Na. Tamimu Adam – Jeshi la Polisi.

Jeshi la polisi nchini, limeanzisha mpango wa   kuboresha usalama wa jamii  nchi nzima ambao unalenga  kuboresha  utoaji wa huduma bora kwa wananchi, kuboresha mawasiliano  ya ndani na nje ya Jeshi la polisi kwa kuwashirikisha wadau  mbalimbali wa usalama ambapo mpango huo utaanza kutekelezwa katika mkoa wa kipolisi kinondoni  ambapo lengo lake ni  kupunguza uhalifu kwa asilimia kumi ifikapo mwaka 2019.

Akihitimisha  maabara ya mpango huo iliyofanya kazi kwa wiki sita, Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi  Abdulrahmani  Kaniki  aliwahakikishia  washiriki wa maabara ya kuboresha usalama wa jamii, kuwa Jeshi la polisi litatekeleza  kwa vitendo mapendekezo yote yaliyotokana na maabara hiyo, kwani baadhi ya mapendekezo   hayahitaji bajeti  hivyo utekelezaji wake utaanza mara moja.

 “Kazi iliyofanywa  na maabara hiyo ni kubwa  na umuhimu katika kuboresha usalama wa jamii katika nchi yetu hivyo mapendekezo yote ni lazima yafanyiwe kazi ili kuleta mafanikio chanya”. Alisema Kaniki.

Aliongeza  kuwa mpango huo umeanzia  katika mkoa wa kipolisi kinondoni na baadaye utaenea nchi nzima, ambapo alizitaja sababu zilizopelekea kuanza na kinondoni kuwa ni pamoja na  kuongezeka kwa makosa,  kupanuka mji, idadi kubwa ya watu na uwepo na shughuli nyingi za kiuchumi ukilinganisha na maeneo mengine.

Naye, Mtendaji mkuu wa  ofisi ya Rais ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi (PDB), Omari Issa alisema mpango huo wa uboreshaji wa usalama wa jamii ambao unaanza na mkoa wa Kinondoni uliandaliwa kwa kuwashirikisha wadau kutoka taasisi mbalimbali za serikali na kijamii ambao kwa pamoja walishirikiana kwa pamoja katika kuangalia namna ya kuboresha usalama wa jamii  ili kuwezesha jamii  kuwa salama.

Aliongeza kuwa mpango wa matokeo makubwa sasa unahitaji kuzingatia vitu vikuu vitatu katika utekelezaji wake ambavyo ni kujiwekea vipaumbele, nidhamu ya utekelezaji na uwajibikaji hivyo alisema hana wasiwasi na Jeshi la Polisi katika utekelezaji wa mpango huo hapa nchini.

Mpango wa uboreshaji wa usalama  wa jamii unalenga  kuboresha  na kurahisisha huduma mbalimbali zinazotolewa na Jeshi la polisi ikiwemo kuboresha mazingira ya kufanyia kazi kwa askari, usimamizi wa rasirimali watu na vifaa na kuweka mikakati ya kuwashirikisha wadau wa kada mbalimbali ndani  ya jamii katika kuboresha usalama wa jamii.
 Maabara hiyo ya  kuboresha usalama wa jamii ripoti yake inatarajiwa kukabidhiwa kwa Inspekta Jenerali wa Polisi hivi karibuni ili kuanza utekelezaji wake kwa kuanza na mkoa wa kipolisi wa Kinondoni.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...