JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI

              

 



               

Mkataba wa Afrika wa Usalama wa Usafiri Baharini na Maendeleo (The African Charter on Maritime Security, Safety and Development) umepitishwa katika Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi za Afrika (The AU Extraordinary Summit) uliofanyika tarehe 15 Oktoba, 2016 Lome, Togo. Kupitishwa kwa Mkataba huu kumefuatia makubaliano yaliyofikiwa katika Mikutano ya Kilele ya Wakuu wa Nchi za Afrika iliyofanyika Younde Juni, 2013 na Visiwa vya Shelisheli Februari,2015.
Tanzania imewakilishwa katika Mkutano huo na Mhe. Balozi. Dkt. Augustine P. Mahiga (MB), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa niaba ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye hakuweza kuhudhuria Mkutano huu kwa sababu ya Majukumu mengine ya Kitaifa.
Akihutubia Mkutano huo Balozi Dkt. Mahiga alisema, Mkataba huo ni kati ya nyaraka muhimu zitakazoelimisha kuhusu kutunza amani ya Dunia, usalama na maendeleo katika karne hii ya 21. Alisisitiza kwamba Bara la Afrika liko kati ya bahari kuu mbili yaani Atlantic na Hindi ambazo ni kati ya bahari zilizo na shughuli nyingi sana za usafirishaji duniani. 
Tanzania ikiwa katika nusu ya ukanda wa pwani ya Mashariki na pwani ya Magharibi ya Bahari ya Hindi yenye urefu wa Kilomita 1400, Mkataba huu ambao Balozi Mahiga ametia sahihi kwa niaba ya Tanzania ni muhimu sana hivyo amewasihi wanachama wengine kuhakikisha wanafanya hivyo.
Sambamba na hilo Balozi Dkt. Mahiga amesema Mkataba huu si muhimu tu kwa Afrika kulinda bahari na rasilimali zake bali ni muhimu kwa dunia nzima. Balozi. Dkt. Mahiga ameomba Nchi zote na Mashirika ya Kimataifa kuunga mkono utekelezaji wa mkataba huu. Kufuatia kupitishwa kwa mkataba huu ameiomba Sekretariati ya Umoja wa Afrika kupeleka Mkataba huu kwenye Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na katika Jumuiya ya Kimataifa ili kuweza kutambuliwa.
Aidha, Balozi Mahiga amesisitiza kuwa bahari ni hadhina muhimu si tu ya samaki na gesi bali rasilimali nyinine za thamani kama vile madini ambazo zimekaa tu chini ya bahari hivyo ni jukumu la kila mwana Afrika kuhakikisha analinda rasilimali muhimu tulizo nazo zikiwemo hizi ambazo zinapatikana baharini.
Akimalizia hotuba yake Balozi. Dkt. Mahiga alisisitiza “Hivi karibuni bahari hizi ( Atlantic na Hindi) zitakuwa chanzo muhimu cha nishati, hivyo kusaidia jitihada za  kuleta maendeleo kupitia rasilimali za bahari, naamini mkataba huu utakuwa ni silaha muhimu katika kulinda rasilimali hizi za bahari kwa ajili ya sasa na vizazi vijavyo”. Balozi. Dkt. Mahiga ameusihi Umoja wa Afrika na Wanachama wote kuendelea kuuboresha Mkataba huu na kupitisha viambasho muhimu na hatimaye kuharakisha kuuridhia Mkataba huu ili utekelezaji wake uanze bila kuchelewa.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
Dar es Salaam, 16 Oktoba, 2016.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...