TAKWIMU zinaonyesha kwamba wananchi hawaelewi nafasi rasmi ya Ukawa
22 Septemba, Dar es Salaam: Asilimia 62 ya wananchi wanasema kwamba wanajisikia wapo karibu zaidi na chama cha CCM kuliko vyama vingine. 
 
Aidha, walipoulizwa watawachagua wagombea wa chama gani – bila kutajiwa majina ya wagombea – wananchi 6 kati ya 10 walisema kwamba watawachagua wagombea wa CCM kwa Urais (66%), Ubunge (60%) na Udiwani (60%). Takwimu hizi zinatoa picha kwamba CCM inaungwa mkono, kama ilivyokuwa mwaka 2012.

Chadema ni chama cha pili kinachopendwa kushinda vyama vingine vya upinzani. Lakini wananchi wanaosema kwamba watawachagua wagombea wa Chadema kwa Urais, Ubunge na Udiwani wamepungua kidogo. Ikumbukwe kuwa, inawezekana wananchi wanaopenda zaidi mseto wa Ukawa waliunga mkono vyama vya CUF, NCCR-Mageuzi au NLD.

Mbali ya CCM na vyama vinavyounda Ukawa, chama cha ACT-Wazalendo kilitajwa na zaidi ya asilimia moja ya wananchi.

Walipoombwa kutaja moja kwa moja jina la mgombea Urais ambaye wangemchagua, asilimia 65 ya wananchi walimtaja mgombea wa CCM, John Magufuli. Asilimia 25 walimtaja mgombea wa Chadema (na Ukawa), Edward Lowassa. Asilimia 10 iliyosalia iligawanyika kati ya wale waliomtaja mmoja miongoni mwa wagombea urais wengine, waliokataa kujibu na waliokuwa bado hawana mgombea waliyempendelea. Hata hivyo, takwimu zilikusanywa kabla vyama vingine, kikiwemo ACT-Wazalendo, kuteua wagombea wao wa Urais. Takwimu hizi (zilizokusanywa kati ya Agosti na Septemba) sio utabiri wa matokeo ya uchaguzi. Zinaonyesha tu kwamba mwanzoni mwa kipindi cha kampeni, mgombea Urais wa CCM, John Magufuli, alikuwa anaongoza katika kura za maoni.


Aidha, vigezo muhimu vinavyohusu makundi mbalimbali ya watu (demografia) vilitumika kuchambua ni nani au makundi gani yanayowaunga mkono John Magufuli na Edward Lowassa. Wahojiwa ambao walikuwa vijana zaidi, wasomi zaidi, wanaume na wakazi wa mijini, walimuunga mkono Edward Lowassa. Makundi ya wahojiwa wazee zaidi, waliokuwa na elimu ya msingi tu, wanawake na wakazi wa vijijini walielekea kumuunga mkono zaidi John Magufuli kuliko vijana zaidi, wasomi zaidi, wanaume au wanaoishi mijini.

Hata hivyo, katika makundi yote haya, John Magufuli wa CCM anaonekana kuongoza. Kwa mfano, asilimia 33 ya wananchi wenye umri wa 18 – 29 na asilimia 30 ya wenye umri wa 30 – 39 wanamuunga mkono Lowassa, tofauti na asilimia 15 ya watu wenye umri zaidi ya miaka 50. Pamoja na hayo, asilimia 57 ya watu wenye umri wa 18 – 29 na asilimia 76 ya watu wenye umri wa 30 – 39 wanamuunga mkono Magufuli. Upande wa makazi, asilimia 28 ya wakazi wa mijini walimuunga mkono Edward Lowassa tofauti na asilimia 24 ya wakazi wa vijijini. Asilimia 66 ya wakazi wa vijijini na asilimia 61 ya wakazi wa mijini wanamuunga mkono John Magufuli.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...