Na Mary Gwera, Mahakama

Mahakimu Wakazi wapya wametakiwa kuwa waadilifu wakati wa kutekeza majukumu yao kwa kuzingatia kanuni za maadili za Maafisa wa Mahakama wanapotekeleza jukumu la msingi la utoaji haki.

Kauli hiyo imetolewa jana tarehe 17 Januari, 2022 kwenye ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki-Temeke Dar es Salaam na Jaji Mkuu wa Tanzania, Prof. Ibrahim wakati akiwaapisha jumla ya Mahakimu Wakazi wapya 29.

Alisema kuwa kazi ya uhakimu ni kazi inayoheshimika katika jamii hivyo inapaswa kuishi katika misingi ya kazi hiyo.

“Hakimu ni mtu mkubwa sana katika jamii na ndio maana amevikwa vazi la uheshimiwa, mnafanya kazi ambayo inaheshimika sana na jamii na inajaribu kukupa kila msaada ili uweze kutoa haki, hivyo inabidi kuenzi heshima hii kwa kuwa waadilifu katika kutoa haki,” alisema Mhe. Prof.Juma.

Aliwataka Mahakimu hao kusoma kanuni za maadili za Maafisa wa Mahakama kwa kuwa nyaraka hiyo ni muhimu kwa Majaji na Mahakimu na inatoa mwongozo katika masuala ya uadilifu.

“Ni vyema hata leo jioni mkipata nafasi muweke kikao na ndugu zenu msome kanuni hizo ili wasiwaingize mtegoni, ukisoma kwa makini kanuni hizo zinagusa hata ndugu zetu kwa sababu wanaweza kufanya jambo likachukuliwa ni sehemu yako ya uvunjifu wa maadili kwani wanaweza kufanya jambo kwa kutumia jina lako au kwa niaba yako" alisema Jaji Mkuu.

Aidha; Mhe. Jaji Mkuu aliwataka Mahakimu hao kuhakikisha wanatenda haki katika utekelezaji wa majukumu wao kwani wakikosea watakuwa wanachelewesha upatikanaji wa haki.

Katika hatua nyingine, Prof. Juma aliwaeleza Mahakimu hao kuzingatia uhuru wa Mahakama na kwamba hawataingiliwa na mtu yeyote ikiwemo Majaji katika utendaji kazi zao ikiwemo utoaji wa hukumu.

Pia amewataka Mahakimu hao kujiadhari, kujichanganya ya watu hovyo ikiwemo mitandao ya kijamii kama vile makundi ya ‘WhatsApp’ kwani wanaweza kuingia katika mtego wa kuongelea mambo ya Mahakama ambayo hawastahili kuzungumza.

Kwa upande wake Jaji Kiongozi, Mhe. Mustapher Siyani aliwaeleza Mahakimu hao kwamba, kazi yao inahitaji uaminifu vinginevyo hawatadumu na watakuwa wamekosea kuchagua kazi hiyo.

Idadi hiyo ya Mahakimu itasaidia kuongeza nguvu kazi ambayo itasaidia kupunguza mlundikano wa mashauri Mahakam ana hatimaye haki kupatikana kwa wakati.

Baada ya Mahakimu wa leo kuapishwa wamefika Mahakimu 1,369 ambao watasaidia kutoa huduma katika maeneo mbalimbali hapa nchini.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza katika hafla ya kuwaapisha Mahakimu Wakazi wapya 29 (hawapo pichani) katika ukumbi wa mafunzo uliopo katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kilichopo Manispaa ya Temeke Jijini Dar es salaam, jana tarehe 17 Januari, 2022.

Baadhi ya Mahakimu Wakazi wapya 29 walioapishwa wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani) akizungumza katika hafla ya Uapisho huo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...