
Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Sayansi, Elimu na Utamaduni (UNESCO) nchini Tanzania, Bi. Zulmira Rodrigues (kulia) akimwelezea Katibu Tawala, Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro, Lemuel Kristian Kileo (wa pili kushoto), namna mradi wa ujenzi wa kituo cha sanaa ikiwa ni pamoja na kutoa mafunzo ya ujasiliamali wa bidhaa zinazotokana na mifugo kwa akinamama na wasichana kutoka Kata tano za Wilaya ya Ngorongoro utakavyotekelezwa juzi katika Kijiji cha Ololosokwan. Wengine ni maofisa miradi kutoka UNESCO wakishuhudia.
SHIRIKA la Kimataifa la Sayansi, Elimu na Utamaduni (UNESCO) nchini Tanzania linatarajia kutekeleza mradi wa ujenzi wa kituo cha sanaa ikiwa ni pamoja na kutoa mafunzo ya ujasiliamali wa bidhaa zinazotokana na mifugo kwa akinamama na wasichana kutoka Kata tano za Wilaya ya Ngorongoro kama jitihada za kuongeza kipato kwa familia za jamii ya Wamasai.
Akitoa maelekezo ya mradi huo juzi katika Kijiji cha Ololosokwan mbele ya Katibu Tawala, Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro, Lemuel Kristian Kileo, Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Sayansi, Elimu na Utamaduni (UNESCO) Tanzania, Bi. Zulmira Rodrigues alisema mradi huo unatarajia kutekelezwa kuanzia Mwezi Agosti, 2015.
Bi. Rodrigues alimueleza Kileo kuwa mradi huo unajumuisha ujenzi wa kituo cha kisasa cha sanaa ambacho kitatumiwa na wajasiliamali wa jamii ya Kimasai kwa ajili ya kuuza bidha zao za asili mbalimbali kwa watalii wanaofika kutembelea vivutio anuai vya utalii ikiwemo Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro inayozunguka vijiji hivyo.
Akifafanua zaidi juu ya mradi huo, Ofisa Mradi Utamaduni wa Shirika la Kimataifa la Sayansi, Elimu na Utamaduni (UNESCO) nchini Tanzania, Rehema Sudi alisema mradi huo utajumuisha mafunzo ya ujasiliamali juu ya utengenezaji wa bidhaa za ngozi, pembe za ng'ombe pamoja na shanga ili kuziongezea thamani na kuuzwa kwa watalii anuai wanaotembelea vivutio na kukuza vipato vya familia hasa akinamama.
Bi. Sudi aliongeza kuwa kata zinazotarajia kunufaika na mafunzo na ujenzi wa kituo hicho cha kisasa kwa ajili ya mauzo ya bidhaa hizo za asili za Wamasai ni pamoja na Kata za Ololosokwani, Arash, Soit Sambu, Oloipili na Kata ya Aoliani Magaidulu zote za Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro.
"Mradi huu utajumuisha akinamama na wasichana kutoka kata tano ambazo ni Ololosokwani, Arash, Soit Sambu, Oloipili na Kata ya Aoliani Magaidulu, tutawapatia mafunzo juu ya utengenezaji wa bidhaa mbalimbali zinazotokana na ngozi na pembe za ng'ombe pamoja na shanga ikiwa ni hatua ya kuziongezea thamani kisha kuziuza kwa watalii ambao wanatembelea vivutio vya utalii eneo hili hasa Kijiji cha Ololosokwan," alisema Ofisa Mradi Utamaduni Unesco, Bi. Sudi.


Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...