Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama akikabidhi mpira kwa timu za mpira wa miguu kwa wawakilishi wa timu hizo wakati wa Sherehe za ufunguzi wa michezo ya SHIMIWI iliyofanyika jijini Tanga.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na washiriki wa Michezo ya Idara na Wizara za Serikali (SHIMIWI) wakati akifungua rasmi Sherehe za Michezo hiyo kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.
Baadhi ya washiriki wa Michezo ya Idara na Wizara za Serikali (SHIMIWI) wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama (hayupo pichani) wakati akifungua Sherehe za Michezo hiyo katika Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.
Naibu Waziri, Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kufungua Sherehe za Michezo ya Idara na Wizara za Serikali (SHIMIWI) kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.
Sehemu ya watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakipita kutoa salamu mbele ya mgeni rasmi Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama wakati wa Sherehe za ufunguzi wa Michezo ya Idara na Wizara za Serikali (SHIMIWI) zilizofanyika jijini Tanga.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mchezo wa netiboli kabla ya kuanza kwa mchezo huo katika uwanja wa Bandari jijini Tanga wakati wa Sherehe za ufunguzi wa Michezo ya Idara na Wizara za Serikali (SHIMIWI).

Na. Veronica Mwafisi-Tanga

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama amesema Michezo ya Idara na Wizara za Serikali (SHIMIWI) inasaidia kujenga afya za watumishi wa umma ili waweze kutekeleza majukumu yao vema na kutoa mchango katika maendeleo ya taifa.

Mhe. Jenista amesema hayo, wakati akifungua rasmi Michezo ya Idara na Wizara za Serikali (SHIMIWI) kwa mwaka 2022 katika Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, iliyoanza Oktoba 01, 2022 na inatarajiwa kufikia tamati Oktoba 15, 2022.

Mhe. Jenista amesema, Serikali inaendeleza michezo ya SHIMIWI ili kujenga afya za watumishi wa umma nchini na kuhakikisha inakuwa na rasilimaliwatu yenye tija katika kutoa huduma bora kwa wananchi.

Ameongeza kuwa, kutokana na umuhimu wa michezo ya SHIMIWI, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kupitia kwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa, alielekeza kurejeshwa kwa michezo ya SHIMIWI ili itumike kujenga afya ya akili na mwili kwa watumishi wa umma nchini, maelekezo ambayo yalitolewa na Mhe. Waziri Mkuu wakati akimuwakilisha Mhe. Rais Samia kwenye mbio za hisani zilizoandaliwa na benki ya CRDB.

Aidha, Mhe. Jenista awewataka watumishi wote wa umma wanaoshiriki michezo ya SHIMIWI mwaka huu, kuzingatia nidhamu na uadilifu katika kipindi chote watakachokuwa jijini Tanga wakishiriki michezo hiyo ya SHIMIWI.

“Sitegemei kusikia kuna mtumishi yeyote amejihusisha na vitendo vya utovu wa nidhamu kwani michezo ya SHIMIWI ni sehemu ya kazi,” Mhe. Jenista amesisitiza.

Kwa upande wake, Naibu Waziri, Wizara ya utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul amewapongeza watumishi wote waliopo jijini Tanga kuziwakilisha taasisi zao na kuwataka kuzingatia nidhamu katika kipindi chote wanachoshiriki michezo ya SHIMIWI.

“Ni matumaini yangu kuwa, michezo hii itaendeshwa kwa kuzingatia nidhamu, weledi na viwango vya hali ya juu ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na serikali,” Mhe. Gekul amesisitiza.

Mhe. Gekul ameongeza kuwa, licha ya michezo hiyo kujenga afya za watumishi wa umma pia inasaidia kujenga undugu, mshikamano na ushirikiano miongoni mwa watumishi wa umma na hatimaye kuweka mazingira mazuri ya kufikia lengo la Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan la kuujenga utumishi wa umma wenye kuzingatia uadilifu na uwajibikaji.

Naye, Mwenyekiti wa SHIMIWI, Bw. Daniel Mwalusamba ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutambua umuhimu wa michezo kwa watumishi wa umma na kuridhia watumishi wa sekta zote kushiriki michezo ya SHIMIWI kwa ajili ya kujenga afya.

Sanjari na hilo, Bw. Mwalusamba, amemshukuru Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kwa kufungua michezo hiyo muhimu inayowakutanisha watumishi wa umma kutoka katika Wizara, Mikoa, Idara zinazojitegemea, Taasisi na Wakala wa Serikali ambao wananufaika na michezo katika kujenga afya zao.

Zaidi ya watumishi 1000 wanashiriki michezo ya SHIMIWI mwaka huu inayojumuisha soka, netiboli, riadha, kuvuta kamba, bao, kurusha tufe, karata, mbio za baiskeli pamoja na drafti na yenye Kaulimbiu “Michezo hupunguza magonjwa yasiyoambukiza na huongeza tija mahala pa kazi…..Kazi Iendelee”.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...