Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, TAMISEMI anayeshughulikia Afya Dk. Dorothy Gwajima amesimamisha majukumu ya uongozi wajumbe nane wa timu ya uendeshaji na usimamizi huduma za afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni Mkoani Singida kwa kushindwa kuwajibika kikamilifu katika kutekeleza wajibu wao wa msingi.
Kufuatia hali hiyo, amewataka waendelee na majukumu yao ya kitaaluma na si majukumu ya uongozi hadi hapo itakapoelekezwa vinginevyo.
Naibu Katibu huyo ameyasema hayo leo wakati akikagua utendaji kazi wa watoa huduma za afya katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Mkoani Singida.
Pamoja na hayo, Dk.Gwajima amemuagiza Mganga mkuu wa mkoa wa singida Dk.Victorina Ludovick kushirikiana na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri kuteua timu ya mpito hadi hapo uchunguzi wa kina wa tuhuma za uzembe utakapofanyika kwa ajili ya hatua zaidi.
Pia ameagiza timu iliyosimamishwa kutoa maelezo ndani ya siku 7 kwanini walishindwa kusimamia kikamilifu utendaji kazi wa kituo hicho na kwa nini wasivuliwe majukumu ya uongozi jumla.
Vilevile, amemtaka mganga mkuu wa mkoa wa singida na timu yake nao kutoa maelezo kwa nini wameshindwa kubaini uzembe wa uwajibikaji wa timu ya usimamizi na uendeshaji huduma halmashauri ya wilaya hiyo na kwa nini nao wasiwe sehemu ya kuchangia tatizo.
Dk. Gwajima ameitaka timu ya afya Mkoa kutoondoka Manyoni hadi changamoto zote zinazohitaji hatua za haraka zifanyiwe kazi na atoe taarifa Ofisi ya Rais Tamisemi ambayo itarejea kwa ukaguzi wa kina.
Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anayeshughulikia afya, Dkt. Dorothy Gwajima akizungumza na wajumbe wa kamati ya uendeshaji afya ya Mkoa wa Singida wakati alipofanya ziara katika wilaya ya Manyoni
Baadhi ya wajumbe wa kamati ya uendeshaji afya ya wilaya ya Manyoni na Mkoa wa Singida wakimsikiliza Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Dkt Dorothy Gwajima jana mjini Manyoni.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...