Kinyanganyiro cha kuwania taji la Miss Manyara 2014, kinatarajia kufanyika Juni 14 mwaka huu katika ukumbi wa CCM Mkoa, mjini Babati, ambapo warembo kumi wanatarajia kuchuana.
Mkurugenzi wa Mirerani Entertainment, Akon Clement ambaye ni Mratibu wa mashindano hayo alisema mgeni rasmi wa mashindano hayo anatarajiwa kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji) Mary Nagu.
Akon alisema msanii maarufu wa kizazi kipya, Bob Junior kutoka jijini Dar es salaam anatarajiwa kutoa burudani kali wakati akisindikiza michuano hiyo ambapo pia wasanii chipukizi kutoka mjini Babati watashiriki kunogesha.
Aliwataja wanyange hao wanaotarajia kushiriki mashindano hayo kuwa ni Miss Mirerani 2014 Amina Omary, Miss Mirerani namba mbili Catherine Emmanuel na Miss Mirerani namba tatu Happy William.
“Wengine ni Fatuma Salim, Betha Fredrick, Rose Evason, Edna Mushi, Hosiana John, Mary Ruta na Flora Godlizen, ambao ni warembo walioshinda kwenye mashindano ya wilaya za Babati, Hanang’ na Mbulu,” alisema Clement.
Aliwataja wadhamini wa mashindano hayo ni kampuni ya Tanzania Breweries (TBL), kupitia kinywaji chake cha Redd’s Original, Open University, Manyara Computer, mireranitanzanite.blogspot.com na Active Classic Fashion.
Mratibu huyo alisema kuwa wadhamini wengine wa shindano hilo ni TanzaniteOne, Assey Printing company, Trimus Saloon, Kifaru Agrovet, Winners Hotel, Sarafina Lodge na Kimweri Sport Wear.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...