JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA AFYA, MAENDELEO YA JAMII,
JINSIA, WAZEE NA WATOTO
TAARIFA KWA UMMA
AJIRA YA MADAKTARI WA
TANZANIA NCHINI KENYA
Mnamo tarehe 18 Machi
2017 Ujumbe wa Serikali ya Kenya ukiongozwa na Waziri wa Afya Dkt. Cleopa Mailu
uliwasili nchini ambapo ulikutana na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph
Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa madhumuni ya kuomba
kuajiri kwa Mkataba Madaktari wa Tanzania mia tano (500) ili kupunguza uhaba wa
Madaktari nchini Kenya. Mheshimiwa Rais alikubali ombi hilo.
Tarehe 18 Machi, 2017
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ilitangaza nafasi
hizo za ajira kwa Madaktari wa Tanzania kwenda kufanya kazi nchini Kenya. Maombi
hayo yalipokelewa ambapo hadi tarehe 27 Machi, 2017 ambapo jumla ya maombi
takribani 496 yaliwasilishwa. Baada ya kufanya uchambuzi wa maombi haya
ilibainika kuwa, Madaktari 258 walikidhi vigezo vilivyotakiwa kwenda kufanya
kazi nchini Kenya.
Baadhi ya vigezo hivyo ni pamoja na:
·
Uhakiki
wa vyeti vya taaluma na vyeti vya Sekondari.
·
Chuo
alichosoma na mwaka wa kuhitimu masomo.
·
Sehemu
alikofanya mafunzo ya vitendo (Intership) na mwaka wa kuhitimu mafunzo hayo.
·
Uzoefu
wa kazi.
·
Umri
wa mwombaji usizidi miaka 55.
·
Usajili
wa mwombaji katika Baraza la Madaktari la Tanganyika.
·
Asiwe
mtumishi wa Umma, Hospitali Teule za Halmashauri na Hospitali za Mashirika ya
hiyari wanaolipwa mishahara na Serikali.
Wakati Serikali ya
Tanzania ikiendelea kukamilisha utaratibu wa ajira za Madaktari wake nchini
Kenya ikiwa ni pamoja na kutangaza nafasi hizo za kazi na kufanya uchambuzi wa
maombi ya kazi, kuandaa Hati ya Makubaliano kati ya Serikali ya Tanzania na
Serikali ya Kenya kuhusu ajira hizo za Madaktari na Mkataba wa Ajira kwa
Madaktari hao, wananchi (Madaktari) watano wa Kenya waliwasilisha pingamizi Mahakamani
kuitaka Serikali ya nchi yao kusitisha kuajiri Madaktari kutoka Tanzania.
Kwa kuwa ratiba ya
utekelezaji wa ajira hizi za Madaktari ilikubalika na pande zote mbili kuwa iwe
imekamilika ifikapo tarehe 6 Aprili, 2017 na kuwa Madaktari hao wawe tayari kusafiri kwenda
nchini Kenya kati ya tarehe 6-10 Aprili, 2017 na kwa kuwa hadi tarehe ya
taarifa hii Mahakama nchini Kenya haijaondoa pingamizi lililofunguliwa kuhusu ajira
za Madaktari wa Tanzania nchini Kenya, Mheshimiwa
Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameamua kuwa,
Madaktari hao 258 ambao waliokuwa tayari kwenda kufanya kazi nchini Kenya
waajiriwe na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mara moja.
Kufuatia uamuzi huu, Majina ya Madaktari husika na vituo watakavyopangiwa kazi
yatatangazwa katika tovuti ya Wizara www.ehealth.go.tz pamoja na wataalamu
wengine wa Afya 11 walioleta maombi yao na kukidhi vigezo.
Aidha, Serikali ya
Tanzania itakuwa tayari kushughulikia upya ombi la Serikali ya Kenya kupatiwa
Madaktari 500, pale ambapo hakutakuwa na vikwazo vya kupeleka Madaktari wetu
nchini Kenya.
Imetolewa na:
Ummy
A. Mwalimu (Mb),
Waziri
wa Afya, Maendeleo ya Jamii,
Jinsia,
Wazee na Watoto,
Chuo
Kikuu cha DODOMA,
S.L.P.
743,
DODOMA.
19
Aprili, 2017
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...