Makamu wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan akikagua miti iliyopandwa
wakati wa kampeni ya kukijanisha Dodoma katika eneo la Mzakwe jijini Dodoma
ikiwa sehemu ya ufuatiliaji wa ukuaji wa miti hiyo.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Mkurugenzi wa
Jiji la Dodoma Bw. Godwin Kunambi wakati wa ziara ya ukaguzi wa miti iliyopandwa
wakati wa kampeni ya kukijanisha Dodoma. Wengine katika picha ni Mkuu wa Wilaya ya
Dodoma Bw. Patrobas Katambi na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Mhandishi
Joseph Malongo
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipata maelezo kutoka kwa
Mwakilishi wa Wakala wa Misitu Tanzania Kanda ya Kati Bi. Teddy Yoramu juu ukuaji wa miti iliyopandwa katika eneo la
Mzakwe jijini Dodoma wakati wa kampeni ya Kuifanya Dodoma ya Kijani.
Lulu Mussa na Monica Sapanjo
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amesema azma ya kuifanya Dodoma
kuwa ya Kijani iko pale pale.
Hayo yamesemwa leo mara baada ya
kutembelea shamba la miti lililopo katika eneo la Mzakwe katika Kambi ya Jeshi
la Makutupora Jijini Dodoma, ikiwa ni ufuatiliaji wa Kampeni aliyozindua mwaka
2017 ya kuifanya Dodoma kuwa ya kijani.
Makamu wa Rais ameupongeza
uongozi wa Kambi ya Jeshi ya Makutupora, Wakala wa Misitu Tanzania na Watendaji
wa Ofisi yake kwa kuhakikisha miti iliyopandwa mwezi Desemba 2017 inastawi.
“Vitabu vya dini vinasema Moja
kati ya sadaka endelevu ni kupanda miti, miti hii imekuwa na kustawi kwasababu
ya jitihada zenu za kuimwagilia na kuitunza, msikate tamaa, endeleeni na kazi
hii njema ambayo matokeo yake yanaonekana ikiwa ni pamoja na kuimarika kwa
mifumo ya hali ya hewa ambayo huimarisha shughuli za kilimo na maendeleo ya
viwanda.” Alisisitiza Makamu wa Rais.
Nae Mkuu wa Kambi ya Jeshi ya
Makutupora Luteni Kanali Festo Mbanga amesema kuwa miti 2300 ilipandwa tarehe 21/12/2017 na kati ya hiyo miti 2076
imekuwa na kustawi ikiwa ni sawa na asilimia 90.3 ya miti yote iliyopandwa.“Katika miti iliyooteshwa awali
baadhi haikuota, hivyo tumefanya jitihada za kuirudishia, tumepanda takriban
miti 300 ya ziada” alisema Luteni Kanali Mbanga.
Katika hatua nyingine Makamu wa
Rais ameagiza Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) kuhakikisha tafiti zinakamilika
mapema kutoka katika sampuli ya udongo iliyochukuliwa ili kubaini aina ya miti
inayostawi katika eneo hilo na Jiji la Dodoma kwa Ujumla.
Kampeni ya Kukijanisha Dodoma
ilizinduliwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe
21/12/2017 katika eneo la Mzakwe Jijini Dodoma ambapo miti 2300 ilipandwa siku
hiyo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...