Na  Bashir  Yakub.

Kuna malalamiko  katika  baadhi  ya  maeneo   na  zaidi  malalamiko  haya   yamekuwa  yakielekezwa  kwa   mamlaka  za  serikali  za  mitaa. Nimewahi  kuandika  kuhusu   ukiukaji  wa  taratibu  mbalimbali   ambao  hufanywa   na  serikali  za  mitaa  katika  maeneo  au  ardhi  za  watu.  Pia  niliandika  kuhusu  upotoshi  wa  mamlaka  za  serikali  za  mitaa  katika  kuwaandalia  watu  mikataba  ya  mauzo  ya  ardhi  wakati  wakijua  kuwa  hawaruhusiwi  kufanya  hivyo  jambo  ambalo  huwasababishia  wananchi  usumbufu  mkubwa  wanapoamua  kutafuta  hati  au  kubadili  majina   kwakuwa  mikataba  hiyo  ya  serikali  za  mitaa  huwa  haikubaliki  kisheria na  hivyo  watu  hurudishwa  kuibadili.  

Leo  tena  nazungumzia  ubabe   walionao  serikali  za  mitaa   wa  kutwaa  maeneo  ya  watu  na  kuyapangia  shughuli  mbalimbali  za  mtaa   huku  yakiwa  ni  maeneo   ya  watu  binafsi. Kugeuza  maeneo  ya  watu  njia  bila  fidia  ni  moja   ya  uonevu   mkubwa    ambao  wamekuwa  wakiupata  wananchi  kutoka  serikali  za  mitaa. Kwa  ufupi  tutaangazia  jambo  hilo likoje  kisheria. 

1.SERIKALI  ZA  MITAA  HAWARUHUSIWI  KUTANGAZA  ENEO  FULANI  KUWA  NI  NJIA.

Serikali  za  mitaa  hawana  mamlaka  kisheria   kuchukua  eneo  la  mtu  kulitangaza  kuwa  njia.  Kinyume  na   ilivyozoeleka  ambapo    viongozi  wa  serikali  za mitaa  hutembea  maeneo  mbalimbali  ya  mtaa   na  kuchukua  maeneo  ya  wananchi  kwa  madai  kuwa  yanapaswa  kuwa  njia.  Sheria  ya  ardhi  inasema  kwamba serikali  kuu au  serikali  ya mtaa  au  chombo  chochote  hakiruhusiwi  kutenga  maeneo   kuwa  njia  isipokuwa   lazima  watume  maombi  kwa  kamishna  wa  ardhi  ambaye  ndiye  atakuwa  na  mamlaka  ya  kutangaza  eneo  fulani  kuwa  ni  njia.  

Sheria  inaendelea    kusema  kuwa maombi  hayo  yatakuwa  yamewekwa  katika  fomu  maalum  na  kujazwa  katika  namna  inayokubalika.  Kwa  hiyo  kumbe  hali  haiko  kama  tulivyozoea  ambapo  serikali  za  mitaa  huamua  kuchukua  eneo  la  mtu  na  kulifanya  njia  bila  ruhusa ya  kamishna  wa  ardhi.  Ieleweke  kuwa utaratibu  ndio  huo  wa  kutuma  maombi   kwa  kamishna  wa  ardhi  na  si  kuamka  asubuhi  na  kulifanya  eneo  la  mtu  kuwa  ni  njia.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...