Na Veronica Simba

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amewakaribisha wawekezaji kutoka Italia, kuja kuwekeza nchini hususan katika sekta ya nishati.

Profesa Muhongo alitoa ukaribisho huo kupitia kwa Balozi wa Italia hapa nchini, Roberto Mengoni, aliyemtembelea Waziri ofisini kwake jijini Dar es Salaam hivi karibuni na kufanya mazungumzo baina yao.

Waziri Muhongo alimweleza Balozi Mengoni kuwa, zipo fursa nyingi za uwekezaji hapa nchini katika sekta ya nishati ikiwemo uzalishaji wa umeme kwa kutumia vyanzo mbalimbali ambavyo alivitaja kuwa ni gesi asilia, makaa ya mawe, jotoardhi, upepo, tungamotaka, mawimbi ya bahari na maji.

Aidha, alitaja fursa nyingine ya uwekezaji kuwa ni katika Bomba la kusafirisha mafuta ghafi la Afrika Mashariki, litakalotoka Hoima Uganda hadi Tanga nchini Tanzania.

Hata hivyo, Profesa Muhongo aliweka bayana kuwa, fursa zote za uwekezaji zitatolewa kwa njia ya ushindani wa wazi.

Awali, akieleza madhumuni ya kumtembelea Waziri; Balozi Mengoni alisema Italia ingependa kuwekeza katika sekta za nishati na madini nchini ili pamoja na mambo mengine, kuendeleza na kuimarisha uhusiano mzuri uliopo baina ya nchi hizo mbili.

Profesa Muhongo alitumia fursa hiyo pia kuiomba Italia, ufadhili wa masomo yanayohusu sekta za nishati na madini katika ngazi ya shahada za uzamili na uzamivu, suala ambalo, Balozi Mengoni aliahidi kulifanyia kazi.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (Kulia) na Balozi wa Italia nchini Tanzania, Roberto Mengoni, wakiwa katika picha ya pamoja, baada ya kikao baina yao.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (katikati), akiwa ameshikana mikono na Balozi wa Italia nchini Tanzania, Roberto Mengoni (kushoto) na Ofisa kutoka Ubalozi huo (kulia), ikiwa ni ishara ya ushirikiano baina ya nchi ya Italia na Tanzania.
Mtaalam kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Jensen Mahavile, akifafanua jambo kuhusu fursa za uwekezaji katika miradi ya umeme vijijini, wakati wa kikao cha Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na Balozi wa Italia nchini Tanzania, Roberto Mengoni (hawapo pichani). Wengine pichani ni viongozi na wataalam wa Wizara na Taasisi zilizo chini yake, walioshiriki kikao hicho.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kushoto), akimsikiliza kwa makini Balozi wa Italia nchini Tanzania, Roberto Mengoni (kulia), wakati wa kikao baina yao hivi karibuni. Kushoto kwa Waziri ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara, Profesa James Mdoe.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...