Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imependa kuwatakia kheri na mafanikio watoto wote wa kidato cha nne walioanza kufanya mtihani wa Taifa wa kuhitimu elimu ya Sekondari kuanzia tarehe 01 Novemba, 2016. Wizara yenye dhamana ya maendeleo ya watoto inawaomba watoto wanaotahiniwa kutambua kuwa, muda wa kufanya mtihani ni fursa adhimu kwao, hivyo ni lazima kuutumia kwa umakini mkubwa kwa ajili ya mustakabali wa maisha yao binafsi, familia na taifa kwa ujumla.

Wizara inawaasa kuwa waangalifu muda wote wa kutahiniwa, wazingatie kanuni na taratibu stahiki, na pia kuepuka kuandika mambo ambayo yasiyotakiwa katika karatasi za mtihani. Kipindi cha kufanya mtihani ni kifupi ukilinganisha na muda wa miaka minne ambayo watoto hawa wamekaa madarasani wakiwa katika masomo; hivyo watoto wanahimizwa kujiepusha na vishawishi vyovyote ikiwemo vitendo vya udanganyifu katika chumba cha mtihani ambavyo vinaweza kusababisha kubatilishwa kwa matokeo yenu na hivyo kukatisha ndoto zenu. Ni matarajio ya Wizara kuwa wote mtamaliza mitihani yenu vizuri na kwa amani na utulivu.



Wakati watoto wetu wakiendelea kufanya mitihani yao, Wizara inawakumbusha wazazi na walezi kutambua kuwa mnaowajibu wa kuweka mazingira ya kuwasaidia kukumbuka yote waliyojifunza kipindi chote cha masomo yao na kuwa tayari kujibu mitihani yao wakiwa wameandaliwa kisaikolojia ili kuhitimu vizuri. Aidha Serikali haitarajii kusikia au kuona mzazi au mlezi yeyote akijaribu kutengeneza mazingira ya kuharibu ndoto ya mtoto yeyote hasa watoto wa kike kwa kupanga kuwaozesha mara tu wanapomaliza mitihani ya Taifa ya kidato cha Nne.



Wizara inaamini kuwa wazazi na walezi watakuwa makini kuandaa mazingira ya watoto kufikia ndoto zao kielimu, na kuwaepusha watoto wa kike na janga la ndoa za utotoni, hadi watakapofikia umri stahiki. Wizara inasisitiza kwamba atakayethubutu kukatisha ndoto ya mtoto wa kike kwa kumwozesha chini ya umri wa miaka 18, Serikali haitasita kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya mzazi na mlezi huyo ili kulinda haki na masilahi ya mtoto kulingana na sheria, taratibu na kanuni zinazomlinda mtoto.



Wizara inatoa rai kwa wazazi, walezi, makondakta na jamii kwa ujumla, kuwapa ushirikiano madhubuti watoto wetu katika kipindi hiki cha mitihani yao ili waweze kuhitimu vizuri mitihani yao. Watahiniwa ni hawa ni vijana wetu wanaotarajiwa kuendeleza taifa letu, hivyo tuwajengee mazingira murua ya kupata haki ya elimu ili kuwa na vijana mahiri na wenye weledi wakiwa na stadi na maarifa ya kubeba majukumu ya Taifa katika harakati za kuelekea uchumi wa kati,
MARGARET S. MUSSAI 

KAIMU MKURUGENZI WA MAENDELEO YA WATOTO 
WIZARA YA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...