Na Karama Kenyunko, Michuzi TV
WALIMU wanne, raia wa Kenya, wanaofundisha shule ya msingi na Sekondari ya Kings na Mtanzania mmoja, wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na shtaka la kufanya kazi nchini bila ya kuwa na kibali.
Akisoma hati mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Augustine Rwizile, wakili wa serikali Faraji Nguka, amewataja washtakiwa hao kuwa ni.Esrom Maina, (45), Ruth Njuguna (30), Joseph Kuria (30), Charles Sakawa (32) na mtanzania Stella Bizulu (44).
Imedaiwa kati ya Septemba 2018 na Machi 18, 2019 huko katika shule ya msingi na Sekondari ya Kings iliyoko eneo la Goba ndani ya Wilaya ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam, washtakiwa hao raia wa Kenya walikutwa wakifanya kazi ya ualimu katika shule hiyo bila ya kuwa na kibali kutoka idara ya Uhamiaji.
Katika shtaka la pili imedaiwa, siku na mahali hapo mshtakiwa Bizulu, akiwa kama Meneja wa shule hiyo, aliwaajiri walimu hao bila ya kuwa na kibali cha kufanya kazi nchini kutoka Uhamiaji.
Hata hivyo, washtakiwa wamekana kutenda makosa hayo na wameachiwa kwa dhamana hadi Mei 15, ambapo upande wa mashtaka unatarajiwa kufanyia mabadiliko hati ya mashtaka.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...