Na. John Mapepele-WUSM


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mhe, Samia Suluhu Hassan ameipongeza Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa ubunifu na mikakati kabambe ya kuandaa matamasha mbalimbali ya sekta hizo yanayoleta tija kwa wananchi na kuielekeza kukaa pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii ili kuja na mkakati wa kuandaa matamasha bora zaidi ili yatumike kuitangaza Tanzania na kutoa ajira kwa wananchi.

Rais Samia ameyasema haya leo Januari 22, 2022 kwenye Uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi wakati akizindua Tamasha la Utamaduni la Mkoa wa Kilimanjaro lililoratibiwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Chama cha Umoja wa Machifu Tanzania kupitia Mwenyekiti wa Machifu Mkoa wa Kilimanjaro, Frank Mareale na Mkoa wa Kilimanjaro.

Mhe. Rais amesema, kutokana na umuhimu mkubwa wa Utamaduni aliamua kuunda wizara maalum ya Utamaduni, Sanaa na Michezo ili kutunza maadili, kuzalisha ajira na kukuza michezo na kuwachagua viongozi vijana kuongoza wizara hiyo ambapo amesisitiza kuwa wanaisimamia kwa ubunifu mkubwa.

Ameongeza kuwa katika kipindi kifupi Wizara imeweza kufanya mapinduzi makubwa kwenye sekta hizo na kutaka kuendelea kushirikiana na wadau ili kuboresha zaidi.

Ameyataja baadhi ya matamasha ya kihistoria ya utamaduni ambayo yameratibiwa na Wizara kwa ubunifu wa hali ya juu katika kipindi hiki baada ya Serikali yake kuingia madarakani kuwa ni pamoja na Tamasha la Utamaduni la Bagamoyo, Tanga, Tamasha la Machifu la Utamaduni la Mwanza na Morogoro.

Aidha, ameipongeza Wizara kwa kuandaa Mkutano wa machifu uliowakutanisha machifu wote jijini Dodoma na kuazimia kuwa na jukwaa la pamoja ambapo amefafanua kuwa yeye atakuwa Mwenyekiti wa jukwaa hilo.

Amesisitiza kuwa Serikali yake itaendelea kuimarisha bajeti ya Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo ili kuendelea kubaini, kulinda na kuendeleza utamaduni wa watanzania kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.

Naye Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Pauline Gekul amesema Sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo ni sekta mtambuka za nguvu ya kimkakati kwa taifa na zinatoa fursa ya ajira kwa vijana wengi.

Amemhakikishia Mhe. Rais kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano, ubunifu na weledi ili kuhakikisha malengo ya Serikali na Ilani ya Chama cha Mapinduzi yanatekelezwa kikamilifu.





 


 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...