JAMHURI
YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA
MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA
Simu: 255-22-2114615, 211906-12
Barua pepe: nje@nje.go.tz
Barua pepe: gcu@nje.go.tz
Tovuti : www.foreign.go.tz
Nukushi: 255-22-2116600
|
|
20 KIVUKONI FRONT,
P.O. BOX 9000,
11466 DAR ES SALAAM,
Tanzania.
|
TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
Wizara
ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa imepokea kwa mshtuko na masikitiko
makubwa taarifa za kufariki kwa Mahujaji zaidi ya 700 na wengine zaidi ya 800
kujeruhiwa wakati wakishiriki ibada ya Hijja iliyofanyika Makkah, Saudi Arabia
tarehe 24 Septemba, 2015.
Kwa
mujibu wa taarifa kutoka Ubalozi wa Tanzania, Saudi Arabia
Mahujaji
hao walifariki na kujeruhiwa kutokana na msongamano mkubwa wa watu uliotokea
kwenye eneo la Mina.
Aidha,
taarifa hizo zinaeleza kuwa hadi sasa Mahujaji wapatao watano (5) kutoka
Tanzania wamefariki dunia na wengine kujeruhiwa. Majina ya Watanzania
waliofariki na kutambuliwa ni Bi.
Mwanaisha Hassan Juma, Mkungwe
Suleiman Hemedi na Sefu Saidi
Kitimla. Mtu mwingine aliyefariki ni Raia wa Kenya anayeishi nchini ambaye
ametambulika kwa jina la Bi. Fatuma
Mohammed Jama.
Ubalozi
unaendelea na jitihada za kupata jina la Mtanzania mwingine aliyefariki kwenye
tukio hilo. Aidha, Serikali ya Saudia imetangaza kuwa itatoa taarifa kamili
ikiwemo idadi ya watu waliofariki na majeruhi na nchi wanazotoka mara
itakapokamilika.
Pia
Ubalozi wetu kwa kushirikiana na Taasisi zinazoshughulikia masuala ya Hijja za
Tanzania ikiwemo BAKWATA pamoja na Mamlaka za Serikali ya Saudi Arabia
unaendelea kufuatilia kwa karibu ili kujua endapo kuna vifo na majeruhi wengine
kutoka Tanzania.
Hivyo
basi, Wananchi wanaombwa kuwa watulivu katika kipindi hiki kigumu wakati
Serikali ikiendelea kufuatilia.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya
Serikali kwa Umma,
Wizara ya Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa,
Dar es Salaam
25 Septemba, 2015
Ankal
ReplyDeleteKwetu wanadamu, huu ni msiba mkubwa sana. Lakini Mungu ndiye anafahamu njia zake. Tumtegemee wakati huu wa majonzi.
Nilifundishwa katika dini yangu ya Katoliki kwamba tukifa katika mazingira kama haya, ambapo tunakuwa tumejitakasa kiroho, ni kifo chema. Kwa msingi wa imani hii, na kwa kuzingatia kuwa hao mahujaji walikuwa katika hali safi kiroho, wameenda kwenye mapumziko ya milele mbinguni. Hii ni faraja. Iwe faraja kwa wafiwa na wengine.
Papo hapo, wakati huu wa majonzi, zimejitokeza taarifa kuwa kiongozi mmoja huko Saudia amewalaumu wa-Afrika kwa tukio hili la kusikitisha. Kama taarifa hizo ni kweli, sioni busara yake, hasa kwa kipindi hiki kigumu:
http://howafrica.com/saudi-prince-blames-black-africans-for-hajj-stampede-717-dead-so-far/