JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MAMBO YA NJE NA
USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI
Mkataba wa Afrika wa
Usalama wa Usafiri Baharini na Maendeleo (The African Charter on Maritime Security, Safety and Development) umepitishwa
katika Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi za Afrika (The AU Extraordinary Summit) uliofanyika tarehe 15 Oktoba, 2016
Lome, Togo. Kupitishwa kwa Mkataba huu kumefuatia makubaliano yaliyofikiwa
katika Mikutano ya Kilele ya Wakuu wa Nchi za Afrika iliyofanyika Younde Juni,
2013 na Visiwa vya Shelisheli Februari,2015.
Tanzania imewakilishwa
katika Mkutano huo na Mhe. Balozi. Dkt. Augustine P. Mahiga (MB), Waziri wa
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa niaba ya Mheshimiwa Dkt.
John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye hakuweza
kuhudhuria Mkutano huu kwa sababu ya Majukumu mengine ya Kitaifa.
Akihutubia Mkutano huo
Balozi Dkt. Mahiga alisema, Mkataba huo ni kati ya nyaraka muhimu
zitakazoelimisha kuhusu kutunza amani ya Dunia, usalama na maendeleo katika
karne hii ya 21. Alisisitiza kwamba Bara la Afrika liko kati ya bahari kuu
mbili yaani Atlantic na Hindi ambazo ni kati ya bahari zilizo na shughuli
nyingi sana za usafirishaji duniani.
Tanzania ikiwa katika nusu ya ukanda wa
pwani ya Mashariki na pwani ya Magharibi ya Bahari ya Hindi yenye urefu wa
Kilomita 1400, Mkataba huu ambao Balozi Mahiga ametia sahihi kwa niaba ya
Tanzania ni muhimu sana hivyo amewasihi wanachama wengine kuhakikisha wanafanya
hivyo.
Sambamba na hilo Balozi
Dkt. Mahiga amesema Mkataba huu si muhimu tu kwa Afrika kulinda bahari na
rasilimali zake bali ni muhimu kwa dunia nzima. Balozi. Dkt. Mahiga ameomba
Nchi zote na Mashirika ya Kimataifa kuunga mkono utekelezaji wa mkataba huu.
Kufuatia kupitishwa kwa mkataba huu ameiomba Sekretariati ya Umoja wa Afrika
kupeleka Mkataba huu kwenye Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na katika
Jumuiya ya Kimataifa ili kuweza kutambuliwa.
Aidha, Balozi Mahiga
amesisitiza kuwa bahari ni hadhina muhimu si tu ya samaki na gesi bali
rasilimali nyinine za thamani kama vile madini ambazo zimekaa tu chini ya
bahari hivyo ni jukumu la kila mwana Afrika kuhakikisha analinda rasilimali
muhimu tulizo nazo zikiwemo hizi ambazo zinapatikana baharini.
Akimalizia hotuba yake
Balozi. Dkt. Mahiga alisisitiza “Hivi karibuni bahari hizi ( Atlantic na Hindi)
zitakuwa chanzo muhimu cha nishati, hivyo kusaidia jitihada za kuleta maendeleo kupitia rasilimali za bahari,
naamini mkataba huu utakuwa ni silaha muhimu katika kulinda rasilimali hizi za
bahari kwa ajili ya sasa na vizazi vijavyo”. Balozi. Dkt. Mahiga ameusihi Umoja
wa Afrika na Wanachama wote kuendelea kuuboresha Mkataba huu na kupitisha
viambasho muhimu na hatimaye kuharakisha kuuridhia Mkataba huu ili utekelezaji
wake uanze bila kuchelewa.
Imetolewa
na:
Kitengo
cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara
ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
Dar
es Salaam,
16 Oktoba, 2016.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...