Na Evelyne Mpasha, MBARALI
Wakulima wa zao la mpunga wilayani Mbarali Mkoani Mbeya wametakiwa kuongeza matumizi
ya mbegu bora zilizotafitiwa na Watafiti kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) ili
kuongeza tija katika uzalishaji wa mpunga na kuachana na kilimo cha mazoea ambacho tija yake
ni ndogo.
Wito huo umetolewa leo (2.07.2022) na Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Maendeleo ya Wilaya
ya Mbarali Bwana Geoffrey Mwaijobele wakati akifungua maonesho ya Kilimo Biashara cha
Mpunga yaliyoandaliwa na Kituo cha TARI Uyole kwa kushirikiana na Vituo vya TARI Dakawa na
TARI Ifakara pamoja na Shirika la Kimataifa la Utafiti wa Mpunga (IRRI). Maonesho hayo
yamefanyika katika Kata ya Ubaruku Wilayani Mbarali iliyoko mkoa wa Mbeya.
Katika hotuba yake, Mwaijobele ameipongeza TARI kwa kuleta matokeo ya utafiti wa zao la
Mpunga karibu na wananchi hususan katika Wilaya ya Mbarali na kutoa elimu kwa wakulima.
Elimu iliyotolewa katika maonesho ya kilimo biashara cha mpunga ni pamoja na sifa za mbegu
mpya za mpunga, maandalizi ya shamba, matumizi bora ya mbolea, palizi na hatua za uvunaji
hatua ambayo itasaidia wakulima wa Wilaya ya Mbarali na maeneo mengine yanayofaa kwa
kilimo cha mpunga kulima kisasa, kuwa na uhakika wa chakula na ziada ya kuuza kwa ajili ya
maendeleo yao binafsi na Taifa kwa ujumla .
Awali, Kaimu Mkurugenzi wa Kituo cha TARI Uyole ambaye Dkt. Denis Tippe alieleza kuwa
Kituo cha TARI Uyole kiliweka majaribio ya mbegu mpya sita katika skimu ya umwagiliaji Kata ya
Ubaruku Wilayani Mbarali ili kuongeza matumizi ya mbegu bora za mpunga na kuliongezea tija
baada ya kubaini changamoto iliyopo ya kushuka kwa tija katika uzalishaji wa zao hilo.
Dkt. Tippe aliongeza kuwa mbegu hizo mpya za mpunga za SARO 5, TARI RIC 1 & 2, Komboka,
SATO 1 & 9 ambazo zina sifa za kutoa mavuno mengi kuanzia tani 7.5 hadi 8.5 kwa hekta,
kunukia, kuwa na punje nzuri, kukomaa kwa muda mfupi na baadhi zinavumilia maeneo
yaliyoathiriwa na magadi na chumvi chumvi zimeonyesha kufanya vizuri katika majaribio
yaliyoandaliwa kwa ajili ya maonesho hayo ambayo yanalenga mkusaidia mkulima kuchagua
mbegu ambayo itamfaa kulingana na eneo lake.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa TARI aliyehudhuria maonesho hayo
Dkt. Richard Kasuga amesema maonesho hayo ni moja moja ya majukumu muhimu ya TARI ya
kuhakikisha teknolojia zinazotafitiwa zinawafikia wakulima na wadau wa kilimo kupitia njia
mbalimbali za mawasiliano ikiwemo maonesho ya kilimo biashara, vituo mahiri, vyombo vya
habari na mitandao ya kijamii. Aliongoeza kuwa matumizi ya mbegu bora za mpunga zitasaidia
kuongeza uzalishaji na hivyo kufikia malengo ya Serikali ya kujitosheleza kwa chakula na pia
Malengo ya yaliyoainishwa katika Azimio la Malabo la kukabilana na njaa.
Akizungumzia kazi kubwa inayofanywa na Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na
Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, Dkt. Kasuga ameongeza
kuwa katika mwaka wa 2022/2023 bajeti ya maendeleo ya utafiti imeongezeka kutoka takriban
bilioni 11 hadi billion 41.
Ameongeza kuwa, Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Hussein Bashe ameweka mkazo na malengo
ya AJENDA 10/30 yenye kaulimbiu KILIMO NI BIASHARA yenye lengo la kujitosheleza kwa
chakula na ziada kwa ajili ya kuuza na kujiongezea kipato, Hivyo maonesho haya ni fursa katika
kuwahamasisha wakulima kutumia fursa za masoko ambalo Wizara imeendelea kuyatafuta
ikiwemo la Ubeljiji kwa ajili ya kuuza mchele.
Katika hatua nyingine, baadhi ya wakulima wa zao la mpunga Wilayani Mbarali wameipongeza
na kuishukuru TARI kwa kuwezesha kuweka majaribio ya mbegu mpya za mpunga Wilayani
humo na kuuomba Uongozi wa Wilaya ya Mbarali kuwaletea wataalamu wa TARI karibu yao ili
waweze kuwasaidia kuwapimia afya ya udongo na kuwapa elimu zadi ya matumizi ya mbegu
mpya, matumizi sahihi ya udongo pamoja na ushauri ili waweze kupata tija zaidi katika kilimo
chao ikiwa ni pamoja na kuwa na uhakika wa uwepo wa mbegu hizo Wilayani Mbarali.
Wakulima hao wameeleza kuwa muda wote walikuwa wakilima kilimo cha mazoea ambacho
hakikuwa na tija kwani walikuwa wakipata gunia 8 -10 kwa ekari moja, lakini sasa wanataka
kubadilika na kutumia mbegu mpya za TARI ambazo humuwezesha mkulima kupata kati ya
gunia 30 - 40 kwa ekari moja.
Wakulima waliohudhuria maonesho hayo ya Mpunga Kilimo Biashara wametoka katika vijiji vya
Ubaruku, Kapunga, Madibila, Uturo na Buyuni Wilayani Mbarali.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...