Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imevitaka vyama vya siasa, wagombea, wananchi na watendaji wa uchaguzi kuzingatia na kuheshimu matakwa na masharti ya Sheria za Uchaguzi, Sheria za Nchi na Maadili ya Uchaguzi wakati wa upigaji kura, kuhesabu, kujumlisha kura, na kutangaza matokeo katika uchaguzi mdogo utakaofanyika kesho Jumapili kwenye majimbo ya Ukonga na Monduli na kata 9 za Tanzania Bara.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa NEC, Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Semistocles Kaijage katika risala yake kuelekea uchaguzi huo mdogo unaofanyika kufuatia sababu mbalimbali ikiwamo wabunge na madiwani kujizulu, kufariki, kutohudhuria vikao na kufutwa uanachama.

Jaji Kaijage aliwataka wadau hao wa uchaguzi kushirikiana na Tume kuhakikisha kuwa viashiria vya kuvunjika kwa amani na utulivu vinaepukwa ili uchaguzi utakaofanyika uwe huru, wazi na wa haki.
Mbali na wito huo, Mwenyekiti huyo aliwasihi wapiga kura wote waliojiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura na wanaoishi kwenye maeneo yanayofanya uchaguzi mdogo, kujitokeza kwa wingi kupiga kura ili kuwachagua viongozi wanaowataka wawaongoze kwa kipindi cha takribani miaka miwili ijayo. 

“Wananchi wafanye na kutekeleza zoezi la kuwachagua wawakilishi wao bila hofu, woga, wasiwasi au ushawishi kwani chini ya Kanuni ya 3.1 (b) ya Maadili ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2015, Serikali imepewa wajibu wa kuhakikisha kuwa kuna hali ya usalama, amani na utulivu katika kipindi chote cha Uchaguzi.”, aliongeza Jaji Kaijage na kusisitiza kuwa:

“Ni matumaini ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuwa, hali ya amani na utulivu kwenye maeneo ya Uchaguzi ambayo imekuwepo hadi hivi sasa, itaendelea kudumishwa ili kuhakikisha uchaguzi huu mdogo unafanyika na kumalizika salama kwa ustawi wa Taifa letu.”

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...