Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisoma hotuba ya kuahirisha Mkutano wa Kumi na Tatu wa Bunge jijini Dodoma, Novemba 16, 2018. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

UTANGULIZI
       Mheshimiwa Spika, awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia uzima na afya njema na kutufikisha siku ya leo tunapohitimisha Mkutano wa 13 wa Bunge lako tukufu tuliouanza siku ya Jumanne tarehe 6 Novemba, 2018.

     Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana na kukupongeza kwa kuendelea kuliongoza Bunge hili Tukufu kwa umahiri mkubwa. Niwashukuru pia Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wenyeviti wa Bunge kwa kuendelea kukusaidia katika kutekeleza ipasavyo majukumu ya kuliongoza Bunge lako Tukufu.
      Mheshimiwa Spika, vilevile, niwapongeze Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa kukamilisha shughuli zote zilizopangwa kutekelezwa kwenye Mkutano huu, na kutoa michango mingi mizuri kupitia mijadala ya hoja mbalimbali zilizowasilishwa na Serikali. Nitumie fursa hii kuwahakikishia kuwa, Serikali imepokea michango yenu yenye nia ya kujenga na kuimarisha utendaji wa Serikali na tutaifanyia kazi.

Salamu za Pole

     Mheshimiwa Spika, tarehe 20 Septemba 2018, Taifa lilipokea kwa mshtuko mkubwa taarifa za kuhuzunisha za kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere. Ajali hiyo mbaya iligharimu maisha ya Watanzania wapatao 227.  Aidha, katika kipindi cha Septemba hadi Novemba 2018, wapo Watanzania wenzetu waliopatwa na maafa mbalimbali ikiwemo ajali za barabarani ambazo zimegharimu maisha, kusababisha majeruhi na uharibifu mkubwa wa mali.

    Mheshimiwa Spika, vilevile, mvua iliyoambatana na upepo mkali pamoja na radi iliyonyesha mkoani Geita tarehe 17 Oktoba 2018 ilisababisha vifo vya wanafunzi sita na walimu wawili wa Shule ya Msingi Emaco na kujeruhi wengine 25. Hivyo, nitumie fursa hii kutuma salamu zangu za pole kwa wale wote waliopoteza wapendwa wao Mungu aweke roho zao mahali pema peponi, Amina. Tuendelee kuwaombea uponaji wa haraka kwa waliopata majeraha kwenye ajali mbalimbali. Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu mahala pema peponi. Amina!

Pongezi

     Mheshimiwa Spika, kama unavyofahamu Wabunge wanne walishinda chaguzi ndogo zilizoendeshwa katika majimbo ya Monduli, Ukonga, Korogwe Vijijini na Liwale. Wabunge hao ni Mheshimiwa Julius Kalanga Laizer (Mb.), Mheshimiwa Mwita Mwikwabe Waitara (Mb.), Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava (Mb.) na Mheshimiwa Zuberi Mohamed Kuchauka (Mb.). Hongereni sana Waheshimiwa Wabunge kwa heshima kubwa mliyoipata ya kuaminiwa na wananchi wa majimbo yenu. Nitumie nafasi hii pia kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wanne walioapishwa jana tarehe 15 Novemba, 2018 ambao ni Mheshimiwa James Kinyasi Millya (Mb.), Simanjiro; Mheshimiwa Joseph Michael Mkundi (Mb.), Ukerewe; Mheshimiwa Ryoba Chacha Marwa (Mb.), Serengeti na Mheshimiwa Paulina Philip Gekul (Mb.), Babati kwa kupita bila kupingwa kwenye majimbo yao.

      Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii pia kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri wapya kwa kuaminiwa na kuteuliwa kushika nyadhifa mbalimbali  ambao ni Mheshimiwa Joseph George Kakunda (Mb.), Waziri wa Viwanda Biashara na Uwekezaji; Mheshimiwa Japhet Ngailonga Hasunga (Mb.), Waziri wa Kilimo; Mheshimiwa Mary Machuche Mwanjelwa, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora; Mheshimiwa Constantine John Kanyasu (Mb.), Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii; Mheshimiwa Mwita Mwikwabe Waitara (Mb.), Naibu Waziri Ofisi ya Rais - TAMISEMI na Mheshimiwa Innocent Lugha Bashungwa (Mb.), Naibu Waziri wa Kilimo.

        Mheshimiwa Spika, niwakumbushe Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri wote kuwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wananchi wana matarajio makubwa kutoka kwenu katika kuwaletea maendeleo.  Hivyo, nawaomba tusiwaangushe.

HALI YA USALAMA WA VYOMBO VYA USAFIRI

           Mheshimiwa Spika, wakati naanza kusoma hotuba yangu nimetoa salamu za pole kutokana na ajali mbalimbali zilizohusisha vyombo vya usafiri. Ajali hizo ambazo zimegharimu maisha ya wananchi wengi ni pamoja na kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere.

      Mheshimiwa Spika, kufuatia ajali hiyo Serikali iliunda Tume ya kuchunguza chanzo cha ajali na kutoa mapendekezo yatakayosaidia kuepusha ajali nyingine ya aina hiyo na kubainisha vyanzo vya ajali na watendaji ambao hawakutekeleza wajibu wao ipasavyo. Tayari Serikali imepokea taarifa ya tume hiyo na inaifanyia kazi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...