NA HAMZA TEMBA - WMU

WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe amevipongeza vyombo vya habari nchini kwa mchango wake katika vita dhidi ya ujangili huku akitoa rai kwa vyombo hivyo kuongeza bidii katika kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa uhifadhi endelevu wa maliasili za taifa kwa faida ya jamii iliyopo na vizazi vijavyo.

Prof. Maghembe ametoa pongezi na rai hiyo leo wakati akifungua mkutano wa sita wa mwaka wa wahariri na wanahabari waandamizi wa vyombo vyote vya habari nchini ulioandaliwa na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) jijini Tanga huku kaulimbiu ya mkutano huo ikiwa UTALII WA TANZANIA YA UCHUMI WA VIWANDA.

"Ujangili bado upo, Majangili tumepambana nao kweli kweli, na ninyi wanahabari mmetusaidia sana katika kuhabarisha jamii juu ya matukio ya kukamatwa kwao na hukumu wanazozipata, jambo ambalo limesaidia kujenga uoga kwa watu kushiriki katika vitendo hivyo", alisema Maghembe.
Alisema hofu hiyo pamoja na jitihada za Serikali za kupambana na ujangili imesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza matukio ya ujangili nchini hasa katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita ambapo mizoga ya tembo inayotokana na ujangili imeonekana kupungua kwa kiasi kikubwa ukilinganisha ni miaka iliyopita.

Akizungumzia changamoto ya mifugo kwenye maeneo ya hifadhi nchini amesema sheria za uhifadhi zinakataza watu kuingiza mifugo kwenye maeneo yaliyohifadhiwa kisheria, hivyo ni wajibu kwa wanahabari kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa kutii sheria hizo.  "Ni vema wanahabari wakatumia kalamu zao vizuri kuelimisha jamii juu ya athari za muingiliano wa binadamu, mifugo na wanyamapori".

Alisema wanyamapori wanabeba virusi vya magonjwa mbalimbali ikiwemo homa ya bonde la ufa, ndigana, kifua kikuu, homa za vipindi (brucolosis) na kimeta, Magonjwa ambayo yanaweza pia kuambukiza mifugo na binaadamu wanaoishi karibu na wanyamapori. Alisema kuwa endapo muingiliano huo utaendelea kuwepo kwa muda mrefu unaweza kusababisha mlipuko mkubwa wa magonjwa hayo kwa binaadamu na mifugo hivyo kusababisha vifo vingi kwa wakati mmoja.

Prof. Maghembe alisema kumekuwepo na kisingizio cha kumega maeneo ya hifadhi nchini kwa ajili ya matumizi ya kawaida kutokana na ongezeko la wananchi jambo ambalo sio sahihi na kwamba njia pekee na salama ni kubadili mfumo wa matumizi ya rasilimali zilizopo ikiwepo ya ardhi kwa kutumia sayansi na teknolojia na kuweka matumizi bora ya ardhi kwa kulenga matokeo chanya.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...