Wakazi wa Zanzibar wameipongeza kampeni ya”Wait to Send” inayohamasisha usalama barabarani kwa madereva. Kampeni hiyo inayoendeshwa na Baraza la Taifa la Usalama Barabarani kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi la usalama barabarani na Vodacom Tanzania imefanyika Zanzibar mwishoni mwa wiki na kuwavutia wakazi wengi wa kisiwa hicho ambao walisema inaweza kwa kiasi kikubwa kupunguza tatizo la ajali kisiwani humo. 
 Akiongea juu ya kampeni hiyo Kamishna Msaidizi wa Polisi wa Usalama Barabarani wa Zanzibar, ACP Nassor A.Mohamed alisema kuwa ajali za barabarani bado ni tatizo kubwa hapa nchini na ajali nyingi zinasababishwa na uzembe wa madereva hasahasa kutokana na kutozingatia sheria za usalama barabarani. 
 “Unakuta dereva wa gari la abiria anaendesha gari wakati huo huo anatuma ujumbe wa maneno kwenye simu au anaongea na simu wengine pia kuangalia picha kutoka kwenye mitandao ya simu,utakosaje kupata ajali au kuwasababishia ajali watumiaji wengine wa barabara,tena jambo la ajabu hata waendesha pikipiki nao wanatumia simu wakati wanaendesha vyombo hivyo jambo ambalo ni hatari kwa usalama wao”.Alisema. 
 Aliwataka madereva kuzingatia sheria za barabarani na aliishukuru kampuni ya Vodacom na wadau wengine ambao wako mstari wa mbele kuhamasisha uzingatiaji wa sheria za barabarani. 
 Kwa upande wake Meneja Mauzo wa Vodacom Tanzania Kanda ya Zanzibar, Mohamed Mansour alisema kuwa kampeni ya ‘Wait to Send’ inalenga kupunguza ajali za barabarani na inawataka madereva kuacha kutuma meseji au kuongea na simu zao wanapoendesha vyombo vya moto. 
“Katika kufanikisha kampeni hii Vodacom imetoa pete maalum za kuwakumbusha madereva kuacha kutuma meseji wanapoendesha vyombo vya moto na tumezileta kwa ajili ya madereva wa Zanzibar na tutaendelea kuzigawa kama ambavyo tumekuwa tukifanya katika sehemu mbalimbali za nchi ambako kampeni hii imefanyika”Alisema 
 Baadhi ya madereva walieleza kuwa kampeni hii ni muhimu katika kupunguza ajali “Nashauri kampeni hii zifanyike mara kwa mara ili kuwakumbusha madereva kuzingatia sheria za usalama barabarani “.Alisema Abdul Kassim dereva wa basi la abiria Zanzibar. 
 Naye Mansour Juma alisema ajali nyingi zinazotokea zinasababishwa na kukua kwa teknolojia ikiwemo matumizi ya simu,wengine kuangalia televisheni wakati wakiendesha magari na magari yanayoingizwa nchini ni rahisi kwa kila mtu kuyaendesha bila kuhitaji mafunzo ya ziada hivyo alishauri kampeni za aina hii zifanyike mara kwa mara ili kuwakumbusha madereva kuwa makini ili kuepusha ajali zisizo za lazima.
 Kamishna Msaidizi wa Polisi wa Usalama Barabarani wa Zanzibar, ACP Nassor A.Mohamed (kushoto) akikabidhiwa vitendea kazi, fulana, pete na stika ofisini kwake Malindi mjini Zanzibar na Meneja Mauzo wa Vodacom Tanzania Kanda ya Zanzibar, Mohamed Mansour mwishoni mwa wiki kwa ajili ya mwendelezo wa kampeni ya usalama barabarani ya “Wait to Send” inayohamasisha madereva wa vyombo vya moto kutokutumia simu za mkononi wakati wakiwa wanaendesha vyombo hivyo. Wengine katika picha wa pili toka kushoto ni Meneja Uhusiano wa kampuni hiyo Matina Nkurlu na Mwenyekiti wa Kamati ya Mafunzo ya Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, Henry Bantu.
  Mwenyekiti wa Kamati ya Mafunzo ya Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, Henry Bantu (kulia) na ACP Nassor A. Mohamed wakionyesha pete zenye ujumbe maalumu wa Wait to Send baada ya Kamishna Msaidizi wa Polisi wa Usalama Barabarani wa Zanzibar kukabidhiwa vitendea kazi mbalimbali na Meneja Mauzo wa Vodacom Tanzania kanda ya Zanzibar, Mohamed Mansour (kulia) Malindi mjini Zanzibar kwa ajili ya mwendelezo wa kampeni ya usalama barabarani ya “Wait to Send” inayohamasisha madereva wa vyombo vya moto kutokutumia simu za mkononi wakati wakiwa wanaendesha vyombo hivyo. Wengine katika picha wa pili toka kushoto ni Meneja Uhusiano wa kampuni hiyo Matina Nkurlu.
 Mwenyekiti wa Kamati ya Mafunzo ya Baraza la Taifa la  Usalama Barabarani, Henry Bantu na Ofisa wa Jeshi la Polisi kituo cha Malindi mjini Zanzibar, Abdullah Juma kwa pamoja wakimvisha pete maalumu dereva Khamis Sheha Madua anaeendesha daladala iendayo Kizimbani Spice ikiwa na ujumbe wa “Wait to Send” wakati wa zoezi la kutoa elimu kwa madereva mbalimbali lililofanyika mjini Zanzibar mwishoni mwa wiki. Pete hiyo inamkumbusha dereva asitumie simu wakati akiendesha chombo cha moto. Wengine kutoka kushoto ni Meneja wa Mauzo wa Vodacom Tanzania kanda ya Zanzibar,  Mohamed Mansour na Frank Maston.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...