Na Beatrice Lyimo-MAELEZO
Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. Jakaya Kikwete anatarajia kufungua mkutano wa Kanda ya Afrika kuhusu Mpango wa Uendeshaji wa Shughuli za Serikali kwa uwazi (OGP).
Kwa mujibu wa taarifa kutoka Ikulu inaeleza kuwa mkutano huo wenye kauli mbiu isemayo “Kuimarisha Utawala Bora Unaozingatia Uwajibikaji na Uwazi” utafanyika Mei 20 hadi 21, 2015 katika ukumbi wa kimataifa wa Mwalimu Nyerere, jijini Dar es Salaam.
Aidha, imeeleza kuwa dhumuni la mkutano huo ni kuleta ufanisi katika utekelezaji wa masuala mbalimbali ya uwajibikaji na utawala wa Serikali ili kutoa mrejesho kwa wananchi pamoja na uwazi kuhusu masuala ya ardhi.
“Kupata uzoefu wa utekelezaji wa OGP kutoka nchi wanachama katika bara la Afrika nan je ya Afrika kama vile taarifa za uwazi zinazoimarisha uwajibikaji” iliongeza taarifa hiyo.
Taarifa hiyo ilisema kuwa mkutano huo ni wa kwanza kufanyika nchini Tanzania na ni wa pili kwa Kanda ya Afrika ambapo kwa mara ya kwanza ulifanyika nchini Mombasa nchini Kenya mwaka 2013.
Mkutano huo unatarajiwa kuwa na washiriki 200 kutoka Serikalini, Asasi za kirai, Washirika wa Maendeleo wakiwemo Mawaziri kutoka ndani na nje ya nchi, Makatibu Wakuu, Wakuu wa baadhi ya Taasisi za Serikali, wawakilishi kutoka Nchi wanachana wa OGP kutoka bara la Afrika.
Washiriki wengine ni kutoka nchi za Botswana, Zambia, Uganda, Marekani, Zimbabwe pamoja na washirika wa Maendeleo kutoka Benki ya Dunia, UNDP, UNICEF, UNESCO, MCC, USAID, DFID na JICA.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...