NA K-VIS BLOG/Khalfan Said, Morogoro
SERIKALI imekabidhi rasmi eneo la mradi wa umeme wa maporomoko ya maji ya Mto Rufiji (RHPP), leo Februari 14, 2019 kwa mkandarasi Kampuni ya Arab Contractors kwa pamoja na ile ya Elsewedy  Electric zote kutoka nchini Misri.
 Hatua hiyo sasa inaashiria kuanza kwa kazi ya ujenzi wa mradi huo wa umeme ambao utazalisha Megawati 2,115 ambazo zitaingizwa kwenye dridi ya Taifa na kuifanya Tanzania kuwa na umeme mwingi na wa uhakika.
 Akizungumza  wakati wa kukabidhi mradi huo kwa mkandarasi katika hafla iliyofanyika ndani ya Pori la Akiba la Selous, Waziri wa Nishati, Dk. Medard Kalemani, amesema kuwa hatua hiyo inatokana na uamuzi wa Rais Dk. John Magufuli kwa kusimamia uamuzi wa ujenzi wa mradi huo mkubwa.
 Alisema mradi huo ulibuniwa kwa muda mrefu tangu mwaka 1970 ambapo kazi ya uchambuzi ilifanyika lakini haukutekelezwa kwa sababu ya gharama zake kuwa kibwa.
 "Wakati ule (1970), mahitaji ya umeme yalikuwa megawati 100. Lakini leo mahitaji ya umeme ni makubwa sana. Na ilipangwa kwa wakati ule kutekelezwa kwa awamu ambapo ungeanza na megawati 400, awamu ya pili 800 na baadaye megawati 900. Hatua tuliyofikia leo ndiko serikali ya awamu ya tano inataka ya Tanzania ya viwanda
 "Huu ni mradi wa manufaa miji yote iliyozunguka mradi huu itakuwa kwa kasi sambamba na uzalishaji wa umeme," alisema
 Waziri huyo wa Nishati, alisema kuwa mkandarasi Arab Contractors, atafanyakazi ya kujenga bwawa la umeme ikiwamo kingo za kuta pamoja na kujenga vituo  ya kuzalisha umeme.
 "Ninapenda mtekeleze mradi huu kwa wakati na kwa ufanisi ili kuondoa mashaka kwa watu ambao wenye shaka. Leo mnakabidhiwa eneo la kazi ni matumaini yetu itaifanyakazi hii kwa wakati ili wananchi waweze kunufaika na umeme.

"Na kuanzia leo (jana) wakandarasi msiondoke site nyumba zipo, miundombinu ipo iwe jua, mvua jengeni mradi wakati wote na msiondoke hapa," alisema

Alisema pia kitajengwa kituo cha kupoza na kukuza umeme cha kV 400  na njia za kusafirisha umeme kwa msongo wa kV 400 kutoka eneo la mradi hadi Chalinze kwenda Dodoma na Dar es Salaam na utakamilika mwaka 2022.
MANUFAA YA MRADI
 Dk. Kalemani, alitaja manufaa ya mradi huo ikiwamo kuifanya nchi kuwa na umeme wa uhakika na wa kutosha utakaosaidia maendeleo ya uchumi wa viwanda na maendeleo endelevu ya wananchi.
 Mbali na hiyo pia nchi itakuwa na maji ya uhakika kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji hivyo kuongeza uzalishaji wa mazao na ufugaji kwenye eneo lililo chini ya eneo la mradi wa maporomoko ya Mto Rufiji.
 "Kuboresha shughuli za utalii katika Pori la Akiba la Selous kwa kuwapo mazingira mazuri ya ustawi wa wanyama pori kutokana na uhakika wa maji wakati wote ya bwawa litakalotokana na ujenzi wa mradi.
 "Kuongeza mapato ya nchi kutokana na kustawi kwa shughuli za kitalii katika eneo la mradi. Kuvutia uwekezaji katika sekta ya viwanda na sekta mbalimbali za uchumi kutokana na kuwepo kwa umeme wa uhakika na wa bei nafuu hivyo kupunguza tatizo la ajira.
 "Kupunguza athari za mafuriko ya Mto Rufiji kwa wakazi waliopo maeneo ya Rufiji chini hadi delta ya Mto Rufiji na kuongeza pato la Taifa na lishe kutokana na mazao ya uvuvi," alisema Dk. Kalemani. 
MAKAMU WA RAIS ARAB
 Kwa upande wake Makamu wa Rais wa Kampuni ya Arab Contractors,  Wael Hamdy, alisema umuhimu wa mradi huo si kwa Tanzania tu bali ni kwa Afrika kwa ujumla.
 Alisema kwa niaba ya Serikali ya Misri, watahakikisha wanatekeleza mradi huo kwa si mara ya kwanza kupingwa kwani hata walipoteleleza ujenzi wa Bwawa la Azuan, walipingwa na mataifa mengine lakini Tanzania kupitia Mwalimu Julius Nyerere, aliwaunga mkono Misri.
 "Hata kazi ya kupata zabuni ya mradi huu haikuwa kazi nyepesi lakini tunaamini kwa usimamizi wa Rais Dk. John Magufuli, tunaiona Tanzania ikiwa kwenye mwekeo sahihi. Na katika hili linadhirisha hata mwaka jana nilipofika hapa Tanzania na Rais Abdufatah Al-sis, ninaiona Tanzania leo ikiwa imepiga hatua kubwa hapa ni kazi tu," alisema Hamdy

WIZARA YA FEDHA
Akitoa salamu za Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango, Naibu Waziri wa wizara hiyo, Dk. Ashatu Kijaji, alisema kuwa wao kama wizara ambao ni wadau muhimu kwenye utekelezaji watatoa ushirikiano wa kila aina unaohitajika ili kazi ikamilike kwa wakati.

"Haya matunda ya Serikali ya awamu ya tano sote tunajua wapi tulipotoka, tulipo na tunapokwenda. Na tunajua sasa tupo kwenye utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo ya Taifa Awamu ya pili ambao hadi kufikia mwaka 2025 tunataka kuwa Tanzania inayotekegea uchumi wa kati na wa viwanda. Na utekelezaji wa mradi huu tunaambiwa hakuna viwanda bila umeme na mradi huu sasa unakwenda kulifanya Taifa kuwa na umeme mwingi na wa uhakika zaidi," alisema Dk. Kijaji

DK. MWINUKA
 Awali akitoa maelezo kuhusu mradi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Dk. Tito Mwinuka, alisema kuwa ujenzi huo utajumuisha bwawa kuu aina ya Rollar Compacted lenye uwezo wa kutunza maji takribani mita za ujazo bilioni 34, kituo cha kufua umeme zenye uwezo wa MW 2,115. 
"Aidha patajengwa majengo ya ofisi, karakana, makazi, stoo na huduma za jamii kwa ajili ya uendeshaji wa kituo," alisema
Alisema zabuni ya kumpata mkandarasi wa ujenzi ilipelekea kuipata Kampuni ya ubia ya Arab Contractors ambayo inaundwa na kampuni za Osman A. Osman & Co na Elsewedy Electric zote kutoka nchini Misri.
Mkurugenzi huyo Mtendaji alisema katika kutekeleza mradi huo kutakuwa na mtaalamu mshauri wa mradi kwa ajili ya kuangalia ubora wa utendaji kazi wa mkandarasi kwa kushirikiana na timu ya timu ya wazalendo kwa niaba ya mwenye mradi.
 Alisema baada ya kusainiwa kwa mradi huo kuna mambo ambayo mkandarasi alitakiwa kuyafanya na amekamilisha kwa mujibu wa masharti ya mkataba.
Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani, akibadilishana mawazo na naibu waziri wa Nishati, Mhe.Subira Mgalu, (wapili kulia) Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji, (watatu kulia) na Mkurugenzi Mtedaji wa Shirika la Umeme Tanzania TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka muda mfupi baada ya hafla hiyo.
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani, (katikati) akisindikizwa na manaibu waziri na wakandarasi, akikata utepe ikiwa ni ishara ya kukabidhi rasmi mradi wa ujenzi wa kuzalisha umeme wa bonde la Mto Rufiji leo Februari 14, 2019.
Mratibu wa Mradi wa umeme wa Rufiji Mhandisi Justus Mtolela (waliokaa kulia) na mwakilishi wa mkandarasi  Mhandisi Ahmed Ouda wakisaini mkataba wa makabidhiano ya eneo la mradi tayari kuanza kazi. Hafla hiyo iliyoshuhudiwa na Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani manaibu waziri na viongozi mbalimbali wa serikali ilifanyika eneo la mradi wilayani Rufiji leo Februari 14, 2019.


Mratibu wa Mradi wa umeme wa Rufiji Mhandisi Justus Mtolela(kulia) na Mhandisi Ahmed Ouda, wakionyesha hati hizo baada ya ksuaini.
 Makamu wa Rais wa kampuni ya Elsewedy Electric ya Misri, Mhandisi Wael Hmdy, akitoa hotuba yake
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani akitoa hotuba yake kwa niaba ya Serikali.
Mbunge wa Rufiji Mhe.Mohammed Mchengerwa, akitoa hotuba.
 Dkt. Kalemani akisalimiana na Naibu waziri wake, Mhe. Subira Mgalu, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji, na Naibu Waziri wa Maliasili Costantine Kanyasu, mara baada ya hafla hiyo.



Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka, (kushoto), akijadiliana jambo na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo anayeshughulikia uwekezaji, Mhandisi Khalid James, mara baada ya hafla hiyo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...