Mkurugenzi wa Masoko na Uhusiano wa UTT AMIS, Daudi
Mbaga, akizungumza na waandishi wa habari (hawako pichani)

**********************

Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya UTT AMIS inayomilikiwa na Serikali kupitia
Wizara ya Fedha na Mipango, imeanzisha huduma mpya ya
Mfuko wa Hati Fungani ‘Bond Fund’ ili kuiwezesha jamii iweze
kuzifikia fursa za uwekezaji na kujikomboa kiuchumi.

Kuanzishwa kwa mfuko huo kumeongeza idadi ya mifuko na
kufikia sita yote ikisimamiwa na kampuni hiyo iliyoanzishwa
mwaka 2013 ikichukua jukumu ya usimamizi wa Mifuko ya
Uwekezaji wa Pamoja kutoka kwa Dhamana ya Uwekezaji
Tanzania (UTT).

Akiuzungumzia mfuko huo, Mkurugenzi wa Masoko na
Uhusiano wa UTT AMIS, Daudi Mbaga, alisema utatoa fursa
kwa wawekezaji wadogo, wakati kuzifikia fursa za uwekezaji
zilizokuwa zikifikiwa na wawekezaji wachache, wakubwa.

Alifafanua kuwa, baadhi ya bidhaa hizo zinaeleweka kirahisi
ambapo namna ya kuzifikia, kuwekeza ni rahisi lakini wakati
mwingine hazitoi faida shindani kwa wawekezaji.

Alisema mfuko huo utaondoa changamoto ambazo huwakuta
wawekezaji kwenye soko la fedha ambalo lina bidhaa nyingi
zilizobuniwa ili kukidhi mahitaji tofauti ya watumiaji.

“Mbali ya Mfuko wa Hati Fungani, UTT AMIS inasimamia
mifuko mingine ya uwekezajiambayo ni Mfuko wa Umoja,
Wekeza Maisha, Watoto, Kujikimu, Mfuko wa Ukwasi.

“Kuanzishwa kwa Mfuko wa Hati Fungani kumetokana na
mahitaji ya wawekezaji pamoja na uchambuzi wa bidhaa za
kifedha zilizoko kwenye soko la mitaji kwa sasa,” alisema.

Mbaga alisema mfuko huo utawekeza kwenye hati fungani
zilizoorodheshwa katika soko la hisa kwa asilimia 90, asilimia
10 itakuwa kwenye uwekezaji wenye ukwasi mkubwa.

Lengo ni kuwawezesha wawekezaji wanaohitaji kuchukua fedha
kutokana na uwekezaji wao waweze kufanya hivyo, kumfanya
mwekezaji achague kama anapenda kukuza mtaji au kupokea
gawio kila mwezi, kila miezi sita kulingana na hitaji lake.

Alisema kampuni hiyo pia inatoa huduma ya usimamizi wa mali
za kifedha ili kukidhi mahitaji maalum kwa wawekezaji binafsi
wa kipato cha kati, cha juu na taasisi.

Aliongeza kuwa, baadhi ya wawekezaji hasa wadogo ni vigumu
kuwekeza katika baadhi ya bidhaa kwenye soko la fedha, Mfuko
wa Hati Fungani umeratibiwa ili kuondoa changamoto hizo.

“Mwekezaji anapata faida sawa na wawekezaji wakubwa,
akihitaji fedha anauza baadhi ya umiliki wake kwenye mfuko
kwa utaratibu rahisi bila kupoteza faida aliyoipata.

“Mfuko pia unawafaa wawekezaji wakubwa kwani ina faida
shindani, gharama ndogo za kuwekeza, ukwasi wa kutosha,
usalama wa mtaji, hatari ndogo za uwekezaji,” alifafanua.

Alisema mfuko huo hutoa fursa kwa wawekezaji kuwekeza,
kushiriki katika masoko ya mitaji, kufaidika na uwekezaji huo,
umeanzishwa ili kutoa fursa kwa wawekezaji wa kipato cha
chini, kati na kipato cha juu.

Mbaga alisema watu binafsi, kampuni, taasisi, vikundi rasmi
wanaweza kushiriki katika uwekezaji kwenye mfuko huo, lengo
ni kuwafanya wawekezaji wawe na ushiriki mpana kupitia
uwekezaji wa vipande, kuhamasisha utamaduni wa kuweka
akiba kupitia hati fungani na masoko ya fedha.

Mfuko huo unatoa fursa ya uwekezaji rahisi wa muda mrefu
kwa wawekezaji wanaopenda kuwekeza ili kukuza mtaji, kupata
gawio kila mwezi au baada ya miezi sita kama anavyohitaji.

“Kimsingi Mfuko wa Hati Fungani una mipango miwili ya
uwekezaji ili kukidhi matakwa tofauti ya wawekezaji, kuna
mpango wa kukuza mtaji, gawio kila mwezi na gawio kila baada
ya miezi sita.

“Mpango wa kukuza mtaji, gawio la mara kwa mara
halitatolewa kwa wawekezaji badala yake faida iliyopatikana
itarudishwa kwenye uwekezaji wa awali kwa kununua vipande
vitakavyonunuliwa kwa bei ya wakati huo.

“Mpango huo utawafaa wawekezaji wanaohitaji kuweka akiba
kwa malengo maalum mfano kujenga nyumba au wafanyakazi
wenye kipato na wangependa kuwa na fedha ya akiba kama
dharura itatokea au kwa matumizi ya baadae wanaweza
kuchagua mpango wa kukuza mtaji,” alisema.

Mbaga alifafanua kuwa, wawekezaji katika mpango huo
wanaweza kuuza kiasi chochote cha uwekezaji kama watakidhi
vigezo ya mfuko vinavyohusu uuzwaji wa vipande.

Mpango wa gawio kila mwezi hutokana na mahitaji ya kifedha
ya mwekezaji na anavyochagua kwenye fomu ya maombi ya
kuwekeza kwenye mfuko.

Wawekezaji ambao wanahitaji kuchukua faida kila mwezi
mfano wastaafu wanaopata fedha zao za mkupuo, kuwekeza
kwenye mfuko wanashauriwa kupokea gawio kila mwezi ili
wapate kipato cha kuishi bila kupoteza fedha walizopata.

Mbaga alisema wawekezaji wengine wanaopata fedha nyingi
kwa mara moja mfano wachimba madini wadogo, wanaweza
kuchagua kupata gawio kila mwezi ili waweze kuendesha
shughuli zao bila kuathiri mtaji walioupata.

Pia wawekezaji watakaojiunga na mpango huo wanaweza kuuza
vipande kidogo au vyote ili mradi wawe wamekidhi vigezo vya
mfuko vinavyohusu uuzwaji wa vipande vya mfuko.

Wawekezaji wanaopata fedha nyingi kwa msimu kama
wakulima wa mazao mbalimbali, wanaweza kuchagua gawio la kila miezi sita ili waweze kupata fedha wakati wa kuandaa mashamba yao, kulima na kuvuna ili waweze kuendesha
shughuli zao, kufuata msimu bila kupoteza mtaji.

Akizungumzia gharama za kuwekeza, Mbaga alisema hakuna
gharama yeyote wakati wa kujiunga au kujitoa kwenye Mfuko
wa Hati Funganui, wawekezaji wataruhusiwa kununua, kuuza
vipande kwa thamani halisi ya kipande itakayokuwepo.

“Wawekezaji wote wa ndani na nje ya Tanzania kama Sheria ya
Soko la Mitaji na Dhamana inavyoruhusu, wanaweza kuwekeza
kwenye mfuko huu,” alifafanua.

Kuhusu ununuzi wa vipande, alisema vinaweza kununuliwa siku
yoyote ya kazi isipokuwa kipindi cha kufunga vitabu ambacho
hakitazidi siku saba za kazi.

Alisema kuanzia Septemba 16, mwaka huu hadi Oktoba 16,
mwaka huu, itakuwa kipindi cha mauzo ya awali hivyo ni vizuri
Watanzania wakachangamkia fursa hiyo.

Kiwango cha chini kitakuwa sh. 50,000 na thamani halisi ya
kipande itakuwa sh. 100 ambapo maombi ya kununua vipande
yanaweza kuwakilishwa katika tawi lolote la Benki ya CRDB;
ofisi za madalali waliosajiliwa wa Soko la Hisa la Dar es
Salaam; Ofisi za Shirika la Posta au Wakala yoyote
atakayeteuliwa na UTT AMIS.

“Uwekezaji katika mfuko huu kwa wawekezaji walio nje ya
Tanzania, awasiliane na ofisi za madalali waliosajiliwa wa Soko la Hisa la Dar es Salaam au ofisi za UTT AMIS ili kupata taarifa na muongozo zaidi.

Anaongeza kuwa, thamani ya mwanzo ya kipande itakuwa sh.
100. Thamani ya kuuza na kununua kipande itakuwa sawa na
thamani halisi ya kipande bila gharama yoyote.

Kiwango cha chini kitakuwa sh. 50,000 na hakuna ukomo
kwenye kiwango cha juu, hiyo ni fursa kwa kila Mtanzania
ambapo baada ya muda wa mauzo ya awali, mwekezaji anaweza
kuwekeza kuanzia sh. 5000, mara nyingi kadri awezavyo.

Malipo ya mauzo ya vipande yanaweza kufanywa kwa fedha
taslimu au hundi ya benki itakayolipwa kwenye akaunti ya
Mfuko wa Hati Fungani iliyopo Benki ya CRDB.

“Wawekezaji wanaweza kwenda kwenye tawi lolote la Benki ya
CRDB na kufanya malipo. Pia malipo yanaweza kufanyika kwa
kupitia M-Pesa, Tigo Pesa, Airtel Money,” alisema.

Mbaga alisema kiwango cha chini cha uwekezaji wakati wa
mauzo ya mwanzo kwa Mpango wa Kukuza Mtaji ni vipande
500. Kwa kuwa thamani ya mwanzo ya kipande ni sh. 100,
thamani ya chini ya vipande, mauzo itakuwa sh. 50,000.

Kuhusu mpango wa gawio kila mwezi, kiwango cha chini cha
uwekezaji wakati wa mauzo ya mwanzo kwa mpango wa gawio
kila mwezi ni vipande 100,000, thamani ya mwanzo ya kipande
sh. 100, thamani ya chini ya vipande katika mauzo itakuwa sh.
10,000,000.

Mpango wa gawio kila miezi sita, kiwango cha chini cha
uwekezaji wakati wa mauzo ya mwanzo kwa Mpango wa gawio
kila miezi sita ni vipande 50,000, thamani ya mwanzo kwa
kipande sh. 100, thamani ya chini ya vipande katika mauzo
itakuwa sh. 5,000,000.

Alitoa wito kwa Watanzania wote ndani na nje ya nchi
akiwahimiza wawe sehemu ya uwekezaji katika mfuko huo
mpya kwani una faida nyingi, hawapaswi kuwa na hofu.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...