*Habari nyingi ni za matukio, za kuikosoa Serikali haziandiki

Na Karama Kenyunko,Globu ya jamii

RIPOTI ya matokeo ya Utafiti kuhusu Ubora wa Maudhui ya vyombo vya habari Tanzania kwa mwaka 2018 unaonesha ni nadra kwa vyombo vya habari kuandika au kutangaza habari zenye kuikosoa Serikali huku pia ikionesha kuwa ubora wa kuripoti habari uko chini na nyingi ni za matukio.

Pia ripoti hiyo inonesha kumekuwepo na dhana kwamba vyombo vya habari vinaripoti zaidi habari zinazotoka katika miji mikubwa ikiwemo ya Dar es Salaam,Dodoma, Mwanza, Mbeya,Arusha,Mjini Magharibi na Kusini Pemba.

Kwa mujibu wa watafiti wa utafiti huo ambao ni Christoph Spurk kutoka Switzerland na Abdallah Katunzi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kupitia Spurk Media Consulting Ltd wamesema vyombo vya habari vinawajibu mkubwa wa kuhamasisha maendeleo kwa kutoa habari zenye weledi, maslahi kwa umma na zenye kuwasamamia wenye mamlaka kuhakikisha wanatenda kulingana na taratibu zilizowekwa.

Hata hivyo wamesema wajibu huo muhimu unaweza kutimizwa na kuendelezwa pale tu vyombo vya habari vinapoweza kuripoti kwa kufuata vigezo vya kitaaluma na kwamba utafiti huo wa ubora wa vyombo vya habari Tanzania mwaka 2018 umechambua ubora wa vyombo vya habari kwa kutazama namna vinavyoripoti habari zao kwa kutumia vigezo maalumu ambavyo vimekubaliwa na wadau wa vyombo hivyo.

Akifafanua zaidi, Mtafiti Abdallah Katunzi amesema jumla ya sampuli 1886 ambazo zinajumuisha habari, makala na maoni kwa upande wa magazeti, habari na vipindi vya redio na televisheni pamoja na posti za blogu na mtandaoni kutoka vyombo vya habari 25 Tanzania Bara na Zanzibar na kwamba vyombo hivyo vinajumuisha magezeti saba , redio za kitaifa tano, redio za mikoani saba, televisheni za kitaifa tatu, televisheni ya mtandaoni moja, blogu moja na mitandao moja.

"Kwa ujumla matokeo yanaonesha ubora wa kuripoti kwa vyombo vya habari nchini uko chini kwenye vigezo vingi vilivyotazamwa kwa upande wa vigezo vya kitaaluma zaidi ya 1/3 ambapo asilimia 36 ya sampuli yote iliyochambuliwa imetumia chanzo kimoja cha habari na kwamba habari habari nyingi za waandishi ni zao la habari za matukio kwa asilimia 60 ikiwa ni ongezeko la asilimia nane ukilinganisha na matokeo ya utafiti wa mwaka 2017, ingawa kuna tofauti kubwa kati ya aina ya habari na vyombo vya habari,"amesema Katunzi.

Ametoa mfano kuwa za magazeti ni zao la habari za matukio kwa asilimia 72 wakati makala zinazozalishwa kwa kutegemea jitihada ya vyombo husika ni kwa asilimia 85 na kwamba upande wa televisheni asilimia 78 ya habari ni zao la habari za matukio wakati asilimia 90 ya vipindi vinazalishwa nje ya mfumo wa kufuata matukio.

Pia amesema kuna tofauti kubwa miongoni mwa vyombo vya habari, gazeti la Jamhuri lililofanya vizuri kwa mwaka 2018 habari zake zinatokana na jitihada za wahandishi kutafuta habari hizo kwa asilimia 63 wakati gazeti la The Gurdian ni asilimia 19 pekee.

Katunzi amesema kuwa ukitazama vigezo vya ukamilifu wa habari matokeo pia siyo mazuri kwa wastani ni asilimia 23 tu ya habari ,vipindi na makala zilizochambuliwa ndio zilikuwa na maelezo ya kwanini habari hizo zimeandikwa(root causes).Wakati asilimia tisa pekee ya sampuli yote ndio imeweza kutoa usuli(back ground) wa habari zilizoandikwa.

Kwa upande wa habari kueleweka kwa walengwa , amesema hali inaridhisha kwani asilimia 56 ya kazi zote zilizochambuliwa zina muundo mzuri wa waandishi huku zikiunganisha sehemu mbalimbali za habari kwa mtiririko mzuri.Hata hivyo bado kuna changamoto kwa vyombo vya habari kuelezea takwimu kwa namna ambayo inamsaidia msomaji au msikilizaji kuzielewa takwimu hizo ni asilimia 25 pekee ya kazi zote ndio imeweza kuelezea takwimu kwa kumrahisishia mlengwa kuzielewa.

Kuhusu maadili, amesema asilimia 42 ya sampuli yote imeshindwa kuwapa nafasi watuhumiwa kujieleza ikilinganishwa na asilimia 60 za mwaka 2017 , magazeti yamezingatia kigezo hicho kwa asilimia 50 huku redio na televisheni kwa asilimia 33 mutawalia. "Kuna tofauti kubwa kati ya redio au televisheni na magazeti na chombo kimoja kimoja cha habari.Kwa ujumla magazeti yamefanya vema kwenye vigezo vingi ukilinganisha na televisheni na redio, magazeti kwenye vigezo vyote kwa asilimia 33.2.

Pia amesema utafiti unaonesha kuwa ni vyombo vya habari vichache ndio vinaandika habari za kukosoa utendaji wa Serikali na katika eneo hilo ni Jamii Forums ndio inamaudhui ya kukosoa utendaji wa serikali.

Kupita utafiti huo inapendekezwa ili kuimarisha ubora wa vyombo vya habari inapendekezwa vyombo hivyo vitumie matokeo ya tafiti hiyo na hasa vikijikita kwenye maeneo ambayo havijafanya vizuri au viko chini ya wastani.Hata hivyo vyombo vya habari vinapaswa kujiimarisha kwenye maeneo kama ujumuishaji wa usuli kwenye habari.

"Sababu za kuandikwa kwa habari husika na kuongeza idadi ya habari ambazo zitachochea utendaji kazi wa Serikali ili kuvisaidia vyombo vya habari kujitathimini vyenyewe, utafiti wa mwaka 2018 umeboresha pima kadi ya ubora wa habari ambayo kwa sasa  redio za mikoani inaonesha matokeo kwa kila kigezo kwa kulinganisha na wastani na alama ya juu.Pia utafiti huu umetayarisha pima kadi nyingine ambayo inaonesha nafasi ya kila chombo,"amesema Katunzi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...