Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imetoa agizo kwa wasanii wa hapa nchini kutumia lugha fasaha ya Kiswahili katika kazi zao ili kuitangaza lugha hiyo inayotambulisha Taifa letu.

Agizo hilo limetolewa jana jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Elisante Ole Gabriel wakati akizindua program ya kuuza muziki na filamu kwa njia ya mtandao iliyoandaliwa na Kampuni ya Afroprimiere.

Prof. Gabriel alisema kuwa Tanzania inatambulika Duniani kwa lugha ya Kiswahili hivyo wasanii wana nafasi kubwa ya kuendelea kutumia lugha hiyo kwa ufasaha katika kazi zao wanazofanya ili kukuza lugha ya Kiswahili.

“Wasanii mnafanya kazi zenu kwa Kiswahili ni vyema mkatumia lugha hii kwa ufasaha zaidi lakini pia kuweni sehemu ya mafanikio ya mpango huu ili mfanikiwe zaidi.” Alisema Prof. Elisante.

Aidha amewahakikishia wasanii kuwa Serikali itaendelea kutunza haki za wasanii na kuwaunga mkono katika programu hii ili iwe na faida kwa Serikali katika kupata mapato na wasanii pia kupata faida ya kazi zao. “Kutunza Kazi za wasanii ni jukumu letu, nawahakikishia hakuna atakayekosa faida katika jambo hili kama tutakua pamoja na kushirikiana.” Aliongeza Prof Gabriel.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Afroprimiere ambao ndio waandaaji wa program hiyo Bw. Fredy Ngimba amesema kuwa program yao inalenga kuwasaidia wasanii namna wanavyoweza kufaidika na biashara ya kazi zao mtandaoni.

“Programu hii itawasaidia wasanii kujua idadi kamili ya wanunuzi wa kazi zao mtandaoni na namna ambavyo watagawanya mapato kwa wote wanaohusika kuanzia Serikali, Waandaji, Watengenezaji na wasambazaji wa kazi hizo.”Alisema Bw. Ngimba.

Mapato kwa wote wanaohusika katika kazi hiyo yanaonyesha kuwa Msanii ambaye ndio mwenye kazi yake atapata 50%, Muandaaji 25%, Kampuni ya Mawasiliano 20%, mtengenezaji 08% na Serikali 18%.imeandikwa na Shamimu Nyaki.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Pof.Elisante Ole Gabriel akizungumza na Wasanii (hawapo pichani ) katika uzinduzi wa programu ya kuuza muziki na filamu kupitia mtandao (online)iliyoandaliwa na Kampuni ya Afroprimiere jana Jijini Dar es Salaam.Kushoto ni Kaimu Mkurugenzi maendeleo ya Sanaa Hajjat Shani Kitogo na wa kwanza Kulia ni Bw.Fredy Ngimba Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo.
Baadhi ya Wasanii walioshiriki katika uzinduzi wa programu ya kuuza muziki na filamu kupitia mtandao (online) iliyoandaliwa na Kampuni ya Afroprimiere jana Jijini Dar es Salaam.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...