Na Shamimu Nyaki, WHUSM.
Serikali imesema kuwa Muswada wa
Sheria ya Huduma ya Habari unatoa fursa kwa wanahabari mbalimbali kuwa
na Haki ya kupata Bima ya Afya kwa ajili ya kupata matibabu.
Hayo
yamesemwa na Mkurugenzi wa Idara ya Habari MAELEZO na Msemaji wa
Serikali Bw. Hassan Abbas alipokuwa akizungumza katika kituo cha
Redio E Fm kilichopo Jijini Dar es Salaam, ambapo ameeleza kuwa Muswada
huu utatoa fursa kwa wanahabari kupata Bima ya Afya na kuondokana na
changamoto ya ukosefu wa fedha ya matibabu.
“Muswada huu
utasaidia wanahabari kuwa na Bima ya Afya itakayosaidia kupata huduma
ya kiafya na kuacha utaratibu ulipo sasa wa kutoa michango wakati
mwanahabari anapokuwa mgonjwa au anapofariki.” Alisema Bw. Abbas.
Aidha
Mkurugenzi huyo ameongeza kuwa Sehemu ya tatu ya Muswada huu unaeleza
kuwa kutakuwa na Mfuko kwa ajili ya Habari ambao lengo lake kuu ni
kuwezesha mafunzo kwa wanataaluma ya habari pamoja na kukuza na
kuendeleza utafiti na maendeleo katika nyanja ya Habari na Mawasiliano
ya Umma.
Katika hatua nyingine Mkurugenzi huyo ametoa rai kwa
wadau na wanatasnia kwa ujumla kuusoma Muswada huu na kutoa maoni yao
ambayo yatasaidia kuuboresha ili uweze kutumika kwa ajili ya maendeleo
ya Tasnia ya Habari.
“Naomba wadau muusome Muswada huu muuelewe
na muweze kutoa maoni yenu kabla haujapelekwa Bungeni kwa mara ya pili
ili tasnia hii iwe na hadhi kama inavyostahili.” Aliongeza Bw Abbas.
Muswada
wa Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016 upo katika hatua ya
kujadiliwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii
na wadau kutoa maoni kwa ajili ya kuuboresha Muswada huo kabla ya
kuwasilishwa Bungeni kujadiliwa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...