RAIS Dkt. John pombe Magufuli amewaongoza wakazi wa jiji la Dar es Salaam kuipokea ndege mpya ya pili aina ya Airbus A220-300 na kuwataka Watanzania kuamini kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itaendelea kuwatumia katika kuwaletea Maendeleo.

Akizungumza katika hafla ya upokeaji wa ndege hiyo leo Ijumaa (Januari 11, 2019) Jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli alisema ili kufikia kwa haraka kasi ya kasi maendeleo ya kiuchumi, Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga kutekeleza kwa vitendo dhana ya msingi wa kujitegemea na kupunguza kutegemea misaada kutoka mataifa ya nje.

Rais Magufuli alisema kuwasili kuwasili kwa ndege hiyo ya Airbus A220-300 ni ushuhuda wa nguvu za Watanzania katika kuungana na Serikali katika juhudi mbalimbali za Maendeleo ikiwemo kulipa kodi, jambo ambalo limekuwa likipewa msukumo na Serikali ya Awamu ya Tano katika kuleta Maendeleo ya Watanzania walio wengi zaidi.

“Wakati mwingine misaada inalemaza, hivyo ili nchi iendelee ni lazima tujitegemee na sisi tumeamua kuimarisha Shirika letu la ndege la ATCL, kwa sasa zipo ndege sita na tumepanga kuongeza nyingine mbili ambapo moja aina ya Dreamliner ya pili inategemea kuwasili nchini mwishoni mwa mwaka huu” alisema Rais Magufuli.

Aidha Rais Magufuli alilitaka Shirika la Ndege Nchini (ATCL) kuhakikisha linajipanga kikamilifu katika kuhakikisha kuwa linatoa huduma bora na kuhakikisha kuwa Shirika hilo linajiendesha kibiashara na hivyo kuleta tija na makusudio yanayotarajiwa na Serikali kulingana na Mpango Mkakati uliowekwa na Shirika hilo.

Akifafanua zaidi Rais Magufuli alisema Serikali haitasita kulinyang’anya ATCL ndege hizo iwapo shirika hilo litashindwa kufikia malengo yaliyowekwa na Serikali na hivyo kulitaka Shirika hilo kujipanga kikamilifu ikiwemo kuongeza mtandao wa huduma zake katika vituo vya ndani na nje ya nchi.

Kwa mujibu wa Rais Magufuli, alisema katika kuliongezea nguvu Shirika hilo, Serikali imepanga kutoa ndege mbili zinazotumiwa na Viongozi Wakuu wa Serikali aina ya Focal 28 na Focal 50 kuanza kutoa huduma ya kubeba abiria katika muda ambao ndege hizo zitakuwa hazitumiki na Viongozi hao.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Ndege Nchini (ATCL), Mhandisi Ladislaus Matindi alisema katika kufikia malengo yaliwekwa na Serikali, ATCL imeendelea kutekeleza kwa kasi kubwa kuimarisha mtandao wa huduma katika Shirika hilo kupitia Mpango Mkakati wa Miaka mitano wa Shirika hilo (2017/22) uliolenga katika kuliendesha shirika hilo katika kuongeza faida.

Aliongeza kuwa katika Mpango Mkakati huo, Shirika hilo limepanga kuongeza idadi ya mtandao wa huduma katika vituo vilivyopo ndani nan je ya nchi ikiwemo nchi za Zambia, Afrika Kusini na Zimbabwe pamoja na kuimarisha utoaji huduma katika mikoa yenye idadi kubwa ya wateja ikiwemo Mwanza, Kilimanjaro na Mbeya.

“Kuanzia Januari 16, tutaanza kuboresha huduma za ndege kwa safari za kila siku katika Mji Mkuu wa Serikali kutokana na wingi wa wateja waliopo ambapo hapo awali tulikuwa tukienda mara moja kwa wiki ili kuhakikisha kuwa mji sasa unakuwa kiunganishi na maeneo mengine ya nchi” alisema Mhandisi Matindi.

Alisema mbali na uboreshaji wa huduma za abiria, Shirika hilo limejipanga pia kuhakikisha kuwa linaboresha uwezo wa kusafirisha shehena za mizigo ambapo ndege za Bombadier Q-400 zina uwezo wa kubeba mzigo wa tani 8.6, ndege ya Dreamliner ina uwezo wa kubeba mzigo wa tani 44, na ndege mbili aina ya Airbus ina uwezo wa kubeba tani 19.

Kkwa kwa mujibu wa Mhandisi Matindi alisema kuwa ATCL kwa kushirikiana na Ofisi ya Ubalozi wa Uingereza nchini, imepanga kukutana na wadau mbalimbali wa sekta ya usafiri wa anga ikiwemo watoa huduma na wafanyabiashara ili kuwawezesha kupata fursa mbalimbali ikiwemo masoko ya bidhaa mara baada ya Shirika hilo litakapoanza kupeleka ndege nchini Uingereza.

Naye Balozi wa Canada Nchini, Pamela O'Donnel alisema Serikali ya nchi hiyo itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kuhakikisha sekta muhimu za kiuchumi ikiwemo usafiri wa anga zinapiga hatua kubwa za maendeleo ikiwemo utekelezaji wa miradi mbalimbali ya Maendeleo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...