Na Veronica Simba – Dodoma
Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani amesema kwamba, kwa sasa umeme unaozalishwa nchini unatosheleza mahitaji ya wananchi; bali jitihada za kuzalisha umeme mwingi zaidi zinazoendelea kufanywa na Serikali, ni kwa ajili ya matumizi ya baadaye.
Ameyasema hayo leo, Oktoba 9, 2018 wakati akizungumza na Mwekezaji kutoka Kampuni ya Jos’ Hansen ya Ujerumani, Michael Kabourek, aliyemtembelea Waziri ofisini kwake jijini Dodoma, kwa ajili ya majadiliano kuhusu uwekezaji katika sekta ya umeme.
“Mathalani, leo hii tunavyozungumza, tuna ziada ya takribani megawati 213 za umeme. Hii inadhihirisha kuwa umeme tulionao kwa sasa unatosheleza kabisa mahitaji ya nchi; isipokuwa tunaendelea na jitihada za kuzalisha umeme mwingi zaidi kwa ajili ya matumizi ya baadaye,” amefafanua.
Akifafanua zaidi, Dkt. Kalemani amesema kuwa, Serikali, kwa kutambua kuwa mahitaji ya umeme yanaongezeka siku hadi siku; sambamba na malengo ya kuingia kwenye uchumi wa kati kupitia uanzishwaji viwanda; ndiyo sababu inaendeleza jitihada kuhakikisha kunakuwa na umeme mwingi zaidi unaofikia megawati 5000 ifikapo mwaka 2025 kutoka takribani megawati 1500 zinazozalishwa sasa.
 Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (kushoto), akifafanua jambo kwa Mwekezaji kutoka Kampuni ya Jos’Hansen ya Ujerumani, Michael Kabourek (kulia), aliyemtembelea Waziri ofisini kwake jijini Dodoma, Oktoba 9, 2018 kwa ajili ya majadiliano kuhusu uwekezaji katika sekta ya umeme nchini. Katikati ni Afisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Hassani Mwamweta.
 Mwekezaji kutoka Kampuni ya Jos’ Hansen ya Ujerumani, Michael Kabourek (kulia), akifafanua jambo kwa Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (wa pili-kushoto), wakati wa kikao kilichofanyika Oktoba 9, 2018, ofisini kwa Waziri jijini Dodoma, kujadili kuhusu nia yake kuwekeza katika sekta ya umeme nchini. Wengine pichani (kutoka kulia) ni Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Mbadala, Edward Ishengoma, Afisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Hassani Mwamweta na Mtaalam kutoka Wizara ya Nishati, Mhandisi Christopher Bitesigirwe.
Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (kushoto), akiagana na Mwekezaji kutoka Kampuni ya Jos’ Hansen ya Ujerumani, Michael Kabourek, aliyemtembelea Waziri ofisini kwake jijini Dodoma, Oktoba 9, 2018 kwa ajili ya majadiliano kuhusu nia yake ya kuwekeza katika sekta ya umeme nchini.


KUSOMA ZAIDI BOFYA HAPA

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...