Na Eleuteri Mangi- MAELEZO
Serikali imesema utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa bomba la kusafirishia gesi asilia kutoka Mtwara hadi Dar es salaam unaenda vizuri kulingana na ratiba yake na utakamilika kwa wakati.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue alipotembelea kituo cha kufua umeme kwa kutumia gesi asilia kinachojengwa Kinyerezi wakati akihitimisha ziara yake ya siku mbili ya kukagua mradi wa ujenzi wa bomba la gesi jijini Dar es salaam.
Balozi Sefue alisema kuwa ni vema kufanyakazi kwa uadilifu na hakuna mchezo, kazi ikitolewa ikamilike kwa wakati.
"Tujenge uchumi wa nchi yetu kwa kutumia umeme wa uhakika, uhakika huo unatokana na gesi asilia tuliyonayo" alisisitiza Balozi Sefue.
Akifafanua zaidi Balozi Sefue alisema kuwa kugunduliwa kwa gesi nchini kumeanza kuleta manufaa mengi ikiwamo wanafunzi kupata udhamini katika masomo yao katika ngazi mbalimbali za elimu, shule zimejengwa, wananchi wa mikoa ya Lindi na Mtwara wanapata maji safi na kupata ajira mbalimbali.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Eliakim Maswi alisema kuwa fedha za ujenzi wa kituo cha kinyerezi I na ujenzi wa vituo vingine vya kinyerezi II, III na IV, zinatolewa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na wahisani.
Fedha za ujenzi wa kituo cha Kinyerezi I zimetolewa na Serikali kupitia TANESCO na ujenzi wa kituo cha kinyerezi II fedha itatokana na ubia kati ya Serikali ya Tanzania na Japani , wakati ujenzi wa kinyerezi III na IV fedha zitatokana na kuingia ubia kati ya Serikali na kampuni ya Kichina.
Alimhakikishia Balozi Sefue kuwa Wizara yake ipo tayari kupokea maelekezo na ushsuri kutoka ngazi za juu za Serikali katika kutekeleza mradi huo wa ujenzi wa bomba la gesi asilia na hatimaye kuongeza uzalishaji wa umeme ili kujenga uchumi wa kipato cha kati ifikapo mwaka 2025.
Mkurugenzi Mkazi wa Mradi huo Bw. Shaun Moore, alimweleza Katibu Mkuu Kiongozi na msafara wake kuwa maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho yanaendelea vizuri kutokana na kampuni hiyo kufanya kazi kwa ushirikiano mzuri na kampuni za kitanzania zilizochukua kandarasi tofauti za ujenzi wa kituo hicho ambapo takribani asilimia 98 ya kandarasi na wafanyakazi ni kutoka kampuni za kitanzania.
Ziara hiyo ilianzia mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani na kuhitimishwa Dar es salaam ambapo Katibu Mkuu Kiongozi aliambatana na Makatibu Wakuu 12 wa Wizara zinzotekeleza Mpango wa Mataokeo Makubwa Sasa (BRN).
Katibu
Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue (katikati) akiwasili kituo cha kufua umeme
kwa kutumia gesi asilia kinachojengwa Kinyerezi wakati akihitimisha ziara yake
ya siku mbili ya kukagua mradi wa ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara hadi
jijini Dar es salaam. Wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi Mkazi wa Mradi huo kutoka
kampuni ya Jacobsen Elektro Shaun Moore na wa kwanza ni Katibu Mkuu wa Wizara
ya Nishati na Madini Eliakim Maswi.
Katibu
Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue akikagua maendeleo ya ujenzi wa mradi huo akiwa na Mkurugenzi Mkazi
wa Mradi kutoka kampuni ya Jacobsen Elektro Shaun Moore (wa kwanza kushoto)
na wa pili kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Eliakim Maswi na kulia ni Mkurugenzi Mkuu TANESCO Felchesmi Mramba
Mkurugenzi
Mkuu TANESCO Felchesmi Mramba akimweleza Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni
Sefue na msafara wake hatua zilizofikiwa kwenye ujenzi wa kituo cha kufua umeme
kwa kutumia gesi asilia kinachojengwa Kinyerezi wakati akihitimisha ziara yake
ya siku mbili ya kukagua mradi wa ujenzi wa bomba la gesi jijini Dar es salaam.
Moja
ya eneo la kituo cha Kenyerezi I ambapo inajengwa mitambo ya kufua umeme kwa
kutumia gesi asilia.
Picha
zote na Eleuteri Mangi- MAELEZO
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...