Na Mwandishi Maalum, New York 
Mkuu wa Majeshi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jenerali Davis Mwamunyange, amelishauri Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa, kuweka bayana na kwa uwazi mamlaka ( mandate) ambayo misheni ya kulinda Amani itapaswa kutelekeza kule inakopangiwa kwenda. 
 Ametoa ushauri huu siku ya Alhamisi wakati alipokuwa akitoa mchango wake kwenye mkutano wa Wakuu wa Majeshi ya Ulinzi ambao nchi zao zinachangia katika operesheni za ulinzi wa Amani za Umoja wa Mataifa. 
Katika mkutano huo uliokuwa wa siku moja, na kuhudhuriwa na Wakuu wa Majeshi na Maafisa wa Ngazi za Juu ,kutoka nchi 108, Jenerali Mwamunyage amesema; “ Wakati wa utoaji wa idhini na mamlaka kwa misheni ya kulinda Amani, Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa, linatakiwa kumwita mbwa kwa jina lake kama lilivyo.Mbwa aitwe kwa jina lake. Elezeni bayana na kwa uwazi mamlaka na idhini za utekelezaji za ya misheni ” 
Na kuongeza, “ iwekwe wazi, kama ni misheni ya kulinda Amani, basi ielezwe ni ya kulinda Amani, na kama ni ya matumizi ya nguvu basi na iwe hivyo”. Amesisitiza Mkuu wa Majeshi 
Amesema kwamba, kwa kutamka jina halisi /mamlaka ya misheni pale inapoundwa, Baraza Kuu la Usalama linakuwa linapeleka ujumbe ulio sahihi kwa pande zote zinazohusika pamoja na nini wakitarajie. 
Jenerali Mwamunyage ameuleza washiriki wa mkutano huo mkutano wa kwanza wa aina yake kuwakutanisha Wakuu wa Majeshi zaidi ya mia moja, wakati mmoja na mahali pamoja. Kwamba, uwazi huo pia utasaidia kuweka bayana hatua za utekelezaji zinazofanywa na walinzi wa amani kwenye eneo la utekelezaji. 
Vile vile Mkuu wa Majeshi ya Tanzania ameshauri pia kuwa misheni ambayo tangu kuundwa kwake zilikuwa na mamlaka ya kutumia nguvu, ni vema zisiendelee kutambuliwa hivyo pale mamlaka ya misheni hiyo yanapobadilika kutoka matumizi ya nguvu na kuwa misheni ya kulinda Amani au jina lolote lile. Tanzania inawanajeshi wake katika Misheni mbalimbali ikiwa ni pamoja na UNAMID ( Darfur) UNFIL, ( Lebanon) MONUSCO ( DRC) na katika maeneo mengine. 
Vile vile Tanzania ina Polisi na Askari Magereza ambao nao wanahudumu katika misheni mbalimbali. 
Akizungumzia kuhusu mkutano huo ambao ulifunguliwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na Ban Ki Moon na kufungwa na Naibu Katibu Mkuu Jan Eliasson. Jenerali Davis Mwamunyange amesema, mkutano kama huo unapashwa kuitishwa mara kwa mara kwa kuwa unawawezesha wakuu wa majeshi kubadilishana uzoefu wao katika utekelezaji wa operesheni za ulinzi wa Amani na hasa kwa kuzingatia kwamba nchi wanachama ndio wanaotoa wanajeshi wao na ndio haswa wanaokumbana na changamoto mbalimbmali za utekelezaji wa dhamana hiyo. 
Awali akifungua mkutano huo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon pamoja na kuwashukuru Wakuu hao wa Majeshi kwa mchango wao katika eneo hilo la ulinzi wa Amani, amesema operesheni ya kulinda Amani chini ya Umoja wa Mataifa, licha kwa kwamba ni dhamana inayohitajika sana lakini pia inakabiliwa na changamoto mbalimbali. 
Akazitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni upugufu wa raslimali fedha, zana, vifaa na teknolojia za kisasa lakini pia ugumu na hatari wanazokumbana nazo walinzi wa Amani, ambapo hivi sasa mbinu za kigaidi na uvamizi kwa walinzi wa Amani ni baadhi ya changamoto na hatari wanazokumbana nazo. 
Katibu Mkuu, amewataka wakuu hao wa majeshi kuongeza ushirikiano wao kwa Umoja wa Mataifa na hasa katika kutafuta mbinu za kukabiliana na changamoto za kiulinzi na kiusalama ambazo duni hivi sasa inakabiliana nao. Akaongeza kuwa kujitokeza kwa idadi kubwa ya wakuu hao wa majeshi ya ulinzi kushiriki mkutano huo, kumeipa faraja kubwa Umoja wa Mataifa. 
Naye Naibu Katibu Mkuu Jan Eliasson, akihitimisha mkutano huo, amewataka wakuu hao wa majeshi na serikali zao kuendelea na majadiliano ya mchakaTo wa kuundwa kwa majeshi ya ulinzi ya kikanda, majadiliano ambayo yanatakiwa kuendelea kuelekea mkutano wa Operesheni ya Ulinzi wa Amani utakaofanyika mwezi Septemba mwaka huu. 
 Wakuu hao wa Majeshi ya Ulinzi pamoja na kutoa mchango wa mawazo yao, pia walipata fursa ya kupata maelezo kutoka kwa Viongozi wakuu waandamizi wanaoongoza Idara zinazozohusu Operesheni ya Ulinzi wa Amani.
 Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Davis Mwamunyange akiwa katika ukumbi  wa Baraza la Uchumi la Umoja wa Mataifa maarufu kama ECOSOC ambapo ndipo ulipofanyika  mkutano wa kihistoria wa Wakuu wa Majeshi ya Ulinzi na Maafisa wa ngazi za juu  kutoka nchi  zinazochangia katika  Operesheni za Ulinzi wa Amani  chini ya Umoja wa Mataifa. Akichangia majadiliano ya mkutano huo. Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi amelishauri  Baraza Kuu la Usalama na  UN kuweka bayana na kwa uwazi  mamlaka ya misheni  inazoziunda. Pamoja naye ni  Brigedia Jenerali MG. Luwogo na Brigedia Jenerali HS Kamunde.
 Mkuu wa Majeshi ya  Ulinzi,  Jenerali Davis Mwamunyage akiwa ndani ya Ukumbi Mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, akibadilishana mawazo na  mmoja wa Maafisa wa ngazi ya juu  kutoka Idara ya Masuala ya Siasa katika UN muda  mfupi  kabla ya  Wakuu wa Majeshi ya Ulinzi hawajapiga picha ya  pamoja na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa. 
 Jenerali Davis Mwamunyange akiwa na ujumbe wake katika picha hii ambayo wapiga mbele ya bendera ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  muda mfupi  baada ya kumalizika kwa mkutano wa siku moja wa wakuu wa majeshi ya  ulinzi kutoka nchi 108 kutoka kushoto ni  Kanal Adolf Mutta, Brigedia Jenerali Luwogo, Mkuu wa  Majeshi  Jenerali  Mwamunyange,  Brigedia Jenerali Kamunde,  Meja Ngh'abi, na  Luten  Kanal Itang'are
 "...Mnatuwakilisha vema?" ndilo swali ambalo   Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi,  Jenerali Mwamunyange alilowauliza watanzania hawa wawili,  Afisa wa Usalama wa UN Bw. Jacob Mwashiozya na  Bw.  Joseph Msami, wa Idhaa ya Kiswahili  ya Umoja wa Mataifa walipokuwa  wakisalimiana naye na ujumbe wake  mara baada ya kumalizika kwa mkutano wa wakuu wa majeshi ya ulinzi
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, akiingia kwa staii ya aina yake wakati alipokwenda kufungua mkutano wa kwanza wa aina yake  kufanyika  katika Umoja wa Mataifa,  ambapo Wakuu wa Majeshi  ya ulinzi kutoka  nchi zaidi ya 100 walikutana kwa wakati mmoja na mahali pamoja kujadiliana na kubadilishana mawazo kuhusu operesheni za ulinzi wa amani za umoja wa mataifa.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...