WAZIRI
wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe amevipongeza vyombo vya
habari nchini kwa mchango wake katika vita dhidi ya ujangili huku akitoa
rai kwa vyombo hivyo kuongeza bidii katika kuelimisha jamii juu ya
umuhimu wa uhifadhi endelevu wa maliasili za taifa kwa faida ya jamii
iliyopo na vizazi vijavyo.
Prof.
Maghembe ametoa pongezi na rai hiyo leo wakati akifungua mkutano wa
sita wa mwaka wa wahariri na wanahabari waandamizi wa vyombo vyote vya
habari nchini ulioandaliwa na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania
(TANAPA) jijini Tanga huku kaulimbiu ya mkutano huo ikiwa UTALII WA
TANZANIA YA UCHUMI WA VIWANDA.
"Ujangili
bado upo, Majangili tumepambana nao kweli kweli, na ninyi wanahabari
mmetusaidia sana katika kuhabarisha jamii juu ya matukio ya kukamatwa
kwao na hukumu wanazozipata, jambo ambalo limesaidia kujenga uoga kwa
watu kushiriki katika vitendo hivyo", alisema Maghembe.
Alisema
hofu hiyo pamoja na jitihada za Serikali za kupambana na ujangili
imesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza matukio ya ujangili nchini hasa
katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita ambapo mizoga ya tembo
inayotokana na ujangili imeonekana kupungua kwa kiasi kikubwa
ukilinganisha ni miaka iliyopita.
Akizungumzia
changamoto ya mifugo kwenye maeneo ya hifadhi nchini amesema sheria za
uhifadhi zinakataza watu kuingiza mifugo kwenye maeneo yaliyohifadhiwa
kisheria, hivyo ni wajibu kwa wanahabari kuelimisha jamii juu ya umuhimu
wa kutii sheria hizo. "Ni vema wanahabari wakatumia kalamu zao vizuri
kuelimisha jamii juu ya athari za muingiliano wa binadamu, mifugo na
wanyamapori".
Alisema
wanyamapori wanabeba virusi vya magonjwa mbalimbali ikiwemo homa ya
bonde la ufa, ndigana, kifua kikuu, homa za vipindi (brucolosis) na
kimeta, Magonjwa ambayo yanaweza pia kuambukiza mifugo na binaadamu
wanaoishi karibu na wanyamapori. Alisema kuwa endapo muingiliano huo
utaendelea kuwepo kwa muda mrefu unaweza kusababisha mlipuko mkubwa wa
magonjwa hayo kwa binaadamu na mifugo hivyo kusababisha vifo vingi kwa
wakati mmoja.
Prof.
Maghembe alisema kumekuwepo na kisingizio cha kumega maeneo ya hifadhi
nchini kwa ajili ya matumizi ya kawaida kutokana na ongezeko la wananchi
jambo ambalo sio sahihi na kwamba njia pekee na salama ni kubadili
mfumo wa matumizi ya rasilimali zilizopo ikiwepo ya ardhi kwa kutumia
sayansi na teknolojia na kuweka matumizi bora ya ardhi kwa kulenga
matokeo chanya.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...