Na Mwene Said wa Blogu ya Jamii

Aliyekuwa Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya Bandari (TPA), Ephraim Mgawe  amekiri katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa aliusaini mkataba wa kibiashara kati ya TPA na Kampuni ya China Communications Company Ltd (CCCCL).

Mgawe amekiri kuusaini mkataba huo wa kibiashara leo wakati akisomewa maelezo ya awali (PH)  na Wakili wa Serikali, Pius Hilla mbele ya Hakimu Mfawidhi  wa mahakama hiyo, Isaya Arufani.

Akisomewa maelezo ya awali yanayohusiana na shtaka  la matumizi mabaya  ya madaraka Mgawe alikubali wadhifa wake huo na kwamba aliusaini mkataba huo wa kibiashara siyo  kwa ajili ya  ujenzi wa ghati namba 13 na namba 14 katika Bandari ya Dar es Salaam bali ni kwa minajili ya kuiwezesha kampuni hiyo kupata mkopo nchini mwake China.

Mgawe pia alikubali mahakamani hapo kuwa mwaka 2008 kulikuwepo na mpango wa upanuzi wa bandari wa mwaka 2009-2028 kwa ajili ya upanuzi wa bandari na ujenzi wa ghati na Agosti 9,2009  walikaribisha maoni  ya kupata washauri na wataalam wakufanya upembuzi yakinifu wa mradi huo.

Akiendelea kusomewa maelezo ya awali, Mgawe alikiri kuwa kampuni tano ziliwasilisha mialiko yao ya kutaka tenda hiyo ambazo ni kampuni ya MTBS ya Nethelands,  Scott Wilson ya Uk, Ecorys ya Germany, Mott MacDonald Maritime Consultants ya Uk, HPS  Humburg  ya Ujerumani, SCEC International PTY Limited ya Australia na CPCS Transcom ya Canada.

Mshtakiwa huyo pia alikiri kuwa kampuni ya nchini Canada ya CPCS na kutaja gharama yao kuwa ni dola 323 za kimarekani  ndiyo iliyoshinda zabuni lakini iliyopewa kazi ya upanuzi wa bandari  ni  Kampuni ya China Communications Company Ltd ya China ambayo ilitaja gharama zake kuwa ni dola 523,131,015.97.

Hata hivyo mshtakiwa huyo alikana kuwa baada ya kupewa taarifa hiyo ya gharama za mradi na kampuni ya China ya CCCL alikaa kimya bila ya kutoa  kwenye bodi ya wakurugenzi.

Mgawe na mwenzake Hamad Mussa Koshuma ambaye  alikana kuwa na cheo cha Naibu Mkurugenzi Mkuu mahakamani hapo na kudai kuwa yeye ni Mkurugenzi Mkuu Msaidizi kwa pamoja wanadaiwa kutenda makosa hayo Desemba 5, 2011.

Ilidaiwa kuwa washtakiwa hao  wakati wakiwa kwenye  Mamlaka ya Bandari Tanzania, jijini Dar es Salaam, wakati wakitekeleza majukumu yao ya utumishi wa mamlaka hiyo kwa nafasi ya mkurugenzi mkuu na naibu wake walitumia vibaya madaraka ya kuingia mkataba wa kibiashara kati ya TPA na Kampuni ya China Communications Company Ltd, kwa ajili ya ujenzi wa ghati namba 13 na namba 14 katika Bandari ya Dar es Salaam.

Kwa pamoja washtakiwa hao wanadaiwa kuingia mkataba na kampuni hiyo bila kutangaza zabuni hiyo, kinyume cha masharti ya kifungu cha 31 cha Sheria ya Ununuzi wa Umma, namba 21 ya mwaka 2004, kwa lengo la kuinufaisha kampuni hiyo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...