliko ya hali ya hewa ni changamoto
inayowakabili wakulima misimu yote kwa sababu yana uwezo wa kupunguza
kiwango cha uzalishaji wa mazao, na kama hiyo haitoshi, inaweza
kusababisha ukame, vitu ambavyo vinapunguza pato halisi la kaya
mojamoja, kusababisha uhaba wa chakula na uwezo wa kifedha wa wakulima,
ambao ni takriban asilimia 70 ya wakazi wa vijijini.
Alisema
kuwa FarmCare ni chaguo sahihi ambalo linampa mkulima fursa ya kunufaika
na thamani halisi ya fedha yake kwenye kilimo, kwa kuwa program hii ina
nyenzo nyingi za kutumia kama vile daktari wa mimea, taarifa za hali ya
Hewa, kikokotoo cha mbolea, maelekezo sahihi sawa na ambayo angetoa
bwana shamba kwa kila hatua, na hivyo kuwasaidia wakulima kuzalisha
mazao bora zaidi ambayo nayo yanaongeza kiwango cha uzalishaji kwa eneo
lilelile.
“ Wakulima wanahitaji kuwa na msimamizi wa karibu kila
siku, mshauri, na mshirika ambaye anawahakikisha kuwa wanazalisha
kitaalamu zaidi,wanatumia njia sahihi za kilimo, ili kuondoa dukuduku
lao. Wanahitaji mbia awe nao muda wote, mtu ambaye wanaweza kumtegemea
kuwapatia suluhisho la matatizo na changamoto zao ili wajipatie fedha
zaidi, wapunguze matumizi wakati wa uzalishaji, yaani kwa lugha nyingine
wavune mazao mengi kwa kuwekeza kidogo zaidi,”alisema Mkurugenzi
Mtendaji Winstone Odhiambo.
FarmCare ni programu ya kidijitali
ambayo inagusa maswala mtambuka ya kilimo, iliyosanifiwa maalum
kuhakikisha kuwa mkulima wa Tanzania anakuwa si bora mkulima bali
mkulima bora haswa. Kwa kubonyeza tu vitufe vya simu janja, wakulima
wanajipatia ushauri bora kabisa wa wakati wa kupanda, ikiwa imesheheni
elimu ya uhakika ya kilimo na mbinu nyingi za kuinua ufanisi wa kilimo
kama shughuli. FarmCare ni nyenzo sahihi ya kilimo ambayo ina uwezo wa
kufanya mabadiliko kwenye sekta ya kilimo Tanzania na kukifanya kilimo
kuchukua nafasi na hadhi yake stahili kama msingi madhubuti wa uchumi.
Akizungumza
katika hafla hiyo, Meneja Masuluhisho ya Kidijitali, Deodath Mtei,
alisema “ Yara imeitikia kilio cha wakulima kwa wakati muafaka kwa
kuzindua FarmCare, ambayo ina manufaa lukuki ikiwemo elimu elekezi ya
kilimo kupitia video, orodha ya namna ya kutekeleza majukumu mbalimbali
ya kilimo na utabiri wa hali ya hewa. Ina nyezo mbalimbali zenye lengo
la kusaidia uzalishaji kama daktari wa mimea, , kipimo cha mbolea,
ramani ya shamba, na kitufe cha kutambua maduka ya pembejeo za Yara
yalipo. FarmCare ni program ambayo siyo tu inamsaidia mkulima, bali
inatoa zawadi na kuponi kwa njia ya mashindano.”
Program ya
FarmCare imezinduliwa ikilenga kuwa mwenza wa mkulima na nyenzo ya
uhakika ya kidijitali ya kutoa suluhisho mbalimbali za kilimo,
iliyosheheni taarifa na utalaamu wa hali ya juu ambayo mkulima anaweza
kuirejea wakati wowote anapohitaji kutatua changamoto za kila siku za
shughuli za kilimo msimu mzima.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mbolea ya Yara Tanzania, Winstone Odhiambo (kulia), akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa programu ya kidijitali kwa ajili ya wakulima ijulikanayo kama Yara FarmCare inayotoa taarifa sahihi za kilimo kwa lengo la kuinua ufanisi katika sekta ya kilimo nchini. Hafla hiyo ilifanyika jijini Dar es Salaam leo. Wanaongalia kutoka kushoto ni, Bwanashamba Mwandamizi wa Yara, Maulidi Mkima na Meneja Masuluhisho ya Kidigitali, Deodath Mtei.
Bwanashamba Mwandamizi wa Kampuni ya Mbolea ya Yara Tanzania, Maulidi Mkima (kulia), akizungumza wakati wa uzinduzi rasmi wa programu ya kidijitali kwa ajili ya wakulima ijulikanayo kama Yara FarmCare inayotoa taarifa sahihi za kilimo kwa lengo la kuinua ufanisi katika sekta ya kilimo nchini. Hafla hiyo ilifanyika jijini Dar es Salaam leo. Katikati ni Mkurugenzi Mtendaji wa Yara, Winstone Odhiambo na Meneja Masuluhisho ya Kidigitali, Deodath Mtei. Meneja Masuluhisho ya Kidigitali wa Kampuni ya Mbolea ya Yara Tanzania, Deodath Mtei (kushoto), akizungumza wakati wa uzinduzi rasmi wa programu ya kidijitali kwa ajili ya wakulima ijulikanayo kama Yara FarmCare, inayotoa taarifa sahihi za kilimo kwa lengo la kuinua ufanisi katika sekta ya kilimo nchini. Hafla hiyo ilifanyika jijini Dar es Salaam leo. Katikati ni Mkurugenzi Mtendaji wa Yara, Winstone Odhiambo na Bwanashamba Mwandamizi wa Yara, Maulidi Mkima.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...