Tume ya Taifa ya
Uchaguzi (NEC) imevitaka vyama vya siasa, wagombea, wananchi na
watendaji wa uchaguzi kuzingatia na kuheshimu matakwa na masharti ya
Sheria za Uchaguzi, Sheria za Nchi na Maadili ya Uchaguzi wakati wa
upigaji kura, kuhesabu, kujumlisha kura, na kutangaza matokeo katika
uchaguzi mdogo utakaofanyika kesho Jumapili kwenye majimbo ya Ukonga na
Monduli na kata 9 za Tanzania Bara.
Wito huo
umetolewa na Mwenyekiti wa NEC, Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Semistocles
Kaijage katika risala yake kuelekea uchaguzi huo mdogo unaofanyika
kufuatia sababu mbalimbali ikiwamo wabunge na madiwani kujizulu,
kufariki, kutohudhuria vikao na kufutwa uanachama.
Jaji Kaijage
aliwataka wadau hao wa uchaguzi kushirikiana na Tume kuhakikisha kuwa
viashiria vya kuvunjika kwa amani na utulivu vinaepukwa ili uchaguzi
utakaofanyika uwe huru, wazi na wa haki.
Mbali na wito
huo, Mwenyekiti huyo aliwasihi wapiga kura wote waliojiandikisha kwenye
daftari la kudumu la wapiga kura na wanaoishi kwenye maeneo yanayofanya
uchaguzi mdogo, kujitokeza kwa wingi kupiga kura ili kuwachagua viongozi
wanaowataka wawaongoze kwa kipindi cha takribani miaka miwili ijayo.
“Wananchi wafanye
na kutekeleza zoezi la kuwachagua wawakilishi wao bila hofu, woga,
wasiwasi au ushawishi kwani chini ya Kanuni ya 3.1 (b) ya Maadili ya
Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2015, Serikali imepewa
wajibu wa kuhakikisha kuwa kuna hali ya usalama, amani na utulivu katika
kipindi chote cha Uchaguzi.”, aliongeza Jaji Kaijage na kusisitiza
kuwa:
“Ni matumaini ya
Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuwa, hali ya amani na utulivu kwenye maeneo
ya Uchaguzi ambayo imekuwepo hadi hivi sasa, itaendelea kudumishwa ili
kuhakikisha uchaguzi huu mdogo unafanyika na kumalizika salama kwa
ustawi wa Taifa letu.”
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...