A; KIKAO KAMATI YA UTENDAJI

KAMATI ya Utendaji ya Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), inatarajiwa kukutana Ijumaa Agosti 7, 2015, Dar es Salaam kujadili masuala mbalimbali yahusiyo michezo na waandishi wa habari za michezo hapa nchini.


Pamoja na mambo mengine, kikao hicho kitajadili namna bora ambayo chama kinaweza kushiriki kwa kuangalia jinsi ya kuwaunganisha wanamichezo kwa namna mbalimbali katika Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani utakaofanyika Oktoba 25 mwaka huu kwa maslahi ya michezo nchini.


Moja ya madhumuni ya TASWA wakati inaanzishwa ni kuwaunganisha waandishi wa habari za michezo nchini, kushirikiana katika kukuza na kupromoti michezo na wanamichezo kwa njia ya kalamu na njia nyingine za kupashana habari.

Kwa msingi huo tunaamini kikao kitatoa muongozo mzuri, ambao unaweza ukasaidia wanamichezo hapa nchini kufahamu sera za michezo kwa wagombea mbalimbali na hivyo kufanya uamuzi sahihi wakati ukifika.


Pia kikao kinatarajiwa kufanya uteuzi wa washiriki wa semina mbili zinazotarajiwa  kufanyika hivi karibuni, zikihusisha waandishi wa habari za michezo wa kada ya kati na wale wazoefu.


Tunaamini tumetoka mbali na tunajua safari yetu ya kuchangia kukuza michezo nchini bado ni ndefu na ina mabonde, mabwawa na utelezi. Sisi hatujiulizi ,  Jee tutafika? Bali hujiambia juhudi zetu zitatufikisha tunapotaka kufika.


B; PONGEZI AZAM

Tunatoa pongezi kwa timu ya soka ya Azam FC kwa kuibuka bingwa wa michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati ‘Kombe la Kagame’ mwaka 2015.


Tunaungana na Watanzania wengine katika kufurahia ubingwa huu, baada ya Jumapili Azam kuifunga Gor Mahia ya Kenya mabao 2-0 katika mchezo wa fainali Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, hivyo tunawaomba wachezaji watumie ubingwa wa Kagame kama changamoto ya kufanya vizuri katika michuano ya Kombe la Shirikisho la Soka Afrika (CAF) mwakani.


Azam wasibweteke na kuona tayari wamemaliza kazi, bali waendelee na jitihada za kutafuta mafanikio makubwa zaidi.


C: UTOAJI WA VITAMBULISHO

TASWA ilisitisha kutoa vitambulisho vipya kwa wanachama wake kwa muda kwa sababu ilikuwa ikifanya utaratibu wa kubadili vile vya awali na kuwa na vitambulisho vya kisasa zaidi, ambapo suala hilo lipo hatua za mwisho kukamilika na hivi karibuni wanachama wote wapya watapatiwa vitambulisho vyao.


Nawasilisha,

Amir Mhando,

Katibu Mkuu TASWA

05/08/2015

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...