Kamati ya Katiba, Sheria na Hadhi za Wachezaji ya
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), inatarajiwa kukutana Jumanne
Aprili 18, 2017 kwa lengo la kupitia uamuzi uliofanywa na Kamati ya Usimamizi
na Uendeshaji Ligi Tanzania maarufu kwa jina la Kamati ya Saa 72.
Kwa mujibu wa Katiba ya TFF, Kamati ya Katiba, Sheria na
Hadhi za Wachezaji ya TFF, ina mamlaka ya kutafsiri sheria na kanuni za mpira
wa miguu nchini kama ilivyoainishwa kwenye katiba na sehemu ya utangulizi ya
kanuni za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
Kamati hiyo inakutana kutokana na ombi la timu ya Kagera
Sugar ambayo imeomba kupitiwa upya uamuzi uliofanywa na Kamati ya Saa 72 ambayo
kwa mujibu wa kanuni, ilitoa matokeo mapya ya mchezo kati ya timu hiyo na Simba
uliofanyika Aprili 2, mwaka huu huko Uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera.
Katika mchezo huo, Kagera Sugar ilishinda mabao 2-1,
lakini Simba ilikata rufaa ikidai kuwa Kagera Sugar ilivunja kanuni ya 37 (4)
ya Ligi Kuu ya Vodacom kwa kumchezesha mchezaji Fakhi Mohammed ambaye alidaiwa
na Simba kuwa alikuwa na kadi tatu za njano katika mechi tofauti za Liku Kuu ya
Vodacom. Hivyo, ikaadhibiwa kwa mujibu wa kanuni ya 37 (37) ambayo ilitoa
pointi tatu na magoli matatu kwa Simba.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...