NCHI zinazokabiliwa na misukosuko na mapigano katika ukanda wa Maziwa Makuu
zahimizwa kutoa nafasi zaidi kwa wanawake katika nyadhifa za uongozi ili
kuwashirikisha katika mchakato wa kuleta amani.
Akizungumza leo Februari 14,2019 Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa katika
eneo la Maziwa Makuu Said Djinnit amezitaka nchi za ukanda huo zinazokabiliwa na
misukosuko na mapigano ya mara kwa mara kutoa nafasi zaidi kwa wanawake
katika nyadhifa za uongozi ili kuwashirikisha katika mchakato wa kuleta amani ya
kudumu kwenye eneo hilo.
Kauli hiyo ameitoa jijini Nairobi, Kenya alipoongoza mkutano wa kimataifa kuhusu
mchango wa wanawake katika suala la kutafuta amani na mapatano katika nchi za
ukanda huo.
Djinnit amesema uchaguzi wa hivi karibuni uliofanyika katika Jamhuri ya
kidemokrasi ya Kongo unaashiria kuna uwezekano wa kufikia hali ya amani na
mapatano katika eneo hilo. Djinnit ameendelea kusema: ''Tunataraji kwamba wakati
huu ambapo Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo imeondokana na mchakato wa zoezi
la uchaguzi basi tunatazamia kuwa wanawake watapewa nafasi katika nyadhifa za
uongozi katika nchi hiyo''.
Amesema wanawake wana ushawishi mkubwa katika kushinikiza amani na mapatano
ukizingatia kwamba akina mama na watoto ndio waathiriwa wakuu katika mataifa
yanayokabiliwa na majanga au vita na migogoro ya kisiasa.
Aliyekuwa Rais wa mpito wa Jamhuri ya Afrika ya Kati, Catherine Samba-Panza pia
alikuwa miongoni mwa washiriki wa mkutano huo wa siku moja uliohudhuriwa pia
na viongozi wanawake wa ngazi za juu kutoka nchi za Maziwa Makuu,
wanadiplomasia pamoja na wawakilishi kutoka mashirika ya kijamii.
Wasemaji katika mkutano huo wamesisitiza umuhimu wa watu kuheshimu haki za
binadamu. Wamekemea vikali vitendo vya dhulma dhidi ya wanawake katika nchi
kama vile Sudan Kusini ambapo kumekuwa na ongezeko la visa vya ubakaji wa
watoto na unyanyasaji wa kijinsia kwa ujumla.
Miongoni mwa nchi zilizowakilishwa kwenye mkutano huo ni pamoja na Burundi,
Rwanda, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo na Jamhuri ya Afrika ya Kati. Pia
wajumbe kutoka Umoja wa Afrika na wawakilishi kutoka shirika la maendeleo ya
Ujerumani GIZ ni miongoni mwa mataifa mengine ya Ulaya.
CHANZO DW.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...