NA EVELYN MKOKOI – MWANZA 

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu w rais Muungano na mazingira amelipongeza jiji la mwanza kwa hatua iliyochukua ya kutunza mazingira kwa ujenzi wa Dampo na machinjio ya kisasa kwa lengo la kupunguza uharibifu na uchafuzi wa mazingira kutokana na utupaji taka ovyo.

Aidha, amelipongeza jiji hilo kwa maandalizi ya ujenzi wa miundombinu ya dampo la kisasa kama mizani ya kupimia taka, ofisi na maabara ya kemikali katika dampo hilo uliopelekea jiji hilo kufuzu kupata ufadhili kupitia Bank ya dunia licha ya kutumia mapato ya ndani.”Nikiangalia naona mmewekeza kama zaidi ya milioni 700 ambayo mumewekeza kama manispaa ya Jiji la mwanza.” Alisema Mpina.

Mpina aliongeza kwa kusema kuwa kwa jiji la mwanza kufanya hivyo ni hatua kubwa na kulitaka jiji hilo kuendelea na ari hiyo katika suala zima la hifadhi na utunzaji wa mazingira. Mpina pia aliitaka Manispaa hiyo kukamilisha kwa wakati hatua nyingine za ujenzi wa dampo hilo kama vile za Tathmini ya Athari kwa Mazingira na kulipa fidia kwa wananchi na kaya zilizobakia ili kukamilisha upanuzia wa dampo hilo, na kuepuka vipingamizi visivyo vya lazima.

Katika hatua nyingine Mpina pia aliwapongeza wahisani kwa kuiamini serikali ya awamu ya tano katika mambo mengi ikiwa ni pamoja na kuwekeza katika suala zima la hifadhi ya mazingira. “Naamini katika mradi huu unaokuja wa zaidi ya shilingi Bilioni 19.8 miundombinu ya hapa itakuwa ni mizuri na rafiki zaidi kwa mazingira, kikubwa zaidi ni kuwekeza nguvu zetu katika mradi huu na kuhakikisha kuwa unatekelezwa kama ulivyopangwa”. Alisema Mpina.

Wakati huo huo Naibu Waziri Mpina alitembelea Machinjio ya kisasa ya jiji la Mwanza na kujionea ukarabati wa machinjio unahusisha utunzaji wa mazingira ikiwa ni pamoja na ujenzi wa mtambo wa kisasa wa kutibu majitaka yanayotoka katika machinjio hayo ambapo mtambo huo utazalisha pia biagas kwa ajili ya kuzalisha nishati ya umeme na kuzalisha mbolea. Ukarabati huo unahusisha pia ujenzi wa chumba cha kisasa cha kuhifadhia nyama kitakachowezesha wafanyabiashara ya nyama kusafirisha nje ya nchi.

Katika hali isiyo ya kawaida Naibu Waziri Mpina alitembelea kiwanda cha kuchenjua dhahabu cha Senrun Investment kilichopo eneo la Igoma na kusisitiza kiwanda hicho kiendelee kufungwa kutokana na kubainika kuendesha shughuli zake kinyume na Sheria kwa kutokuwa na vibali vya uchenjuaji dhahabu, cheti cha Tathmini ya athari kwa Mazingira na kibali cha matumizi ya kemikali kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali. 
 
“Nasisitiza kwamba kiwanda hiki kiendelee kufungwa kama ambavyo NEMC wamekifunga na nawataka wamiliki kuwasilisha vibali husika ndani ya siku 7 na wasiendelee na uzalishaji mpaka watakapomaliza zoezi la kufanya tathmini ya athari kwa mazingira”. Awali kiwanda hicho kilifungwa na NEMC kufuatia malalamiko ya wananchi wa maeneo hayo kwa kutiririsha maji yenye kemikali, kutoa moshi mkali kutokana na uchomaji wa taka zenye sumu na kutokuwa na vibali muhimu vya kuruhusu uendeshaji wa shughuli za uchenjuaji dhahabu. 
Karakana za kisasa zilizojengwa katika Dampo la jiji la Mwanza. 
Mwenye Kofia Nyeupe Msimamizi wa Dampo la jiji la Mwanza (Site Manager) Bw. Desderius Pole akimuonyesha Naibu Waziri Mpina tokea mbali karakana za kisasa hazipo katika picha zilizojengwa katika Dampo la jiji hilo, kulia ni wana habari kazini. 
Afisa Mazingira wa jiji la Mwanza wa pili kulia Bi Lidya Nyeme, akimuelezea Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira na Ujumbe wake katika picha kuhusu machinjio ya kisasa ya Jiji la Mwanza iliyojengwa kwa ufadhili wa Bank ya Dunia kupitia Mradi wa hifadhi ya mazingira ya Ziwa Victoria (LVEMP) uliyopo chini ya Wizara ya Maji, Naibu Waziri Mpina yupo katika Ziara ya kikazi jijini Mwanza. 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...