Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi
Lugola (wapili kulia) akiwa ndani ya Kituo Kikuu cha Mabasi cha Msamvu,
mjini Morogoro, wakati alipokuwa anafanya ukaguzi na kupima kilevi kwa
madereva wa mabasi kituoni hapo pamoja na wa malori katika barabara ya
Morogoro-Dodoma. Kulia ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Wilbroad
Mutafungwa.
Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi
Lugola (kulia) akiangalia zoezi la upimaji wa kilevi kwa dereva wa basi
la Kimbinyiko, Omary Sauli (katikati). Dereva huyo hakuwa na kilevi
chochote na aliruhusiwa aendelee na safari yake
Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi
Lugola akiwauliza maswali abiria wa basi la Kimbinyiko kuhusiana na
mwendokasi wa dereva wa basi hilo, na pia kuwapa elimu kuhusiana na
kujua haki zao wanapokuwa safarini. Abiria hao walimweleza Waziri huyo
dereva huyo yupo makini na pia walimshukuru kwa kufanya ukaguzi kwa
mabasi mbalimbali nchini.
Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi
Lugola akitoka ndani ya basi la Kimbinyiko kufanya ukaguzi na kuzungumza
na abiria wa basi hilo, mjini Morogoro, leo. Abiria hao walimweleza
Waziri huyo dereva huyo wa basi hilo yupo makini na pia walimshukuru kwa
kufanya ukaguzi kwa mabasi mbalimbali nchini.
- Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola (kushoto) akizungumza na madereva wa Kituo Kikuu cha Mabasi cha Msamvu, Mjini Morogoro, leo, wakati alipofanya ziara ya kushtukiza kituo hapo kwa ajili ya kukagua na kupima kilevi kwa madereva wa mabasi kituoni hapo. Pia Lugola aliwapima madereva wa malori barabara kuu ya Morogoro Dodoma. Wapili kushoto ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Wilbroad Mutafungwa. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
…………………………..
Na Felix Mwagara, MOHA, Morogoro.
WAZIRI wa Mambo ya Ndani, Kangi
Lugola amefanya operesheni kubwa ya kukagua na kupima ulevi wa pombe kwa
madeveva wa mabasi na malori mjini Morogoro, leo.
Lugola pia alizungumza na abiria
wa mabasi hayo, pamoja na viongozi wa madereva waliopo stendi kuu ya
mabasi Msamvu, mjini humo, ambapo walimwelezea kero mbalimbali
zinazowakabili.
Ukaguzi wa mabasi na malori hayo
ulifanyika barabara kuu itokayo Dodoma kuja Morogoro-Dar es Salaam
ambapo Waziri huyo akiwa na Kamanda wa Polisi Mkoa huo (RPC), Mkuu wa
Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa huo (RTO), alisimamisha vyombo hivyo
vya moto vilivyokuwa vinaingia Mizani iliyopo eneo la Kihonda, nje
kidogo ya Mji wa Morogoro.
Akizungumza na madereva, kondakta,
wapiga debe na abiria mara baada ya kufanya ukaguzi huo, Lugola alisema
ni wajibu wake kufanya hivyo katika hatua ya kupunguza kwa kasi ajali
mbalimbali zinatokana kwa uzembe wa madereva nchini.
“Mimi ni Waziri wa vitendo,
nikiagiza nataka nitekelezwe, na pia nikiahidi lazima nilifuatilie,
niliwaambia nitakua nakuja kufanya ukaguzi muda wowote ambao hamuujui,
na ninafanya hivi kwa lengo moja tu, kuhakikisha sheria za usalama
barabarani zinafuatwa ikiwa ni hatua ya kumaliza kupunguza au kumaliza
kabisa ajali za barabarani hapa nchini,” alisema Lugola.
Aliongeza kuwa, kwasasa ajali
zimepungua nchini, hasa Mkoa wa Morogoro, kwasababu ya askari wa usalama
barabarani kufanya kazi zao kiweledi, na pia madereva kufuata sheria za
usalama barabarani.
Lugola aliwataka madereva nchini,
kuacha uendeshaji wa mashindano, kuwa na leseni na pia kuhakikisha
wanapokuwa barabarani wanakua makini kwasababu ya kuwabeba abiria au
mizigo mbalimbali wanayoisafirisha sehemu mbalimbali nchini na nje ya
nchi.
“Madereva wa mabasi na malori
ambao nimefanikiwa kuwapima kilevi leo, ambao wasiopungua sita,
sijawakuta na kilevi, wapo makini na hii inaleta nguvu na imani kuwa
madereva wanaelewa na kuzingatia sheria za usalama barabarani, na pia
ndani ya mabasi niliyokuwa nayakagua nimezungumza na abiria wakaniambia
madereva wanaendesha vizuri na pia niliwakuta wamevaa mikanda, naamini
safari yetu ya kuondoa ajali za barabarani tunazidi kufanikiwa,” alisema
Lugola.
Wakizungumza kwa wakati tofauti
katika stendi kuu ya mabasi, madereva walilipongeza Jeshi la Polisi Mkoa
wa Morogoro, kwa usimamizi mzuri ambao umewaunganisha na kuwafanya
waifurahie kazi wanayoifanya.
Dereva Juma Rashidi wa basi
linalosafiri kutoka Ifakara kuja Morogoro, alisema wanajisikia furaha
kubwa kwa uongozi mpya wa Jeshi la Polisi ulioletwa Mkoani Morogoro hivi
karibuni.
“Naomba niseme ukweli, RPC na RTO
hakika wanatuongoza vizuri, hakuna kero za ajabu kama zamani, tupo huru
kufanya kazi zetu, hii inaonyesha viongozi hawa wanataka tufanye kazi
ili tuweze kupata riziki zetu kwa njia halali bila usumbufu wa
kusumbuana kama ulivyokuwa siku za nyuma,” alisema Rashidi.
Lugola alifanya ziara katika kituo
hicho, na baadaye kutoka nje ya kituo hicho kuyakagua mabasi na malori,
mara baada ya kumaliza ziara yake aliyoifanya Wilayani Kilosa ya
kutatua migogoro ya ardhi ya wananchi wa Tarafa ya Kimamba wilayani
humo, juzi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...