Na Teresia Mhagama
Imeelezwa kuwa wilaya za Chato na Biharamulo zitapata umeme wa
uhakika ifikapo mwanzoni mwa mwezi Juni mwaka huu mara baada ya
kukamilika kwa ufungaji wa mtambo wa pili wa umeme wilayani Biharamulo
mkoani Kagera.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage
akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Kagera na kujionea maendeleo ya
ufungaji wa mtambo huo utakozalisha umeme wa kiasi cha kilowati 650.
Mwijage amesema kuwa mtambo huo utakaoanza kazi mwanzoni mwa
mwezi Juni utaongeza kiasi cha umeme unaopatikana katika wilaya hizo
mbili hivyo kuwepo kwa uhakika wa upatikanaji wa umeme wa kutosha
tofauti na ilivyo hivi sasa.
"Tumeamua kuongeza mtambo wa pili kwa kuwa huu uliopo haukidhi
mahitaji ya wakazi wa wilaya hizi mbili na hii ni kwa sababu mtambo uliopo
unazalisha umeme wa kiasi cha kilowati 800 wakati mahitaji ya umeme
katika wilaya hizi ni kilowati 1300," alisema Mwijage.
Alieleza kuwa kukamilika kwa mtambo huo wa kilowati 650 utafanya
wilaya hizo kuwa na umeme wa kiasi cha kilowati 1450 na hivyo kuwa na
ziada ya umeme wa kiasi cha kilowati 150.
Alieleza kuwa awali mtambo huo unaofungwa katika wilaya ya Biharamulo,
ulikuwa ukitumika mkoani Kigoma na uamuzi wa kuupelekea mtambo
husika wilayani Biharamulo ulifanyika baada ya mkoa wa Kigoma kupata
mitambo mipya ya uzalishaji umeme.
“Baada ya kuuleta mtambo huu wilayani Biharamulo, Serikali ilinunua
baadhi ya vipuri vipya kwani vile vya awali vilichakaa na kusababisha
mtambo huu kutokufanya kazi kwa ufanisi. Kazi inayofanyika hivi sasa ni
wataalam wetu wa TANESCO kubadilisha vifaa chakavu na kufunga vifaa
vipya ili mtambo huu uanze kuhudumia wilaya hizi mbili,” alisema Mwijage.
Alisema kuwa wataalam wa TANESCO watafanya majaribio ya mtambo
huo ifikapo Mei 30 mwaka huu na majaribio hayo yatafanyika kwa muda wa
siku tatu mfululizo hadi hapo mtambo utakapozinduliwa rasmi Juni 4,
2015.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage (kushoto) akikagua mtambo wa umeme
utakaozalisha kiasi cha kilowati 650, unaofungwa katika wilaya ya Biharamulo mkoani Kagera.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage (wa pili kulia) akiangalia vipuri vitakavyofungwa
katika mtambo wa umeme utakaozalisha kiasi cha kilowati 650 wilayani Biharamulo. Mtambo huo
uliokuwa ukitumika mkoani Kigoma umehamishiwa wilayani Biharamulo baada ya mkoa wa Kigoma
kupata mitambo mipya.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage (wa kwanza kushoto) akikagua baadhi ya mitambo
ya umeme, katika wilaya ya Biharamulo mkoani Kagera, wakati alipokuwa katika ziara yake ya kikazi
mkoani humo kwa lengo la kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...