Na Janeth Raphael- MichuziTv
Bodi ya Filamu Nchini ina lengo la kuratibu uandaaji wa filamu zenye maudhui ya kutangaza utajiri wa nchi katika eneo la utamaduni, historia na jiografia (maeneo mahsusi) ya nchi kwa lengo la kujenga mapenzi hasa kwa vijana wa kitanzania kwa nchi yao na kuwaongezea ufahamu wa rasilimali waliyonayo.
Hayo yamesemwa na Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Filamu Nchini Dkt Kiagho Kilonzo wakati akielezea utekelezaji wa shughuli mbalimbali za bodi hiyo na utekelezaji wa bajeti ya Mwaka wa fedha wa 2022-2023 mbele ya waandishi wa habari leo Oktoba 4,2022 Jijini Dodoma.
Dkt.Kilonzo amesema kuwa Programu hiyo itasaidia kutunza kumbukumbu za kihistoria kwa kuhusisha taarifa za viongozi mbalimbali waliofanya mambo makubwa kama vile Mwl. Julius Kambarage Nyerere ambaye alisaidia ukombozi wa nchi mbalimbali barani Afrika.
"Nchi Ina vivutio vingi sana ambavyo bado havijatangazwa hivyo tunategemea programu mbalimbali tunazotaka kuzianzisha italenga katika kutangaza utajiri mkubwa wa vivutio tulivyo navyo,"Amesema Dkt.Kilonzo
Na kuongeza "Nchi kama Afrika Kusini wao tayari wameshatengeneza filamu inayosimulia kumbukumbu ya Nelson Mandela hivyo na sisi kama Tanzania inabidi tutengeneze ya Mwalimu Nyerere kwani nae alifanya makubwa ikiwemo ukombozi wa Bara la Afrika,"Amesema Dkt.Kilonzo
Aidha Bodi hiyo ina mpango wa Ujenzi wa Eneo changamani la uzalishaji wa Filamu pamoja na Jumba Changamani ikiwa ni Mradi wa kimkakati ambao ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) 2020-2025 unaotarajiwa kuwa na miundombinu ya kisasa itakayowezesha kuwa na uzalishaji wa mazao bora ya filamu kwa kutumia teknolojia za kisasa.
"Ukweli ni kuwa tukisema sisi kama serikali tufanye kila kitu ni ngumu hivyo kwa mpaango huu wa ujenzi wa eneo Changamani la uzalishaji wa filamu na Majumba changamani tunaomba wadau wajitokeze ikiwezekana hata kila mkoa iwe na jumba lake kwa ajili ya kukuza tasnia ya filamu hapa nchini," Amesema Dkt.Kilonzo
Hata hivyo katika kuzitangaza mandhari za nchi yetu mahsusi kwa upigaji picha za filamu, Serikali imeandaa makala (filamu) fupi itakayotangaza maeneo hayo kupitia program yake ijulikanao kama Mapping the Filming Locations huku programu hiyo ikitarajiwa kuzinduliwa hivi karibuni na Waziri Wa Sanaa na Mchezo Mh Mohhamed Mchengerwa kisha kutumwa kwenye majukwaa mabalimbali duniani ili kuvutia waandaaji wengi wa Filamu kuja kuandaa kazi zao hapa Tanzania.
Kwa upande wake Msemaji Mkuu wa Serikali na Mkurugenzi Mkuu wa idara ya Habari Maelezo Gerson Msigwa amesema kuwa Nchi nyingi duniani zimefanikiwa Kupitia Filamu, Filamu zinatumika hata Kwa njia ya ulinzi Kwa hiyo tunatakiwa kuiambia Dunia, Tanzania ni kisiwa Cha Amani ndio maana Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan aliamua kuigiza Filamu ya 'THE ROYAL TOUR FILM' Ili kuongeza kipato Kikubwa kwenye nchi Yetu.
"Naamini hata wengi wenu leo ndio mmejua kuwa Tanzania ni nchi ya pili Afrika kwa utengenezaji wa Filamu ikitanguliwa na Nigeria hivyo hilo ni jambo la kujivumia sana na ndio maana kila mmoja wetu kwa nafasi yake atangaze vivutio vilivyopo hapa nchini Mhe.Rais kashafanya kwa sehemu yake,"Amesema Msigwa.
Bodi ya Filamu Tanzania imehuisha Mpango Mkakati wake kwa miaka mingine mitano Mwaka 2021/22-2025/26, na kuufanya ulenge katika kukuza na kuendeleza Tasnia ya Filamu nchini kwa kuongeza weledi na ubora wa filamu na kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji.
Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Filamu Nchini Dkt Kiagho Kilonzo akielezea utekelezaji wa shughuli mbalimbali za bodi hiyo na utekelezaji wa bajeti ya Mwaka wa fedha wa 2022-2023 mbele ya waandishi wa habari leo Oktoba 4,2022 Jijini Dodoma.Msemaji Mkuu wa Serikali na Mkurugenzi Mkuu wa idara ya Habari Maelezo Gerson Msigwa akizungumza mara baada ya Wasilisho la Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Filamu Nchini Dkt Kiagho Kilonzo akielezea utekelezaji wa shughuli mbalimbali za bodi hiyo na utekelezaji wa bajeti ya Mwaka wa fedha wa 2022-2023 mbele ya waandishi wa habari leo Oktoba 4,2022 Jijini Dodoma.
Sehemu ya Waandishi wa habari wakati wa kikao na Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Filamu Nchini Dkt Kiagho Kilonzo akielezea utekelezaji wa shughuli mbalimbali za bodi hiyo na utekelezaji wa bajeti ya Mwaka wa fedha wa 2022-2023 leo Oktoba 4,2022 Jijini Dodoma.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...