Na Eleuteri Mangi- Dodoma
28/11/2014.
 
Serikali imesema kuwa VICOBA ni taasisi binafsi inayomilikiwa na wananchi wenyewe vikiwa ni miongoni mwa tasisi ndogo za kifedha ambazo ni za kibinafsi na huanzishwa, kuendeshwa na kusimamiwa ama kijijini, kitongojini na hata kwenye kata.

Hayo yamebainishwa leo Bungeni mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha Mwigulu Nchemba alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Rungwe Magharibi Prof. David Mwakyusa (CCM) ambaye alitaka kujua kama Serikali inatambua VICOBA  kama mkombozi wa wanyonge.

Mwigulu amefafanua kuwa taasisi hizo zimo kwenye sekta ya fedha isiyorasmi na zinatoa huduma za kifedha mijini na vijijini.

 “Uwepo wa taasisi hizi, umewezesha kufikisha huduma za kifedha kwa wananchi waliombali na huduma za sekta rasmi ya fedha na hivyo kuwa mkombozi wa wanyonge” alisema mwigulu.

Aidha, kwa kutambua suala hilo, ili kusaidia na kuimarisha taasisi hizo, Mwigulu amesema kuwa Serikali baada ya kupata ushauri kutoka kwa Mshauri Mwelekezi wa masuala ya uchumi na tafiti za kijamii, inafanya mapitio ya Sera ya Taifa ya Taasisi ndogo za huduma ya fedha ya mwaka 2000 ili kuihuisha iweze kukabili na kuzingatia mabadiliko na maendeleo yanayojitokeza katika sekta hiyo.

Vilevile Mwigulu amesema kuwa Serikali inakamilisha uhuishaji wa sera ya taasisi ndogo ndogo za kifedha ambapo hatua inayofuata ni kuandaa mapendekezo ya muswada ambayo yatapelekwa Baraza la Mawaziri mara baada ya kupata idhini na maelekezo ya Baraza hilo na muswada huo utafikishwa bungeni.


Taasisi ya VICOBA ilianzishwa nchini mwanzoni mwa miaka ya 2000, ambapo imekuwa na manufaa kwa wananchi wengi wenye kipato cha chini hususan wanawake waishio vijijini wamefanikiwa kuboresha kipato chao na maisha yao kwa ujumla kwa kujiunga na taasisi hiyo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...