Na Mwandishi Wetu,Same

MKUU wa Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro Kasilda Mgeni amewahimiza  wananchi kuhakikisha wanatunza vyanzo vya maji kwa kutunza mazingira na kupanda miti pembezoni mwa vyanzo vya maji 

Mgeni ametoa ushauri huo wakati wa  kilele  cha Wiki ya Maji kitaifa yaliyofanyika katika Kata ya Hedaru mbapo pia amepanda mti huku akihimiza kila kaya  kupanda mti kwenye maeneo ya nyumba zao,

Pia  amesisitiza wananchi kuepuka kulima ndani ya mita 60 kutoka kwenye chanzo cha maji. Aidha amewaelekeza wataalamu wa maji kuhakikisha wanatoa elimu kwa wananchi kuhusiana na suala zima la mita 60.

Aidha amewaomba wananchi wote kumuunga mkono Rais Dk.Samiha Suluhu Hassani kwa kazi kubwa anayoifanya kuleta maendeleo katika jamii.



MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana amesema ni jukumu la viongozi wa dini kuwaunganisha Watanzania,
kudumisha amani, umoja na mshikamano.


Pia, ametaka kuendeleza utamaduni kuheshimu imani ya kila mmoja kwa kutazama mambo mazuri na sio changamoto chache zinazojitokeza.

Kinana aliyasema hayo leo Machi 26, 2023 wakati akizungumza katika hafla ya mashindano ya kuhifadhi na kusoma Kuraani tukufu yaliyoandaliwa na Taasisi ya Aswhabu al-Kahfi Islamic Centre, yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.

“Hivi sasa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, ameweka mkazo kwenye maridhiano na tuna taasisi ya maridhiano na amani mbayo imeunganisha dini na madhehebu mbalimbali nchini, lengo ni kudumisha umoja, mshikamano na amani katika taifa letu.

“Mimi ningependa kuwasihi viongozi wa dini, kila madhehebu, kila dini ni muhimu tushikamane…msitafute mapungufu ya kila mmoja, mtafute mema ya kila mmoja ili tuweze kushikamana,” alisema.

Kinana aliwasihi Watanzania kuzingatia na kutanguliza mambo mazuri ya kila mmoja kuondoa uwezekano wa kuibua migogoro isiyo na tija kwa ustawi wa taifa.

Awali akimkaribisha Kinana, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Selemani Jafo, alisema amani na maadili yanasisitizwa mahali popote kwani hata Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2020-2025 imetaja ajenda ya amani na maadili.

“Leo tupo hapa tunafanya mashindano ya Kuraani tukufu bila ya changamoto yoyote, hii ni kutokana na maadili, amani na utulivu uliopo nchini,” alisema.


Katika mashindano hayo Jafo aliwataka viongozi wa dini na jamii kwa ujumla kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Rais Dk. Samia kuleta maendeleo nchini.

“Rais Samia anafanya mambo mengi mazuri kazi yetu sisi tumuunge mkono kwa kutunza amani iliyopo ili yeye aendelee kuleta yale mazuri anayoyahitaji kuyafanya ndani ya Tanzania,” alisema.

Akitolea mfano wa faida ya amani na utulivu Jafo alisema tayari Rais Dk. Samia ameshatoa mabilioni ya fedha kutekeleza mradi wa reli ya kisasa (SGR) ambayo ujenzi wake unakwenda kasi.
“Mradi huu unaenda vizuri kwa sababu kila njia ina mkandarasi anafanya kazi,” alisema.

Aidha, alisema kuanzia mwaka jana wanafunzi wote wa kidato cha kwanza walianza shule kwa pamoja na kulikuwa hakuna chaguo la pili kama ilivyozoeleka huko nyuma.

“Mambo hayo yote yanafanyika kwa sababu ya kuwepo kwa amani inayosababaisha miradi ya maendeleo,” alisema

Kaimu Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam, Walid Omar aliwasisitiza wazazi na walezi kuitekeleza kaulimbiu ya mashindano hayo inayosema ‘Jambo limekuwa jambo, Qur’an ni mkombozi wa malezi’.

Alisema kaulimbiu hiyo inatakiwa itekelezwe kwa vitendo hususan kwa wazazi na walezi wa Kiislamu.
“Kila mzazi ashike nafasi yake ya kumlea mtoto wake katika maadili ya dini, akiifuata Qur’an Tukufu kwa kuwa ndio mwongozo bora wa malezi ya watoto na kuifanya jamii iwe na vijana hodari, wenye kumtii Mwenyezi Mungu,” alisema.

Katika mashindano hayo Bakari Hamadi (19) mwanafunzi wa madrasa ya Mjamma Rahmaan ya Mkuranga mkoani Pwani aliibuka mshindi katika kipengele cha kuhifadhi juzuu 30 na kuzawadiwa sh. milioni 2.5.


Pia, Hujaima Othman (8) mwanafunzi wa Madrasat Ibnu Makhtuum iliyopo Chamazi, alishika nafasi ya kwanza kwa upande wa juzuu tatu ambapo alizawadiwa sh. 300,000.
Ndg. Abdulrahman Kinana, Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara Akihutubia  viongozi wa Dini ya Kiislam,Waumini,Washiriki  katika Mashindano ya Nane ya Kuhifadhi Quran Tukufu Mkoa wa Dar es Salaam yaliyoandaliwa na Taasisi ya Asw- haabul Kahfi Islamic Centre, ukumbi wa kimataifa wa Mwl Julius Nyerere,Machi 26,2023.(Picha zote na Fahadi Siraji )

Ndg. Abdulrahman Kinana, Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara Akikabidhi zawadi kwa  Hujaima Othman (8) mwanafunzi wa Madrasat Ibnu Makhtuum iliyopo Chamazi, aliyeshinda nafasi ya kwanza kwa upande wa juzuu tatu ambapo alizawadiwa sh. 300,000.(Picha zote na Fahadi Siraji )

Na Khadija Kalili
MKE wa wa aliyekuwa Rais wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Julius Kambarage Nyerere Mama Maria Nyerere jana usiku Machi 25, 2023 ametunukiwa zawadi ya Malkia wa Nguvu ya mwaka 2023 kwenye kilele kilichofanyika kwenye ukumbiwa Mlimani City Jijini Dar Es Salaam.

Tuzo hiyo ya heshima imetolewa na Spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Tulia Ackson na kumkabidhi Mkuu wa Mkoa wa Manyara Makongoro Nyerere ambaye pia ni mtoto wa mama Maria Nyerere.

Tuzo hizo za Malkia wa Nguvu zimefanyika kwa mara ya saba sasa zimeandaliwa na Clouds Media Group na kudhaminiwa na CRDB Benki, Kilombero Sugar, Bwana Sukari, Kampuni ya Bia Serengeti (SBL), DSTV na Classic Finnishers.

Wanawake wengine walio pata tuzo kwenye vipengele mbalimbali.

Tuzo ya Uongozi imekwenda kwa Kamishna Generali wa Jeshi la Uhamiaji Anna Makakala.

"Namshkuru mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzani Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuniamini pamoja na viongozi wote wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi kwa kumpa ushirikiano katika kazi zangu za kila siku za kukitumikia taifa" amesema Kamishna Makakala mara baada ya kupokea tuzo hiyo ya Uhamiaji, Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Umeme Tanesco Somoe Ismail aliyepata Tuzo ya Funguo ya maisha kusababisha kwa kuwashika mkono Malkia wengine katika eneo lake la kazi.

Tuzo ya Ubunifu na uvumbuzi ilikwenda kwa Tasila Melita ambaye amebuni mashine ya kuteketeza taulo za kike wanazotunia wanapokuwa kwenye hedhi, Tuzo ya Ustawi wa Jamii imenyakuliwa na Dkt.Stella Rwezahura ambaye ni Daktari bingwa wa damu ambaye ndiye alisimamia upandikizwaji wa uloto kwa wagonjwa 11 wenye saratani ya damu nchini huku Tanzania ikiwa nchi ya kwanza katika ukanda wa Afrika Mashariki kutoa matibabu haya.

Akizungumza mara baada ya kupokea tuzo yake Dkt.Rwezahura amesema kuwa jamii inapaswa kuondokana na imani potofu kuwa ugonjwa huu ni wa kurogwa hivyo mara wanapogundulika wanatakiwa kwenda hospitalini mara moja kwa sababu unatibika ni wa kurithi kama ilivyo selimundu na upo duniani kote.

"Naishukuru serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kunipa nafasi ya kusoma na kuwa Daktari bingwa wa damu kwani wakati naanza kusoma kulikua na madaktari bingwa wa damu wawili tu na walikua wakikaribia kustaafu japo awali nilipenda kuwa daktari wa wanawake hivyo nilikubali ushauri niliopewa na kwa sasa nawajibika kwa ajili ya taifa langu najivunia hili na nawashukuru wote pamoja na familia yangu." Amesema Dkt. Rwezahura.

Wengine waliopata tuzo ni Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Foundatin Tuli Ester Mwambapa aliyepata tuzo ya mhamasishaji bora wa mwaka .

Tuzo ya Malkia anayesabababisha ajira ilikwenda kwa mmiliki wa Kampuni ya Zara Tours ambaye ametoa ajira kati ya 300 hadi 600 katika ya utalii nchini washindi wote wamepewa tuzo pamoja na hundi ya Mil.3 kila mmoja zilizotolewa na Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL).

Usiku huo wa Malkia wa Nguvu 2023 umehudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Mke wa Rais wa awamu ya nne Mama Salma Kikwete, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi CCM Sophia Mjema na wawakilishi kutoka vyama mbalimbali vya siasa nchini.
Spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Tulia  Ackson akikamkabidhi tuzo Mkuu wa mkoa wa Manyara Makongoro Nyerere ambaye ni mtoto wa Rais wa Kwanza wa Tanzania Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

TAASISI ya kusaidia sekta binafsi ya kilimo ( PASS) imeanzisha kampeni tanzu iitwayo Pass leasing ili kupanua wigo wa huduma zake ikiwa ni pamoja na kutoa mikopo kwa asilimia 80 ya zana za kilimo na viwanda bila dhamana kwa kushirikiana na wasambazaji wa zana hizo.

Mkurugenzi wa Masoko wa PASS, Adam Kamanda ametoa taarifa hiyo kwenye mkutano wa mashauriano na wadau wa sekta ya kilimo wa kuhamasisha uzalishaji unaozingatia ukuaji wa kijani shirikishi uliofanyika pia mkoani tabora.

Kamanda ambaye alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa PASS, Yohana Kaduma amesema, kwa miaka 23 iliyopita PASS imewanufaisha wajasiliamali milioni 3.4 ambao wametoa ajira milioni 2.7 kati yao asilimia 51 ni Wanawake nchini.

Amesema kwa kipindi hicho benki 14 zilishirikiana na taasisi hiyo na kutoa mikopo yenye thamani ya trioni 1.3 katika 66,077 nchi mzima ambazo zimesaidia kubadilisha hali ya maisha ya watanzania wakiwemo wajasiliamali mali na waajiriwa hao na familia zao.

Kamanda amesema kwa kipindi hicho PASS imekuwa daraja muhimu sana katika kuwawezesha wakulima, wavuvi, wadau wa sekta ya misitu, wafugaji na wajasiliamali wengine kwenye mnyororo mzima wa thamani.

Mkutano huo ulienda sanjari na uzinduzi wa kampeni ya kujanisha maisha na programu ya ukuaji wa kijani katika maisha kwa kanda za kaskazini na magharibi.

Akizungumza katika mkutano huo Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Nurudim Babu ambaye aliwakilishwa na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Kisare Makori aliipongeza PASS kwa kuja na mpango wa kukuza uchumi kupitia ajenda ya ukuaji wa kijani shirikishi kama njia bora ya kuchochea kilimo endelevu

Kwa upande wa Mwakilishi wa Mkuu wa mkoa wa Tabora, Ezekiel Mwansasu amezitaka taasisi za fedha kuwa karibu zaidi na PASS ili kufanikisha mipango yake na kuwakomboa watanzania wenye kipato cha chini.

Miongoni mwa walionufaika na taasisi hiyo, Jeremia Ayo wa kijiji cha Mbunguni wilaya ya Arumeru mkoani Arusha amesema wamenufaika na kubadilisha mfumo wao wa maisha kwa miaka 23 iliyopita.

Ayo amesema katika kikundi chao wapo wanufaika zaidi 1000 ambao wameweza kujenga nyumba bora za kuishi, kuanzisha miradi ya kiuchumi na kuwasomesha watoto wao hadi Vyuo Vikuu na Vyuo vya kati na baadhi yao sasa wanajitegemea.




Na Bakari Madjeshi, Michuzi TV
KOCHA  Mkuu wa timu ya taifa ya Tanzania, Adel Amrouche amewaita kwenye Kikosi cha timu hiyo, Walinzi wawili wa pembeni wa Simba SC, Shomari Kapombe na Mohammed Hussein (Zimbwe Jr) ambao aliwaacha katika safari ya Misri kwenye mchezo dhidi ya Uganda (The Cranes).

Katika Kikosi cha Wachezaji 31 walioitwa awali, kuelekea kwenye mchezo huo wa kuwania kufuzu Michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON), Kocha Adel aliwaacha Walinzi hao licha ya kukutana nao na kuteta nao baada ya mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Simba SC dhidi ya Horoya AC kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa Dar es Salaam.

Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam, Rais wa Shirikisho la Soka nchini (TFF), Wallace Karia amesema Kocha Adel amewajumuisha Wachezaji hao kwenye Kikosi hicho cha Stars ambacho kinatarajiwa kucheza mchezo wa nne wa Kundi F la kuwania kufuzu AFCON dhidi ya Uganda, Machi 28, 2023 kwenye dimba la Mkapa.

“Shomari Kapombe na Mohammed Hussein, kwa sasa watakuwa wamejumuika na wenzao kambini kujiandaa na mchezo huo dhidi ya Uganda siku ya Jumamne (Machi 28, 2023) kwenye uwanja nyumbani, Benjamin Mkapa,” amesema Wallace Karia

“Mwalimu tulikuwa naye siku nyingi (miezi miwili nyuma) alikuwa anakuja kuangalia Ligi Kuu hapa nyumbani, kwa ajili ya kusaka vipaji kwa ajili ya kuunda Kikosi cha timu ya taifa, na alipokuja alipewa orodha ya Wachezaji na Wasaidizi wa timu (Taifa Stars),” ameeleza Karia

Hata hivyo, Rais Karia ameeleza kuwa maandalizi kuelekea mchezo huo yamekamilika na timu ipo tayari kwa ajili ya mchezo, amesema licha ya kukabiliwa na mchezo mgumu dhidi ya Uganda ambao ni washindani wakubwa wa Taifa Stars, ameeleza kujipanga vizuri kwa Kikosi hicho ili kujihakikishia mazingira mazuri ya kufuzu AFCON.

Mchezo wa mwisho uliopigwa kwenye dimba la Suez Canal, Ismailia nchini Misri, Taifa Stars ilishinda bao 1-0 dhidi ya Uganda waliokuwa nyumbani, bao hilo lilifungwa na Mshambuliaji Simon Msuva kwenye dakika ya 68’ na hivyo kufikisha alama nne na kuwa nafasi ya pili kwenye msimamo wa Kundi F lenye timu za taifa za Algeria, Uganda na Niger.
Ndege ya Shirika la Ndege la Serikali ya Ufalme ya Saudi Arabia (The Royal Kingdom of Saudi Arabia) ikiwa katika Uwanja cha Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam bara baada ya kutua leo Machi 26, 2023.

Na Avila Kakingo, Michuzi Tv
MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) leo Machi 26, 2023 wamepokea ndege ya Shirika la Ndege la Serikali ya Ufalme ya Saudi Arabia (The Royal Kingdom of Saudi Arabia) yenye uwezo wa kubeba abiria 180 kwa wakati mmoja.

Shirika hilo, linafanya safari za kimataifa za ratiba maalumu katika nchi zaidi ya 100 duniani katika Mabara ya Afrika, Asia, Ulaya na Amerika Kaskazini. Katika bara la Afrika, Tanzania inakuwa miongoni mwa nchi 14 ambazo shirika hili linakuwa na safari za moja kwa moja ambapo kwa kuanzia litafanya safari za JNIA kwenda Jeddah katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha King Abdulaziz.

Akizungumza wakati wa mapokezi ya ndege hiyo katika Uwanja cha Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa (MB.) amesema kuwa ndege hiyo aina ya Aibus 320 itafanya safari zake kutoka hapa nchi kwenda nchini Saudia mara nne kwa wiki na itarahisisha usafiri kwa watanzania na abiria kutoka Tanzania kwenda moja kwa moja nchini Saudi Arabia.

Pia itawarahisishia wasafiri wa nchi jirani kuchagua njia ya usafiri wa moja kwa moja ambao ni nafuu na wa muda mfupi wakiwemo waumini wa dini ya kiislamu wanaokwenda kufanya ibada ya Hijja.

“Leo hii tunashuhudia moja ya matunda ya ziara ya Mheshimiwa Rais aliyofanya nchini Saudi Arabia mnamo Mwezi, Juni 2022. Ziara hiyo imewezesha kuongezeka kwa mashirika makubwa ya ndege ya Kimataifa yanayofanya safari zake nchini ikiwemo shirika hili la ndege la Serikali ya Ufalme ya Saudi Arabia.” Amesema Prof. Mbarawa

Ameongeza kuwa Maamuzi ya Shirika hili ya kuanzisha safari za ndege za ratiba maalum hapa nchini yamechagizwa kwa kiasi kikubwa pia na kuimarika kwa mazingira ya kibiashara na uwekezaji yaliyopelekea uhitaji wa usafiri wa anga wa moja kwa moja kutoka Tanzania kwenda Saudi Arabia

“Kabla ya kuanzishwa kwa safari za ndege za shirika hili, abiria walilazimika kupitia mataifa mengine ili kufika nchini Saudi Arabia ambapo uzoefu unaonyesha walitumia masaa takribani kumi (10) ili kukamilisha safari zao. Hivyo, kwa kutumia Shirika hili, abiria wataweza kusafiri kwenda Jeddah moja kwa moja na watatumia masaa takribani manne na dakika arobaini.” Ameeleza Prof. Mbarawa

Kwa Upande wa Kaimu Balozi wa Saudi Arabia nchini Tanzania, Fardi Al Harbi, amesema ujio wa ndege hiyo kutoka Saudi Arabia kutaongeza shughuli za usafiri wa anga, biashara na utalii kati ya nchi hizi mbili.

“Hii itangangia kwa kiasi kikubwa katika kuimarisha na kuendeleza mahusiano kati ya nchi hizi mbili.”

Amesema kuwa Ujio wa Ndege hiyo hapa nchini utasaidia katika biashara pamoja na mahujaji pamoja na watalii kutembelea maeneo ya utalii katika nchi zote mbili.

Akizungumzia ujio wa ndege hiyo, Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, Mussa Mbura amesema ujio wa ndege hiyo ni matokeo ya maelekezo ya kuongeza mashirika ya ndege hapa nchini.

Kwa mujibu wa takwimu za Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) za mwaka 2022, idadi ya abiria wa kimataifa nchini inaonekana kuongezeka kwa asilimia 55 kutoka abiria 1,694,085 katika mwaka 2021 hadi kufikia abiria 2,618,119 mwaka 2022.

Picha za pamoja.

Viongozi mbalimbali wakipata zawadi mara baada ya kuwasili Ndege ya Shirika la Ndege la Serikali ya Ufalme ya Saudi Arabia (The Royal Kingdom of Saudi Arabia) katika Uwanja cha Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam leo Machi 26, 2023.
Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa (MB.) akizungumza wakati wa mapokezi ya Ndege la Serikali ya Ufalme ya Saudi Arabia (The Royal Kingdom of Saudi Arabia) katika Uwanja cha Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam leo Machi 26, 2023.
Kaimu Balozi wa Saudi Arabia nchini Tanzania, Fardi Al Harbi, akizungumza wakati wa mapokezi ya Ndege la Serikali ya Ufalme ya Saudi Arabia (The Royal Kingdom of Saudi Arabia) katika Uwanja cha Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam leo Machi 26, 2023.
Balozi wa Tanzania nchini Saudi Arabia, Ali Jabir Mwadini akizungumza wakati wa mapokezi ya Ndege la Serikali ya Ufalme ya Saudi Arabia (The Royal Kingdom of Saudi Arabia) katika Uwanja cha Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam leo Machi 26, 2023.
Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, Mussa Mbura akizungumza wakati wa mapokezi ya Ndege la Serikali ya Ufalme ya Saudi Arabia (The Royal Kingdom of Saudi Arabia) katika Uwanja cha Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam leo Machi 26, 2023.

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa (MB.) akisalimiana na baadhi ya wageni waliokuja na Ndege la Serikali ya Ufalme ya Saudi Arabia (The Royal Kingdom of Saudi Arabia) katika Uwanja cha Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam leo Machi 26, 2023.
Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa (MB.) akishirikiana na viongozi mbalimbali kukata utepe kuashiria uzinduzi wa ndege ya Serikali ya Ufalme ya Saudi Arabia (The Royal Kingdom of Saudi Arabia) katika Uwanja cha Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam leo Machi 26, 2023.



Viongozi mbalimbali wakiwa katika picha ya pamoja.




Baadhi ya abiria wakipanda ndege ya Serikali ya Ufalme ya Saudi Arabia (The Royal Kingdom of Saudi Arabia) katika Uwanja cha Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam leo Machi 26, 2023 wakielekea Saudia.


 

WAZIRI  wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa Tuzo ya Umahiri kwa watafiti wanaochapisha matokeo ya tafiti zao katika majarida yenye hafadhi ya juu Kimataifa 'High Impact Factor Journals' iliyofanyika leo Machi 26,2023 jijini Dodoma.

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. James Mdoe,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa Tuzo ya Umahiri kwa watafiti wanaochapisha matokeo ya tafiti zao katika majarida yenye hafadhi ya juu Kimataifa 'High Impact Factor Journals' iliyofanyika leo Machi 26,2023 jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Idara ya Sayansi,Teknolojia na Ubunifu Prof.Maulilio Kipanyula,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa Tuzo ya Umahiri kwa watafiti wanaochapisha matokeo ya tafiti zao katika majarida yenye hafadhi ya juu Kimataifa 'High Impact Factor Journals' iliyofanyika leo Machi 26,2023 jijini Dodoma.

SEHEMU ya Washiriki wakifatilia hotuba ya Waziri   wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof.Adolf Mkenda,akizungumza na waandishi wa habari (hayupo pichani)  wakati wa hafla ya uzinduzi wa Tuzo ya Umahiri kwa watafiti wanaochapisha matokeo ya tafiti zao katika majarida yenye hafadhi ya juu Kimataifa 'High Impact Factor Journals' iliyofanyika leo Machi 26,2023 jijini Dodoma.

WAZIRI  wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda,akizindua Tuzo ya Umahiri kwa watafiti wanaochapisha matokeo ya tafiti zao katika majarida yenye hafadhi ya juu Kimataifa 'High Impact Factor Journals' hafla iliyofanyika leo Machi 26,2023 jijini Dodoma.

 

WAZIRI  wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuzindua Tuzo ya Umahiri kwa watafiti wanaochapisha matokeo ya tafiti zao katika majarida yenye hafadhi ya juu Kimataifa 'High Impact Factor Journals' iliyofanyika leo Machi 26,2023 jijini Dodoma.

Alex Sonna-DODOMA

WAZIRI  wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amezindua tuzo kwa wahadhiri wa elimu ya juu ambao tafiti zao zitachapishwa katika majarida ya juu ambapo chapisho litakalokidhi vigezo na kushinda litapata Sh milioni 5o.

Prof. Mkenda ameyasema hayo leo Machi 26,2023 Jijini Dodoma  wakati wa uzinduzi wa Tuzo ya Umahiri kwa watafiti wanaochapisha matokeo ya tafiti zao katika majarida yenye hafadhi ya juu Kimataifa 'High Impact Factor Journals'.

Prof Mkenda  amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira wezeshi na kuimarisha uwezo wa nchi katika kufanya tafiti na ubunifu unaolenga kuchagiza maendeleo ya uchumi wa viwanda na kuboresha maendeleo ya watanzania.

Amesema juhudi hizi zinajumuisha, pamoja na masuala mengine, kuongeza fedha na kujenga miundombinu ya kisasa ya utafiti na ubunifu sambamba na kuongeza idadi ya rasilimali watu yenye weledi stahiki na morali.

“Katika kuimarisha juhudi hizo na kuhakikisha kwamba nchi yetu inazalisha matokeo ya utafiti yanayoakisi na kujibu changamoto mbalimbali za kijamii na kiuchumi na yenye hadhi ya kimataifa.

“Wizara imeanzisha Tuzo ya kila mwaka kwa watafiti kutoka Taasisi za Elimu ya Juu za Umma na Binafsi nchini wanaochapisha matokeo ya tafiti zao katika majarida yenye hadhi ya kimataifa `High Impact Factor Journals`,”amesema Prof Mkenda.

Prof Mkenda amesema upatikanaji wa washindi wa tuzo hiyo  utazingatia utaratibu na vigezo vilivyoainishwa katika mwongozo wa Kitaifa ambao umezinduliwa  na kuanza kutumika rasmi kushindanisha machapisho yaliyochapishwa ndani ya kipindi cha kuanzia  Juni 1  2022 hadi Mei  31  mwaka huu.

“Tuzo hii itaanza kutolewa kwa machapisho katika fani za Sayansi Asilia na Hisabati na Tiba,”amesema 

Aidha,Mkenda  amesema tuzo hiyo  itajumuisha cheti na fedha taslimu Shilingi Milioni 50 kwa kila chapisho litakalokidhi vigezo na kushinda.

Vilevile, tuzo hiyo itatolewa kwa machapisho yote yanayokidhi vigezo kwa mwaka husika kwa kuzingatia uwezo wa kibajeti. Amesema kwa mwaka huu wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni moja. Amesema wahadhiri watakaohusika na tuzo hiyo ni wale waliofanya utafiti kwenye maeneo ya sayansi asilia, hisabati na tiba na matokeo ya tafiti zao kuchapishwa katika majarida ya juu ya kimataifa.

Prof Mkenda amesema kwa kawaida matokeo ya mtafiti yatachapishwa katika majarida hayo kama dunia itayatambua na kuona kuwa mtafiti amesogeza uelewa wa binadamu katika maeneo ya sayansi na tiba.

Amesema majarida yenye hadhi ya kimataifa yatachanguliwa kwa kwa kuzingatia kigezo cha “Impact Factor”ambacho  kinachoakisi ubora wa machapisho katika Jarida husika.

“Mwombaji lazima awe Mtanzania kutoka katika Taasisi yoyote ya Elimu ya Juu iliyothibitishwa na mamlaka husika nchini mathalan TCU na NACTVET.

“Kila chapisho linalokidhi vigezo na kushinda litapokea Tuzo moja pekee inayojumuisha cheti na shilingi milioni 50; na ikiwa litakuwa limehusisha waandishi wa kitanzania zaidi ya mmoja, kiasi hicho cha fedha kitagawanywa kwa kuzingatia utaratibu ulioainishwa katika Mwongozo wa Tuzo

“Mchakato wa kupata washindi utasimamiwa na Kamati ya Tuzo ambayo itateuliwa na Wizara kwa kuzingatia vigezo na uwiano ulioainishwa katika Mwongozo wa Tuzo,”amesema Prof Mkenda.


Mkuu wa Wilaya ya Gairo ndugu Jabiri Makame amesema Wilaya ya Gairo ni Moja ya Wilaya zilizopendelewa sana katika kipindi Cha 𝗠𝗶𝗮𝗸𝗮 2 𝘆𝗮 𝗨𝗼𝗻𝗴𝗼𝘇𝗶 𝘄𝗮 𝗠𝗵𝗲. 𝗗𝗸𝘁 𝗦𝗮𝗺𝗶𝗮 𝗦𝘂𝗹𝘂𝗵𝘂 𝗛𝗮𝘀𝘀𝗮𝗻, 𝗥𝗮𝗶𝘀 𝘄𝗮 𝗝𝗮𝗺𝗵𝘂𝗿𝗶 𝘆𝗮 𝗠𝘂𝘂𝗻𝗴𝗮𝗻𝗼 𝘄𝗮 𝗧𝗮𝗻𝘇𝗮𝗻𝗶𝗮.

Akizungumza katika Mkutano wa Maadhimisho ya Miaka 2 ya Uongozi wa Rais Samia, DC Makame amesema Wilaya ya Gairo imetekeleza miradi yenye thamani ya zaidi Bilioni 30 katika Sekta zinazogusa maisha ya Wananchi zikiwemo Sekta ya Afya, Maji, Barabara, Elimu, Kilimo na Utawala Bora. Miradi iliyotekelezwa ni pamoja na Mahakama ya Wilaya, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Hospitali ya Wilaya, Vituo 2 vya Afya, Zahanati 8, barabara za lami na zege, madarasa 79, miradi ya Maji Vijiji na mjini nk.

Kwa upande wake Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Gairo Danistan Mwigoha alieleza Mbunge wa Jimbo la Gairo Mhe. Ahmed Shabiby kupitia Ofisi ya Jimbo imetumia zaidi ya milioni 120 kutekeleza miradi ya maendeleo na kwamba Mbunge wa Jimbo hilo anaendelea kufanya jitihada za kutafuta fursa mbalimbali za Maendeleo kwa ajili ya Jimbo la Gairo.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Gairo ndugu Dastan Mwendi naye alieleza kuwa, Rais Samia ameitendea haki Ilani ya Chama Cha Mapinduzi katika Wilaya ya Gairo, kwani Wilaya ya Gairo inapiga hatua za Maendeleo kwa Kasi kubwa katika Sekta mbalimbali za huduma za Kijamii, na kuwataka Watendaji wa Serikali kwenda na Kasi ya Rais Samia ili kukidhi matarajio ya Wananchi.



















NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.

NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohammed Said Mohammed ‘Dimwa’,amesema Chama Cha Mapinduzi haitowavumilia baadhi ya wanachama,makada na watu wanaokwamisha juhudi za Wabunge,Wawakilishi na Madiwani kwa kubeza na kukejeli miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa majimboni.

Kauli hiyo ameitoa wakati wa uzinduzi wa kisima cha maji safi na salama kilichopo shehia ya Karakana Jimbo la Chumbuni,Mkoa wa Mjini Magharibi.

Alisema kuna baadhi ya wanachama wanaonyemelea nafasi za uongozi katika majimbo wameanza kujipitisha kwa wananchi wakitoa kauli zisizofaa za kubeza miradi ya maendeleo inayotekelezwa na viongozi waliopa hivi sasa katika nafasi za ubunge na uwakilishi.

Alieleza kuwa watu wanaofanya hivyo wajue kwamba bado Chama Cha Mapinduzi hakijatangaza mchakato wa uchaguzi hivyo wanachokifanya ni kuvunja kanuni,miongozo ya Chama na sharia za nchi.

Katika maelezo yake Dkt.Dimwa, ameweka wazi msimamo wake kuwa katika uongozi wake atawachukulia hatua kali za kinidhamu watu waotengeneza makundi na safu za kukigawa Chama na kuchonganisha viongozi na wananchi.

“Natumia nafasi hii kukumbusheni kuwa CCM tayari imemaliza uchaguzi wa Chama na kuvunja makundi yote, hivi sasa tuna kundi moja ambalo ni Chama Cha Mapinduzi, na kazi yetu kubwa ni kutatua kero na changamoto za wananchi.”,alisema Dkt.Dimwa.

Kupitia hafla hiyo alimuagiza Mwenyekiti wa CCM Jimbo la Chumbuni,kuhakikisha anawafikisha katika kamati ya usalama na maadili watu wote watakaobainika kuhusika na migogoro,uchochezi na makundi ya kuhatarisha uhai wa chama jimboni humo.

Dkt.Dimwa, aliwasihi viongozi hao wa majimbo kuwa wajibu hoja kwa kutekeleza kwa vitendo ahadi walizozitoa wakati wa kampeni zilizopita mwaka 2020.

Alisisitiza kuwa hatua hiyo itarejesha imani kubwa kwa wananchi katika kuiamini CCM kwenye kuleta maendeleo endelevu.

"Ili CCM iendelee kukubalika na kuaminiwa na wananchi kupewa ridhaa yakuongoza Zanzibar kuna umuhimu mkubwa kwa viongozi wa chama kuwa karibu na wananchi kuwatembelea kusikiliza kero zao,"alisema

Alisema CCM inatambua kuwa huduma ya maji safi na salama ni huduma ya msingi ya kila mkazi wa Zanzibar.

Pia,alisema kuwa katika miaka mitano(2020-2025) CCM iliahidi kupitia ilani yake ya uchaguzi ukurasa wa 243 ibara ya 186 vifungu vidogo vya (a)-(i) kwamba inaielekeza SMZ kuendelea kutimiza azma ya ASP na CCM ya kuhakikisha upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wote.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Chumbuni, Ussi Salum Pondeza alisema kisima cha mwanzo kilikauka tangu mwaka 2008.

Alisema kisima hicho kiliharibika Aprili mwaka 2022 na kusababisha wakazi wa Jimbo hilo la Chumbuni kuhangaika na kukosa huduma ya maji safi na salama.

"Hivyo kutokana na hali hiyo wakazi wa shehia hizi zilizopo katika Jimbo la Chumbuni walikuwa hawapati huduma za maji hivyo nikatumia nguvu zangu nikawaleta wataalamu tukaanza kuchimba kisima hichi kipya,"alisema

Mbunge huyo alisema kisima hicho kilianza kuchimbwa katika kipindi cha January mwaka huu.

Alisema kisima hicho ambacho kimechimbwa hivi sasa kitahudumia shehia nne ikiwemo Masumbani,Banko,Maruhubi na Karakana ikilinganishwa na kisima cha awali ambacho kilikuwa kinahudumia shehia mbili
NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohammed Said Mohammed ‘Dimwa’(aliyevaa koti nyeusi na kanzu nyeupe) na Mbunge wa Jimbo la Chumbuni Ussi Salum Pondeza, akifungua bomba maalum ya mashine ya kisima cha maji safi na salama kushiria upatikanaji wa huduma hiyo katika hafla ya uzinduzi wa kisima hicho huko Chumbuni Mzambarauni, Zanzibar.
NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohammed Said Mohammed ‘Dimwa’(aliyevaa koti nyeusi na kanzu nyeupe), akiwa na viongozi mbalimbali wa Chama wakati akizindua jiwe la msingi la kisima hicho.
NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohammed Said Mohammed ‘Dimwa’(aliyevaa koti nyeusi na kanzu nyeupe),akiwahutubia wananchi wa jimbo hilo mara baada ya kukamilisha zoezi la uzinduzi wa kisima cha maji huko katika jimbo la Chumbuni Zanzibar.

MBUNGE wa Jimbo la Chumbuni Zanzibar  Ussi Salum Pondeza, akitoa ufafanuzi juu ya uchimbaji wa kisima hicho cha maji safi na salama katika hafla hiyo iliyofanyika leo tarehe 26/03/2023.


Top News