Klabu ya Rotary ya Oyster Bay pamoja na madaktari na wafanyakazi wa kujitolea wametoa huduma za matibabu kwa wakazi wa Kerege wilayani Bagamoyo. Kambi hiyo ya matibabu imeeefanyika Jumapili tarehe 27 Novemba katika shule ya Msingi ya Kerege.

Vipimo na matibabu vilitolewa bure kwa magonjwa kama vile malaria, upungufu wa damu, kisukari na shinikizo la damu, masikio, pua na koo (ENT), magonjwa ya ngozi, macho pamoja na meno. Huduma nyingine zilizotolewa zilikuwa pamoja na ugawaji wa miwani zilizotolewa kwa watu waliokutwa na matatizo ya macho.
Zoezi la Kambi hiyo ya matibabu bure likiendelea katika mji huo wa Kerege.
Huduma za ushauri kwa wajawazito na vifaa vya kujifungulia vilitolewa bure kwa wajawazito; huduma za ushauri nasaha na upimaji wa UKIMWI pia zilitolewa. Kwa mara ya kwanza, elimu ya usafi na taulo za wanawake zilitolewa kwa wasichana.

Akizungumza katika kambi hiyo, Alfred Woiso, Rais wa Klabu ya Rotary ya Oyster Bay alisema, “Ni furaha yetu kuwa hapa kwa mara nyingine tena na tunafurahi kuona wakazi wa Kerege wamejitokeza kuja kupata huduma hizi. Tumetoa huduma kwa watu waliokuwa na matatizo mbalimbali. Tumeona wagonjwa wengi wenye magonjwa sugu kama kisukari na shinikizo la damu. Inaonekana kuna haja ya kupanua wigo wa huduma zetu kwa vile kuna mahitaji ya huduma za matibabu ya magonjwa mengine.”

Kambi hiyo ya matibabu ilihudhuriwa na wagonjwa wapatao 800 kutoka Kerege na maeneo ya jirani. Kambi hii inayoandaliwa na Klabu ya Rotary ya Oyster Bay imefanyika Kerege kwa mara ya sita sasa kwa lengo la kuwasaidia wakazi wa Kerege kupata huduma za matibabu, wakazi ambao kwa kawaida hawana uwezo wa kumudu gharama za matibabu.

Kambi hiyo ya matibabu imedhaminiwa na Diamond Trust Bank na kuandaliwa kwa ushirikiano na Shree Hindu Mandal Hospital, Vital Supplies, Whitedent, vClick Concepts Inc, MAK Books and Brains, ABACUS Pharmaceuticals, Fazel Foundation na wanachama wa Klabu ya Rotary na Rotaractor.
Zoezi la Kambi hiyo ya matibabu na upimaji bure likiendelea katika mji huo wa Kerege.
Mmoja wa wananchi wa Kerege (kulia) akipima macho katika kambi hiyo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...