Wanatasnia wa filamu na michezo ya kuigiza nchini wameaswa kujua thamani yao na kazi zao katika kulinda maadili na utamaduni wa kitanzania ili kujijengea heshima mbele ya jamii na wapenzi wa kazi zao. Rai hiyo imetolewa leo na Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu nchini Bibi. Joyce Fissoo alipokuwa akizungumza na viongozi wa Kamati ya Matukio, Maadili na Mikataba wa Chama cha Waigizaji Mkoa wa Kinondoni (Tanzania Drama Film Actors Association - Kinondoni) walipotembelea na kufanya kikao katika Ofisi za Bodi ya Filamu Mtaa wa Samora Jijini Dar es salaam.

Bibi. Fissoo alisema baadhi ya wanatasnia ya filamu wanaonyesha mwenendo unaokinzana na maisha na maadili ya kitanzania huku miongoni mwao wakifanya vitendo vinavyodhalilisha utu na heshima hivyo kuitia doa tasnia nzima ya filamu na michezo ya kuigiza.

“Nawapongeza Chama cha Waigizaji kwa kushirikiana na serikali katika kukemea wale wanachama wachache wanao chafua taswira ya tasnia. Ni muhimu kuendelea kuongeza nguvu katika nidhamu, matumizi ya lugha zenye staha, mavazi yanayoonyesha taswira chanya ya taifa letu; hivyo endeleeni kuiunga mkono Serikali katika hatua inazozichukua” alisema Fissoo.

Kwa upande wake Msemaji wa Chama hicho Bw. Masoud Kaftany alisema lengo la kukutana na Bodi ya Filamu Tanzania ni kuwatambulisha viongozi na kamati ya matukio, maadili na mikataba kutoka kwenye chama cha Waigizaji Kinondoni kwa uongozi wa Bodi ya Filamu kama njia mojawapo ya kuendeleza ushirikiano katika tasnia hiyo.

“Kamati yetu inaundwa na wawakilishi 13 wakiongozwa na Mwenyekiti bwana Ahmad Hussein, Katibu bwana Khalifan Ahmed na Msemaji bwana Masoud Kaftany na leo tumekuja Bodi ya Filamu kujitambulisha na kujifunza Sheria, Kanuni na Taratibu zinazotakiwa kufuatwa ili zitusaidie katika utendaji wa kila siku wa kazi zetu” alisema Kaftany.

Kwa upande wake Mjumbe wa Kamati ya Chama hicho Bi. Vanitha Omari ameiomba Bodi ya Filamu kutochoka kutoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wadau wa sekta ya filamu ili waweze kupata uelewa stahiki katika tasnia kwa ujumla.

Chama cha waigizaji wa filamu Mkoa wa Kinondoni ni miongoni mwa vyama vinavyounda vyama vya waigizaji wa filamu taifa na ni chama ambacho kimekuwa mfano katika kutetea maslahi na haki za wanachama wake.
Katibu Mtendaji Bodi ya Filamu Tanzania Bibi. Joyce Fissoo (katikati) akiongoza kikao na viongozi wa Kamati ya Matukio, Maadili na Mikataba wa Chama cha Waigizaji Mkoa wa Kinondoni (Tanzania Drama Film Actors Association-Kinondoni) walipotembelea ofisi za Bodi ya Filamu kuwatambulisha viongozi wa chama hicho kwa uongozi wa Bodi ya Filamu hivi karibuni katika Ofisi za Bodi ya Filamu Mtaa wa Samora jijini Dar es salaam.
Baadhi ya wanachama na viongozi wa Kamati ya Matukio, Maadili na Mikataba wa Chama cha Waigizaji Mkoa wa Kinondoni (Tanzania Drama Film Actors Association-Kinondoni) wakifuatilia taarifa iliyokua ikitolewa wakati wa kikao na Bodi ya Filamu kuwatambulisha viongozi hao hivi karibuni katika Ofisi za Bodi ya Filamu Jijini Dar es Salaam.
Katibu Mtendaji Bodi ya Filamu Tanzania Bibi. Joyce Fissoo (wanne kulia) katika picha ya pamoja na Wanachama na Wajumbe wa Kamati ya Matukio, Maadili na Mikataba wa Chama cha Waigizaji Mkoa wa Kinondoni (Tanzania Drama Film Actors Association-Kinondoni) baada ya kikao na wajumbe hao walitembelea ofisi za Bodi ya Filamu kuwatambulisha viongozi wa chama hicho kwa uongozi wa Bodi ya Filamu hivi karibuni katika Ofisi za Bodi ya Filamu Jijini Dar es salaam.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...