Na Daniel
Mbega, Nzega
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi ya Wilaya ya Nzega leo hii
imemhukumu Masanja Mwinamila (44), mkazi wa Kitongoji cha Kona Nne, Kijiji cha
Ugembe II, Kata ya Mwakashanhala, Tarafa ya Puge wilayani Nzega katika Mkoa wa
Tabora kwenda jela miaka 10 kwa kosa la kuteka mtoto mwenye albinism, Margreth
Hamisi (6).
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama hiyo, Saraphine Nsana,
alitoa hukumu hiyo baada ya mshtakiwa kusomewa shtaka na kukiri kutenda kosa
hilo.
Ilielezwa mahakamani hapo kwamba, mnamo Juni 15, 2015
majira ya saa 3:00 usiku katika Kijiji cha Ugembe II, Kata ya Mwakashanhala
wilayani Nzega, mtuhumiwa alimteka binti huyo kwa lengo la kwenda ‘kumuuza’ ili
ajipatie fedha (kiasi kimehifadhiwa).
Hii ni mara ya kwanza kwa kesi inayohusisha utekaji
nyara, kujeruhi na mauaji dhidi ya watu wenye albinism kuchukua muda mfupi
zaidi, kwani ndiyo kwanza kesi hiyo ya Jinai Namba 116/2015 imefikishwa
mahakamani kwa mara ya kwanza na kutolewa hukumu.
Jitihada za
Polisi
Mafanikio ya kukamatwa kwa Masanja Mwinamila akiwa katika
harakati za kutaka kumuuza mtoto Margreth Hamisi, ambaye ni mpwa wake,
yametokana na umakini wa Jeshi la Polisi nchini ambapo maofisa wake wa Kikosi Kazi cha Taifa waliweka
mtego na kufanikiwa kumnasa mtuhumiwa kabla hajamdhuru mateka wake.
Tukio hilo limefanikisha kuubomoa mtandao hatari wa
mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino) kwani ni takriban wiki tatu tu
tangu maofisa usalama walipofanikiwa kuwanasa watu wengine sita wakiwa katika
harakati za kuuza mifupa inayodhaniwa kuwa ya binadamu (albino) mjini Kahama Mei
22, 2015 ambapo tayari wamekwishafikishwa mahakamani pamoja na wengine watatu
waliokamatwa baadaye.
Matukio hayo mawili makubwa yaliyotokea katika kipindi
hicho yamedhihirisha namna serikali kupitia jeshi hilo na vyombo vingine vya
usalama inavyoshughulikia mitandao hiyo hatari usiku na mchana ili kuhakikisha
Watanzania wote wanaishi kwa amani na usalama.
Masanja Mwinamila (44) mara baada ya kufikishwa katika kituo cha Polisi Wilaya ya Nzega Juni 15, 2015.
Mtoto Margreth Hamisi Machiya (6) aliyenusurika kuuzwa akiwa hai na mjomba wake.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, ACP Juma Bwire akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na tukio hilo Juni 16, 2015.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...